Nakumbuka mwaka 2001 mama alipokuja kunitembelea wakati ule nikiwa bado mwanafunzi katika Chuo Kikuu cha California, Los Angeles (UCLA). Alishangaa sana alipoona utitiri wa wazungu (chokoraa) wasio na makazi wakiomba pesa mabarabarani. Alisema kwa mshangao "kumbe kuna wazungu masikini!"
Watu wengi pia wakisikia njaa moja kwa moja wanafikiri kwamba nchi inayozungumziwa ni lazima iwe ya "ulimwengu wa tatu". Kinachowajia akilini ni picha za vile vitoto vya Kiethiopia vilivyokondeana huku viking'ong'wa na mainzi vikiwa tayari kukata roho kwa ajili ya njaa. Kumbe hata hapa Marekani njaa ipo!
Ripoti ya Wizara ya Kilimo ya Marekani iliyotolewa juzi imeshawangaza watu wengi. Ripoti hiyo inasema kwamba kuna njaa hapa Marekani na mwaka jana Wamarekani wapatao 49,000,000 waliathirika na njaa au hawakuwa na chakula cha kutosha. Hii ni sawa na kusema kwamba kwa kila Wamarekani sita, kulikuwa na Mmarekani mmoja ambaye hakuwa na chakula (cha kutosha)
Kama inavyotegemewa watu wengi wanaoathirika na njaa ni masikini (ambao kutokana na siasa za kitabaka, kibaguzi na kinyonyaji za muda mrefu mimi nadhani wengi wao watakuwa ni Wamarekani Weusi na wahamiaji kutoka Amerika ya Kusini). Inashangaza kidogo kuona kuwa nchi tajiri kuliko nchi nyingine yo yote hapa duniani nayo inakumbwa na tatizo la njaa. Pengine picha hiyo juu itabidi tuifanyie mabadiliko ili kuakisi uhalisia huu mpya: njaa si tatizo la Afrika peke yake!
Rais Obama ameahidi kwamba serikali itaongeza misaada zaidi kwa watu masikini. Isome taarifa hiyo fupi hapa.
Mechi hii ilichezwa tarehe 5/11/2009. Wenye jezi nyekundu ni New Mexico University (NMU) na wenye jezi nyeupe ni Bringham Young University (BYU)
Huyu mchezaji korofi jina lake ni Elizabeth Lambert wa NMU. Cha ajabu ni kwamba pamoja na "vituko" vyote hivi hakupewa kadi nyekundu. Hata hivyo ameshafukuzwa katika timu hiyo.
New Mexico, pamoja na Elizabeth Lambert wao, walilazwa 1-0 na hivyo kutolewa katika mashindano hayo.
Jana (Novemba 17, 2009) kulikuwa na makala nzuri katika gazeti la New York Timesjuu ya ufisadi wa Teodoro Nguema Obiang ambaye ni mtoto wa raisi wa miaka mingi wa Equatorial Guinea - Teodoro Obiang Nguema Mbasogo. Inaaminika kwamba Teodoro Nguema Obiang ambaye pia ni waziri wa misitu na kilimo wa Equatoria Guinea ndiye anaandaliwa kuchukua madaraka ya uraisi baada ya baba yake kuachia madaraka. Mambo chomozi katika makala hiyo ni haya:
Equatorial Guinea inashika nafasi ya tatu katika utoaji wa mafuta barani Afrika ikitanguliwa na Naijeria na Angola. Mwaka 2007 pekee, Equatorial Guinea ilijipatia dola bilioni 4.8 kutokana na mauzo yake ya mafuta.
Paradoksi ni kwamba zaidi ya robo tatu ya wananchi wa Equatoria Guinea ni masikini hohehahe kabisa wanaoishi kwa pato la chini ya dola 1 kwa siku!
Wakati huo huo, mtoto huyu wa rais ambaye bado ana miaka 38 tu ni tajiri wa kutupwa na ni wazi kwamba utajiri huo ameupata kwa kupitia rushwa na ufisadi. Mfano mali zake za kifahari hapa Marekani – bila kutaja akaunti zake za Uswisi na utajiri wake mwingine ni kama ifuatavyo:
(7) Huja kupumzika Marekani zaidi ya mara tatu kila mwaka na kila anapokuja huja na pesa taslimu zaidi ya dola 1,000,000 tena bila kuwajulisha watu wa uhamiaji. Hili ni kosa la jinai kwa sheria za Marekani lakni kwa vile Marekani ndiye mnunuzi mkuu wa mafuta ya Equatorial Guinea, maofisa wa uhamiaji humfumbia macho.
Kwa hivyo:
(8) Ukiwa na mafuta, Marekani itakuruhusu ufanye cho chote unachotaka – hata kama ni kuvunja sheria zake! Ukijifanya jeuri wanakuja kuchukua mafuta yako kwa nguvu (muulize Saddam Hussein atakwambia)
Kwa ufisadi huu kweli, Afrika tutaweza kuendelea? Kinachoumiza moyo ni kuona kwamba umma wa Afrika, pengine kutokana na ukosefu wa elimu ya kweli pamoja na umasikini bado umelala na unaruhusu raslimali na utajiri wake uliopindukia kimo kufaidiwa na akina Teodoro Nguema Obiang wachache. Inasikitisha sana! Tazama hii clip hapa chini juu ya “vichaa wa Afrika"
Ni wazi kwamba hivi sasa mashindano ya urembo ni biashara kubwa sana ndiyo maana yametanda kila kona kuanzia taifa, mikoa, wilaya, tarafa, kata na pengine muda si mrefu yatafika ngazi ya vijiji na hata familia!. Japo mashindano haya yanajumuisha watu wa kila aina wakiwemo watoto wadogo (bofya hapa), kwa kiasi kikubwa vigezo vinavyotumika ni vile vya Kimagharibi ambako ili mwanamke awe "mrembo" ni lazima awe mwembamba hasa hata kama ni ule wembamba wa kiutapiamlo!
Kimsingi hii ni kinyume na dhana ya jumla ya uzuri tuliyokuwa nayo sisi Waafrika ambapo mwanamke wa kwelikweli aliyekuwa akisifika alikuwa ni yule tipwatipwa, mwenye umbo mkatiko (vijana wanaita umbo namba 8), matako makubwa na miguu minene iliyosanifiwa (wenyewe wakiita miguu ya bia a.k.a usafiri wa uhakika!).
Wembamba kwetu sisi ulikuwa ni dalili ya maradhi na ukosefu wa lishe bora (unamkumbuka Clementine katika diwani ya Wimbo wa Lawino?). Wakati huu tulikuwa bado hatujajiingiza sana katika maisha ya deko na kula vyakula vya "kisasa" vilivyokuzwa kisayansi na kushindiliwa makemikali na sumu za kila aina. Kwa hivyo kansa na magonjwa mengine tunayoambiwa sasa kwamba yanasababishwa na unene hayakuwa tatizo sana kwetu. Sasa mambo yamebadilika! Soma makala ya Profesa Mbele kuhusu suala hili hapa.
Inavyoonekana wanawake tipwatipwa, baada ya kuona kuwa wanapigwa dafrau, nao wameamka na kuanza kufanya mashindano yao ya "urembo" pamoja na kufungua vilabu vyao wenyewe (gonga hapa na hapa). Hapa chini ni picha chache za mashindano ya aina hii ambayo nimeambiwa kwamba yalifanyika kule California na kwamba baadhi ya washiriki walikuwa ni Watanzania! (Mdau aitwaye Kessy anayeishi Las Vegas alihudhuria onyesho hili na ndiye ameniletea picha hizi - Asante Bwana Kessy)
Tanzania mashindano kama haya yapo? Kama yapo yanatazamwaje na wanajamii? Kweli Vodacom watakubali kumwaga mamilioni yao kwa mashindano kama haya?
Inaonekana madawa ya kuongeza nguvu kwa wenye VVU yana athari nyingi, zikiwemo usahaulifu, maumivu ya neva na kuzeeka mapema. Isikilize ripoti hii hapa chini. Tangu hapo kinga ni bora kuliko kuponya ati!
Mimi sivuti na lengo langu hapa siyo kuwatetea wavuta sigara. Wanasayansi wameshathibitisha kwamba uvutaji wa sigara ni tabia ya hatari inayoua mamilioni ya watu kila mwaka kutokana na saratani ya mapafu na magonjwa mengine yanayoathiri mfumo wa upumuaji. Kutokana na sababu hii uvutaji wa sigara umepigwa marufuku karibu katika kila kona ya dunia. Sehemu zingine zimefikia hatua ya kutunga sheria zinazowabana wavuta sigara kutovuta hata wakiwa majumbani mwao. Mwezi uliopita chuo kikuu cha Florida kilipitisha sheria ambayo inapiga marufuku uvutaji wa sigara katika maeneo yote ya chuo – ndani na nje. Sijui wavuta sigara watafanyeje!
Swali langu ni hili: mbona tumekomalia sana sigara utafikiri kwamba uvutaji ndiyo tabia pekee-angamizi? Mbona tabia zingine za hatari kama unywaji wa bia (ambao pia, mbali na matatizo mengine, umeshathibitishwa kuwa kisababishi kimojawapo kikuu cha aina mbalimbali za saratani na hasa zile za matumbo) hatuzikomalii kama uvutaji sigara? Vipi kuhusu ulaji wa nyama hasa zile “nyekundu” ambao nao pia umeshathibitishwa kwamba ni hatari kwa afya? Wavuta sigara wanaonewa?
Mimi ni mmoja kati ya watu wasiopenda tabia za kinafiki za kujifanya kuchukia tabia moja angamizi na kukumbatia zingine za aina hiyo hiyo. Ndiyo maana huwa sielewi mtu anaponiambia eti ameamua kuacha kula nyama ili kulinda afya yake na wakati huo huo anazitandika bia sawasawa, kuvuta sigara na hata kuwa “kiwembe”.
Ni mawazo yangu tu. Pengine mwanafalsafa Kitururu angeweza kusema ninachojaribu kukisema hapa kwa ufasaha zaidi!
Wasikilize watafiti hapa wakijadili athari za ulaji wa nyama, uvutaji wa sigara na unene wa futufutu (obesity) kwa afya.
Katuni hii imenikumbusha mambo mawili: Kwanza suala la unene. Kitamaduni unene ulikuwa ni jambo la kujivunia na sidhani kama ulikuwa na madhara makubwa kama tunavyoambiwa sasa. Kila mtu alikuwa na ndoto ya kunenepa na vitambi vilionekana kama ishara ya kufanikiwa kimaisha. Watu walikuwa wanafanya kazi sana na tulikuwa tunakula vyakula vya kiasili - siyo kama sasa ambapo utandawazi umetuvuruga kabisa. Soma hapa,hapa na hapa kuhusu hili suala.
Pili: tabia yetu ya kutukuza wazungu, uzungu na vitu vyao vyote. Japo utawala wao uliisha, kisaikolojia jamaa bado wametuminya kweli kweli! Niliwahi kulalamika kuhusu suala hili hapa. Natumaini hatutafikia hii hatua aliyofikia huyu "Mswahili" mwenzetu kwenye katuni.
Igeni mfano wa Mtoto wa Dandu, Saida Karoli na Mr Ebbo!
Niliwahi kuandika kwa kifupi juu ya matumizi ya Kisukuma katika nyimbo za Mtoto wa Dandu. Katika maakala hii fupi (ambayo imetoka katika gazeti la Kwanza Jamii la leo 10/11/2009), ninatoa wito kwa wasanii wa kizazi kipya kuiga mfano wa Mtoto wa Dandu, Saida Karoli na Mr Ebbo na kuimba katika lugha zao za mama au hata kutia vionjo vya "kikabila" katika nyimbo zao. Kwa kufanya hivi watakuwa wanatoa mchango wao chanya katika vita vinavyoendelea duniani kote kujaribu kuzitetea lugha za kienyeji ambazo ziko katika hatihati ya kuangamizwa na utandawazi. *****************************************************************************
Wanamuziki wa Kizazi Kipya – Tumieni Lugha Zenu za MamakamaAlivyofanya Mtoto wa
Dandu (Cool James)
Na Dkt. Masangu Matondo Nzuzullima
James Maligisa Dandu a.k.a Mtoto wa Dandu a.k.a Cool James a.k.a Ng'wanamalia a.k.a CJ Massive a.k.a Ng'wanawapelana a.k.a Nzokaihenge alikuwa na kipaji cha hali ya juu katika muziki. Ndiyo maana muziki wake ungali unapendwa sana miaka saba sasa tangu aage dunia kwa ajali ya gari tarehe 27/8/2002. Sikupata bahati ya kumwona lakini yeye pamoja na Saida Kalori na Mr Ebbo pengine ndiyo waimbaji wa kizazi kipya ambao kwa kiasi kikubwa wameweza kuzitukuza lugha zao za mama katika nyimbo zao - na hivyo kutupilia mbali ile dhana kwamba kizazi kipya hakiwezi kuguswa na nyimbo zenye ladha ya kikabila. Mtoto wa Dandu japo hakuimba katika Kisukuma moja kwa moja kama afanyavyo Saida Karoli, hapa na pale hakuisahau lugha yake ya mama iliyomkuza na kumlea kule Mwanza (Kisukuma). Hapa ni baadhi ya mifano tu ya matumizi ya Kisukuma katika nyimbo za mwanamuziki huyu mashuhuri aliyeondoka akiwa bado mchanga.
Jina lake mara nyingi alipenda kujiita Nzokaihenge yaani nyoka mwenye makengeza (nyoka makengeza). Alikuwa akijiita pia Ng'wanawapelana yaani mtoto mwenye hasira. Ni kawaida ya Wasukuma kujisifu na hapa ndicho alichokuwa akikifanya Mtoto wa Dandu. Ati, umeshawahi kuona nyoka mwenye makengeza maishani mwako? Unadra wa nyoka wa aina hii ndiyo ujumbe aliokuwa akitaka kuuwasilisha. Kipaji chake cha kipekee katika muziki kilikuwa nadra na muziki wake unaonyesha hivyo mpaka leo. Alipenda pia kujiita Ng'wanamalia - mtoto wa Maria. Hii inaonyesha kwamba pengine jina la mama yake ni Maria (Wasukuma hawana sauti " r" na hivyo mara nyingi huitamka kama "l" - kinyume na Wakurya)
Korasi mashuhuri inayosikika katika nyimbo zake nyingi inasema hivi:
Nimeshakuwa mtu wa thamani (heshima) Hata nikienda ugenini siwezi kukalia gogo Inabidi nipewe kiti kizuri cha kukalia
Inavyoonekana pia alikuwa ni mtu wa kutoa shukrani. Katika baadhi ya nyimbo zake anaonekana akimsifia na kumshukuru Jumanne Kishimba - tajiri mkubwa kule Mwanza na mmiliki wa duka kubwa la Imalaseko Supamaketi jijini Dar es salaam. Anasema hivi:
Jumanne Kishimba Ulinamoyo gwape giti buluba Hangi okumuka mpaga Bulaya
Tafsiri
Jumanne Kishimba Una roho nyeupe mithili ya pamba Tena umeshajulikana mpaka Ulaya
Akijisifu kidogo kama ilivyo kawaida ya Wasukuma anasema hivi:
Mtu mwenye akili haelemewi na mzigo (msemo wa Kisukuma) Nimezindikwa na (madawa ya) nyoka mwenye makengeza
Huyu ndiye Mtoto wa Dandu ambaye hakuusahau utamaduni wake. Huyu ndiye Nyokamakengeza ambaye hakuionea aibu lugha yake ya mama. Huyu ndiye Mtoto wa Maria ambaye hakuuonea aibu Usukuma wake. Huyu ndiye Cool James ambaye alikuwa anatambua kwamba asingeweza kuwa “cool” bila kuwa na utamaduni wake mwenyewe.
Hebu fikiria kama wanamuziki wengi wa kizazi kipya wangeiga mfano wa Saida Karoli, Mr Ebbo na Mtoto wa Dandu, wakaimba nyimbo katika lugha zao za mama (Saida Karoli - Kihaya) au kuingiza vipengele vya lugha zao za mama katika nyimbo zao kama Mtoto wa Dandu (Kisukuma) na Mr Ebbo (Kimasai). Hatua hii ingesaidia sana kukikumbusha kizazi hiki kilichopumbazwa na “usasa” kwamba lugha zao za mama zipo, zina hadhi kama lugha nyingine yo yote na zina manufaa ya kimatumizi hata katika ulimwengu huu wa kisasa. Kwa hivyo dhana ya kwamba lugha hizi ni za kizamani, zimeshapitwa na wakati na hakuna sababu ya kujifunza au kuzizungumza tena haina ukweli wo wote. Ingefurahisha kama nini kama wanamuziki hawa wangetimiza wajibu huu wa kitamaduni na kuziunga mkono lugha zetu za asili katika wakati huu zinapopita katika mikikimikiki ya kudharauliwa na kuonwa kwamba hazifai tena.
Kimsingi huu ni wito wangu kwa waimbaji wa kizazi kipya - tumieni lugha zenu za mama katika nyimbo zenu. Kwa kufanya hivyo mtakuwa mnatoa mchango wenu wa thamani sana katika kuzipa uhai lugha zenu zilizowakuza na kuwalea, lugha ambazo zimo hatarini kufa baada ya vizazi vichache vijavyo kama mtaendelea kuzidharau, kuzionea aibu na kuziona kuwa hazina faida wala nafasi katika ulimwengu wa kisasa.
Mungu aendelee kumpumzisha salama Mtoto wa Dandu a.k.a Cool James a.k.a Ng'wanamalia a.k.a Ng'wanawapelana a.k.a Nzokaihenge a.k.a CJ Massive. Muziki wake kwa hakika utadumu!
Kwa watu wengi wa nchi za Magharibi mbwa ni sehemu ya familia na ana haki sawa na memba mwingine ye yote katika familia. Mbwa anaweza kuwa na bima ya afya na hata kuachiwa urithi; na anapofariki basi familia nzima huomboleza na kumzika kwa gharama kubwa.
Ili kuvutia waumini wapya, hivi karibuni makanisa kadhaa hapa Marekani yameanzisha misa maalum kwa ajili ya mbwa. Misa hizi zinadumu kwa nusu saa ambapo mbwa huombewa wakiwa wamejilaza vitandani huku wakifaidi vitafunwa mbalimbali. Kwa habari zaidi kuhusu habari hii gonga hapa.
Kwetu sisi Waafrika jambo hili linaonekana kama vile utani na sijui Wakristo wana maoni gani kuhusu misa za aina hii. Kazi kweli kweli!
(2) Kama ni lazima upigane, zingatia siri hii. Ukiona unazidiwa - mtegee mpinzani wako anaporusha ngumi na wewe rusha hapo hapo tena kwa haraka ya kufumba na kufumbua. Hii ina matokeo matatu: Kwanza ngumi yake inaweza kukupata kwanza na kukufletisha kabla ya kwako haijatua usoni mwake (epuka hili lisitokee). Pili - ngumi yako inaweza kumpata kwanza na kumfletisha kabla ya kwake haijatua kidevuni mwako (hakikisha hili linatokea). Tatu - ngumi yake na yako zinaweka kutua kwa wakati mmoja na wote mkafletishana (na hii siyo mbaya sana). Nilifundishwa siri hii zamani sana. Tazama video hapa chini (dakika 1:18).
Mbali na kuwa chanzo kikuu cha magonjwa ya moyo, watafiti sasa wanasema kwamba unene ukiwemo ule wa futufutu (obesity) ni kisababishi kikubwa cha aina mbalimbali za kansa. Kwa mfano, watafiti sasa wanasema kwamba:
Unene unasababisha asilimia 49 ya kansa za mfuko wa uzazi, ikifuatiwa na asilimia 35 ya kansa za matumbo. Unene pia unasababisha asilimia 28 ya kansa za kongosho (pancreatic cancer), asilimia 24 ya kansa za figo, asilimia 21 ya kansa za kibofu cha mkojo, asilimia 17 ya kansa za matiti na asilimia 9 ya kansa za utumbo mkubwa (colorectal cancer)
Mbaya zaidi - watu wanene wanaongoza kwa kufa na kansa kwa sababu mara nyingi wanapopata kansa, kansa zao huwa hazitibiki kwa urahisi kama za wenzao wembamba
Mimi nadhani kwamba utafiti huu haukuzingatia sababu zingine zinazosababisha kansa yakiwemo mazingira na mfumo wa maisha ya watu. Nyumbani tuna/tulikuwa na watu wanene lakini kutokana na tabia ya watu kufanya kazi sana pamoja na kula vyakula vya kiasili (ambavyo havijabadilishwa kisayansi ikiwemo kutiwa mahomoni ya bandia, mbolea kali na madawa mengine) hata Shirika la Afya Duniani linakiri kwamba Afrika lilikuwa ni bara lenye wagonjwa wachache kabisa wa kansa. Na halafu utandawazi mpya ukaja.
Leo hii tumebadilisha maisha yetu, tunakula vyakula vile vile tunavyoletewa kutoka nchi za Magharibi na mfumo wetu wa maisha umebadilika. Matokeo yake sasa kuna mripuko wa kansa za kila aina na unene - jambo ambalo miaka michache tu liliyopita ilikuwa jambo la kujivunia - sasa linaonekana kuwa ni jambo la hatari! (Tazama pia hapa na hapa)
Isome ripoti kamili hapa na tazama video fupi ya CNN kuhusu jambo hili muhimu hapa.
Pengine hili ni swali la kipuuzi lakini imebidi niliulize kutokana na kisa kilichonipata jana.
Baada ya kutoka kazini nilipita dukani kununua mboga na nikaona maua waridi (roses) mazuri sana. Dazeni moja ilikuwa inauzwa dola 6.99 tena bado freshi kabisa na yamefungwa na kurembwa vizuri. Bei ya kawaida kwa maua kama haya ni dola 13.99 - 29.99.
Basi nikanunua dazeni moja ili kumpelekea mama watoto wangu.
Nilipotoka nje nikakutana na mwanaume Mmarekani mweusi ambaye alikuwa ameambatana na wanawake wawili.
Wale wanawake wakanisifia kwa kusema "Nice roses. She is going to be very happy today"
Yule mwanaume yeye akanitupia swali "Bro, what did you do?" Wale wanawake wawili wakaanza kucheka.
Ilinichukua muda kidogo kumwelewa lakini nilipopambazukiwa nilielewa alikuwa anamaanisha nini: mtu unamnunulia maua umpendaye wakati umemkosea na unataka kuomba msamaha. Wakati huo nilikuwa karibu na gari langu na sikupata muda wa kumjibu muuliza swali ambaye tayari alikuwa ameshaingia dukani.
Katika kipindi kimoja cha televisheni niliwahi kusikia wanasaikolojia wakisema kwamba mwanaume anayetembea nje ya ndoa/penzi ana uwezekano mkubwa zaidi wa kumnunulia mke/mpenzi wake "orijino" maua kutokana na kusutwa na dhamiri "sense of guilty". Wanasaikolojia hawa walitoa ushauri kwa wake/wasichana kufanya uchunguzi mara moja kama waume/wapenzi wao wataanza kuwapa zawadi na hata kuwanunulia maua wakati si kawaida yao. Hii inaweza kuwa ni matokeo ya ule msuto wa dhamiri.
Kule usukumani, ilikuwa lazima kumnunulia umpendaye zawadi - ndogo au kubwa - kulingana na uwezo wako. Kanga, hereni, viatu, "chachandu"- kitu cho chote ambacho kingemfanya ajisikie kwamba unampenda na kumjali. Nadhani, mbali na kuhongeresha, maua (waridi) pia yanatimiza lengo lilelile kama hizi zawadi za Kisukuma.
Kwa wanaume: Kwa nini mnanunua maua?
Kwa wanawake: Kama mpenzi/mume hana kawaida ya kukuletea zawadi/maua na mara moja anaanza kufanya hivyo, utajisikiaje?Ni kweli utaingiwa na wasiwasi?
Wakati mwingine sisi tulioko ughaibuni Kiswahili kipya kinatupiga chenga. Mnamaanisha nini siku hizi mnaposema eti Kanumba amefulia? Natumaini si tusi (la nguoni) au neno baya!
Profesa mmoja mwanaume ambaye pia alikuwa mkuu wa idara mojawapo hapa chuoni ameachia ngazi kwa tuhuma za kufanya mapenzi na wanafunzi wake.
Inasemekana kwamba alikuwa nao wengi kwa mpigo na mpaka sasa wasichana watatu wameandika barua kuelezea jinsi walivyolaghaiwa naye.
Alikuwa akiwatumia wanafunzi wake picha zake za uchi kwa kutumia simu yake ya mkononi.
Alikuwa akilipwa dola 106,000 kwa mwaka.
Wanafunzi wake wa zamani wamtetea na kusema kwamba ni mmojawapo wa maprofesa wazuri sana - ingawa alipenda mno kuongelea mambo yake binafsi pamoja na familia yake.
Swali: Vipi tungekuwa na kasheria kama haka kule nyumbani? Mnakumbuka yale mambo ya mabinti "kushikwa" na hata "kudisco" wakimzembea Profesa? (sijui sasa kama mambo haya bado yapo yanatendeka au pengine utandawazi umeyamaliza!)
Kwa habari zaidi kuhusu hii ishu soma hapa na hapa
Imegundulika hivi karibuni kwamba kati ya dola bilioni 6.6 ambazo Marekani iliipatia Pakistan ili kuisaidia kupambana na magaidi wa Kitaliban na al-Qaida, ni dola 500 tu zilizotumika kwa lengo hilo.
Badala yake, rais aliyepita wa nchi hiyo, Jenerali Pervez Musharraf, alitumia kiasi kikubwa cha pesa hizo kujaribu kuinua uchumi wa nchi yake uliokuwa ukididimia. Pesa zingine zilitumika kuimarisha majeshi ya Pakistan (ambayo daima ipo katika hatihati ya vita dhidi ya jirani yake India).
Kilichonivutia katika ripoti hii ni kwamba hakuna panapotajwa kwamba Musharraf aliiba pesa hizi na kuzificha kwa manufaa yake binafsi - jambo ambalo pengine tungelitegemea kwa viongozi wengi wa Waafrika.
Badala yake, kiongozi huyu wa kijeshi, aliweka maslahi ya nchi yake mbele na kuamua kuzitumia pesa hizo kuinua uchumi wa nchi yake pamoja na kuimarisha majeshi yake ukiwemo ule mradi tata wa mabomu ya Nyuklia.
Ati, Afrika leo tungekuwa wapi kama viongozi wetu wangetumia pesa za misaada na mikopo (ambazo tumekuwa tukipewa/tukikopa tangu uhuru) kwa kuendeleza nchi zao badala ya kukimbilia kuzificha katika mabenki ya Uswizi?
Pamoja na matatizo yake yote, pamoja na udikteta wake wote - kwa hili namuunga mkono Jenerali Pervez Musharraf na huu ni mfano wa kuigwa na viongozi wa Afrika!
Jana hapa Marekani ilikuwa ni sikukuu ya Halloween- sikukuu ya kipagani iambatanayo na mambo ya kishetani shetani japo inasherehekewa pia na "Wakristo".
Basi jana katika mchezo wa mpira wa kikapu wa NBA kati ya San Antonio Spurs na Sacramento Kings kilitokea kisa cha kushangaza.
Mchezo ulipoanza, na bila kutegemea, alitokea popo ambaye alianza kukatiza uwanja kutokea goli hadi goli. Kidogo kulitokea mtafaruku huku wachezaji wakijaribu kumkwepa popo huyo. Mchezo ulisimamishwa kwa muda.
Popo huyo alipokuwa akijaribu kukatiza tena uwanjani, Manu Ginobili, mchezaji wa San Antonio Spurs kwa kasi ya kutisha alimtandika kwa kutumia mkono wake wa kushoto.
Popo alidondoka chini, Manu Ginobili akamwokota na kumpatia mfanyakazi aliyekuweko, akatia "sanitizer" mikononi na gemu likaendelea.
Matokeo: San Antonio Spurs 113, Sacramento Kings 94.
Ingekuwa nyumbani si ajabu hii ingesemwa kuwa ni kazi ya "kamati ya wazee" kumbe...
Tazama video hapa chini kumwona Ginobili akimfanyizia popo huyu mwenye bahati mbaya.
Baadaye alipata chanjo ya kuzuia vijidudu na aliwaonya watoto wasijaribu kuwaua popo kama alivyofanya kwani inaweza kuwa ni hatari.
Lengo letu ni zuri sana. Kila kata iwe na shule yake ya sekondari. Lakini tumejiandaaje? Kuna walimu wa kutosha katika shule hizi? Kuna vitabu? Kuna maabara? Mazingira kwa ujumla yakoje? Watoto kweli wanapata elimu kama inavyotakiwa? Picha hii ya mama mpishi wa shule imenitatanisha!
Matani kutoka Kenya kutoka tovuti mpya ya Wavuti.com (zamani nukta77.blogspot.com). Kama unavyoweza kuona kuna Ki-sheng hapa na pale; na sarufi na hasa upatanisho wa kisarufi na ngeli za majina zimeparaganyika (mf. ukikunywa maziwa inafika...). Nawapenda Wakenya kwa sababu wao hawatilii maanani sana mambo kama haya ya usanifu wa lugha kama tunavyofanya sisi Watanzania. Nimeandika makala yenye kurasa 25 inayoitwa "Kiswahili Sanifu au Kiswahili cha Tanzania?: Matatizo ya Usanifishaji katika Kiswahili Sanifu" Ikichapishwa nitawapa "link" hapa kwa wanaopenda haya mambo ya lugha. Watanzania - tunayo haki ya kudai kwamba Kiswahili chetu ndicho sanifu kabisa na kile cha Wakenya na hata kile cha Demokrasia ya Kongo (ambacho wenyewe wanadai kwamba ni sanifu pia) si sanifu? *************************************************************************
1. Ati wee ni m-black mpaka ukiingia kwa dinga (gari), dirisha zinakuwa tinted!
2. Kwenu kuchafu mpaka mende zinatema mate, ati ‘THU’ hii hao (HOUSE) ni noma.
3. Vile wewe mfupi, ukipigwa picha ya passport inatokea full.
4. Kwenu nyi wakristu hata dogi zenu zikiona mwizi anaiba, zinawaambia “wee iba tu Mungu anakuona.”
5. Ati hao (house) yenu ina gate lakini hakuna fence.
6. We’ ni mshort mpaka ukikalia kwa pavement (sakafuni) miguu ina hang kwa hewa.
7. We mjinga mpaka uli-fail blood test.
8. Wewe ni mblack mpaka mosquito ikitaka kukuuma lazima itumie torch.
9. We ni mrefu mpaka ukikunywa maziwa inafika kwa tumbo ikiwa mala (MGANDO/MTINDI).
10. Wewe ni mweusi ukikanyanga makaa unawacha footprint za black kwa makaa.
11. Nyanyako (bibi yako) mzee mpaka chawa za nywele yake hutembea na bakora.
12. Ati nyinyi ni wengi nyumbani kwenu yaani buda (baba) yenu hajui majina mpaka huwaaddress kama wananchi. (KAMA RAISI ANAPOTOA HOTUBA)
13. TV yenyu ni Ndogo lazima ufunge jicho moja ndio uone picha.
14. Wewe mblack mpaka unasweat soot.
15. Wewe mnono mpaka ukivaa yellow watoto wanafikiria ni schoolbus.
16. Manzii (mpenzi) wako ni m ugly mpaka alikataliwa ku act horror (movie ya kutisha) Hollywood.
17. Nyumba yenyu ni ndogo mpaka lazima utoke nje kuchange mind.
18. Kwenyu nyinyi ni wengi mpaka kwa hao (house) kuna round-about.
19. Kwenyu nyinyi ni wadaft (WAJINGA) mpaka kupata driving license ilibidi mpelekwe boarding school.
20. Nywele za watoto wenyu ni ngumu mpaka mnazitumianga kama steel wool.
21. Mko wengi kwa hao (house) mpaka kuna rush hours na kukinyesha kunakuwa na jam.
22. Wewe ni mshort mpaka ukishuka kutoka kwa zile vitanda double decker lazima utumie parachute.
23. Ati TV yenu ni ndogo hadi wasee wa news huanza kwa kusema ...ati munatuona jamani?
24. Sistaako ni ugly mpaka monkey ikampatia ndizi.
25. We mblack mpaka ukikutana na mzungu afternoon anakushow good evening?
26. Ngombe yenu mzee mpaka inatoanga yogurt.
27. Kwenu kumekauka mpaka ngombe yenu hutoa milk powder.
28. Wee ni mzee mpaka ukiumwa na mosquito zinatema mate
29. Paka yenu noma mpaka iki shika panya inaitisha chumvi, fork na pilipili.
30. Kwenu nyinyi ni wengi mpaka mkipigwa family photo wengine wanatokea kama wame hang (ning’inia) kwa frame.
31. TV yenu ndogo mpaka wasee wa News (watangazaji wa habari) wamepiga magoti.
32. We mrefu mpaka ukianza kuvaa underwear mbichi by the time ifike kwa magoti imekauka.
33. Nyumba yenu ni chafu mpaka cockroach huvaa slippers (malapa).
Ripoti mpya inayoonyesha usawa wa kijinsia duniani imetoka na nchi za Skandinavia bado zinaongoza (#1-Iceland, #2-Finland, #3-Norway, #4-Sweden). Kwa Afrika, Afrika Kusini (nafasi ya 6) na Lesotho (nafasi ya 10) ndizo nchi pekee za Kiafrika zilizomo katika kumi bora. Kwa Afrika Mashariki Uganda ndiyo inaongoza (nafasi ya 40), Tanzania imeshika nafasi ya 73 wakati Kenya ni ya 98. Marekani - ambako wanawake bado "wanabaguliwa" hasa katika suala la usawa wa mishahara, ajira, pamoja na mambo mengine - imeshika nafasi ya 31. Nchi ya mwisho ni Yemen (#134) ikifuatiwa na Chad (#133) na Pakistan (#132).
Baadhi ya vigezo muhimu vilivyozingatiwa katika uandaaji wa ripoti hii ni pamoja na usawa katika ushiriki wa shughuli za kiuchumi, usawa katika upatikanaji wa elimu ya viwango vyote, usawa katika upatikanaji wa huduma za afya na usawa katika ushiriki wa masuala ya kisiasa. Unaweza kuisoma ripoti kamili hapa na orodha ya nchi zote inapatikana hapa. Tovuti ya World Economic Forum ambayo huchapisha ripoti hii inapatikana hapa.
Jambo la kushangaza ni kwamba ripoti hii inaonyesha kwamba Tanzania inarudi nyuma katika juhudi zake za kuleta usawa wa kijinsia. Mwaka 2006 ilichukua nafasi ya 24, mwaka 2007 (nafasi ya 34), mwaka 2008 (nafasi ya 38) na mwaka huu (nafasi ya 73). Hii ni kweli?
Hapa chini ni Saadia Zahidi - mmojawapo wa waandaji wa ripoti hii akielezea jinsi walivyoweza kuiandaa.
Swali: Nchi za Skandinavia pia ndizo zinaongoza kwa kuwa na talaka nyingi duniani. Je, kuna uhusiano kati ya usawa wa kijinsia na kiwango cha talaka au pengine hii imetokea kibahati tu?
Kituo cha runinga cha History Channel cha hapa Marekani kimeanzisha kipindi kipya kiitwacho Nostradamus-effect. Nostradamus alikuwa mtabiri maarufu wa Kifaransa ambaye wataalamu wengi wa mambo ya utabiri wanadai kwamba alitabiri kwa usahihi kabisa, mbali na mambo mengine, kuzuka kwa Alexander the Great, Adolf Hitler, mashambulizi ya Septemba 11 na hata urais wa Obama. Kwa habari zaidi kuhusu kipindi hiki tembelea hapa.
Katika kipindi cha Nostradamus-effect cha wiki jana wataalamu mbalimbali wa Anthropolojia, Fizikia, Historia, Haidrofizikia na taaluma mbalimbali walijadili kwa kina utabiri maarufu wa Nostradamus kwamba dunia itagharikishwa kwa maji na moto ifikapo mwaka 2012. Walitaja kwamba pengine hili si jambo la kushangaza sana ukizingatia kuyeyuka kwa kasi kwa barafu kunakotokea sasa katika pembe ya kaskazini ya dunia. Athari za tukio hili hazifahamiki na binadamu anaonekana hajali. Wengine walisema kwamba mabomu machache tu ya Atomiki yakiripuka (ama kwa makusudi au kwa bahati mbaya) basi dunia nzima inaweza kugharikishwa na mawingu ya miali hatari kabisa ya atomiki.
Jambo la kushangaza ni kwamba hata kalenda ya Wamaya (ambao himaya yao kubwa na yenye nguvu na maendeleo ya juu ya kisayansi na kiteknolojia iliangamia kutokana na sababu ambazo hazijulikani mpaka leo) inatabiri kwamba dunia itafikia mwisho wake mwaka 2012. Inaaminika kwamba Wamaya (Mayans) walikuwa na uwezo mkubwa wa utabiri na kalenda yao imeonyeshwa kwamba iliweza kutabiri kwa usahihi matukio mbalimbali yakiwemo kupatwa kwa jua, miripuko mikubwa ya volkeno, vita n.k. Cha ajabu ni kwamba hawakuweza kutabiri kuangamia kwa dola lao wenyewe.
Sijui kama wasiwasi huu ni wa kweli au ni yale yale ya Y2K (mnakumbuka?). Lakini ukiwasikiliza vizuri wanasayansi hawa, karibu wote wanakubaliana kwamba dunia itakumbwa na misukosuko ya kimazingira ambayo itasababishwa hasa na mabadiliko ya haraka ya hali ya hewa na mambo mengineyo ingawa hawajui misukosuko hii itatokea lini. Kuna haja ya kuwa wasiwasi?
Tumefika mahali sasa – pengine kutokana na umasikini uliokithiri na ukosefu wa elimu-elimishi – wapiga kura wengi sasa wanafikiri kwamba rushwa wakati wa uchaguzi ni HAKI YAO. Ni ukweli ulio wazi kwamba bila kutoa rushwa huwezi kuukwaa udiwani na hasa ubunge. Nilikuwa nyumbani wakati wa uchaguzi mkuu uliopita na kimsingi nilichokiona hakikuwa “demokrasia” bali mashindano ya kutoa rushwa – kuanzia magunia ya chumvi, sukari, mabati, kanga, vitenge, baisikeli na wajanja waliweza kupata mpaka pikipiki, mitaji ya kufanyia biashara na hata kujengewa nyumba kabisa. Mzee wa vijisenti alikujulikana kwa kufanya iliyokuwa inaitwa “kufuru”. Ni kwa sababu hii sikushangaa sana niliposikia kwamba alikuwa akiandamwa na kashfa mbalimbali za ufisadi. Mabilioni ya shilingi aliyokuwa akiyamwaga wakati wa “kufuru” zake inabidi yalipwe kwani hakuna cha bure hapa duniani.
Basi kama hivi ndivyo, tumlaumu nani katika hili sakata la rushwa wakati wa uchaguzi? Tumlaumu mgombea ubunge ambaye anajua kwamba bila rushwa hatachaguliwa hata kama awe na sera nzuri namna gani, au mpiga kura ambaye hatoi kura yake bila kupewa sukari? Nini suluhisho la mduara huu usio na fundo? Hii kweli ni demokrasia?
Chama cha Wanasaikolojia wa Wamarakeni kimetoa tamko kikiwaonya wanasaikolojia na wafanyakazi wanaojishughulisha na afya ya akili kuacha mara moja kuwaambia wateja wao mashoga na wasagaji kwamba eti wanaweza kubadilika na kuachana kabisa na tabia hiyo. Wanasaikolojia hao wamepinga kwa kina “reparative therapy” – aina ya tiba ya kisaikolojia inayopendekezwa na kikundi kidogo cha wanasaikolojia (ambao wanaungwa mkono na wahafidhina wa Kikristo) ambao wanaamini kwamba mashoga na wasagaji wanaweza kubadilika/kubadilishwa. Kutokana na utafiti ambao wamefanya, wanasaikolojia hawa wanadai kwamba mashoga na wasagaji wakilazimishwa kubadilika wanaweza kutumbukia katika msongo wa mawazo na hata kuamua kujiua.
Dini imetajwa kuwa ndiyo chanzo kikuu cha mashoga na wasagaji kutaka kuachana na mtindo huo wa maisha ambao unapingwa sana na makanisa mengi ya kikristo. Badala ya kuwalazimisha kuachana kabisa na tabia hiyo wanasaikolojia wanapendekeza kwamba ni bora mashoga na wasagaji washauriwe kuishi maisha ya kutofanya mapenzi kabisa au kuhamia makanisa ambayo hayakatazi tabia hiyo.
Ushauri huu wa wanasaikolojia umepingwa vikali sana na Exodus International -mkusanyiko wa makanisa ya kilokole ambayo yanaamini kwamba nguvu za Yesu zinaweza kuvunja “minyororo” ya ushoga na usagaji. Raisi wa shirika hilo aitwaye Alan Chambers mwenyewe ni shahidi mzuri kwani nguvu za Yesu zilimfanya yeye mwenyewe azishinde tamaa zisizotakiwa za kufanya mapenzi ya jinsia moja alizokuwa nazo.
Tafiti mbalimbali zimeonyesha kwamba pamoja na athari za kimazingira, pengine ushoga na usagaji ni tabia ambayo mtu anazaliwa nayo hivyo haiwezi kubadilishwa kirahisi. Wengine wanakwenda mbali hadi kudai kwamba tabia hii itazamwe kama ugonjwa na ianze kutafutiwa tiba kama magonjwa mengine ya kawaida. Watu wa utambuzi mnasemaje kuhusu suala hili na ubadilishaji wa tabia kwa ujumla?
Kwa habari zaidi gonga hapa na unaweza kusoma maoni ya wasomaji. Ted Haggard anayerejerewa mara kwa mara na watoa maoni alikuwa ni mchungaji wa kilokole mashuhuri sana hapa Marekani na ndiye alikuwa kiongozi wa chama chao cha kitaifa kijulikanacho kama "National Association of Evangelicals". Alivuliwa madaraka yote Novemba 2006 baada ya kubainika kwamba alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na malaya mmoja wa kiume!
Niliiona picha hii katika blogu ya Mjengwa na ikanikumbusha mama yangu mzazi. Ingawa yeye ni mzee sana lakini bado analima kishamba chake kidogo, anakwenda kutafuta kuni, kuchota maji kwenye kindoo chake, kuosha vyombo na kufanya kazi zingine kama kawaida. Ukimwambia akae apumzike basi mtagombana vibaya sana. Kipindi fulani nilijaribu kumleta Dar es salaam eti apumzike lakini haikuwezekana. Nilipomuuliza ni kwa nini alikuwa hataki kukaa mjini ambako kuna kitu jibu lake lilinishangaza. “Maisha gani haya ya kukaa tu bila kufanya kazi?”
Jibu hili kidogo lilinishangaza kwani huyu ni mwanamke ambaye tangu nipate ufahamu wa kuelewa mambo sijawahi kumwona amepitisha siku bila kufanya kazi isipokuwa pengine akiwa mgonjwa – tena mgonjwa wa kweli kweli. Nilijaribu kutaka anieleze kulikuwa na ubaya gani kupumzika kidogo Dar es salaam baada ya miaka yote ile ya kufanya kazi. Jibu lake kwa swali hili lilinishangaza zaidi. Alidai kwamba akiacha kufanya kazi basi atakufa na sikujua kama alikuwa anatania ama la!
Tafiti mbalimbali zimeonyesha kwamba kufanya mazoezi mara kwa mara pengine ndiyo jambo la muhimu kuliko yote katika kulinda afya zetu pamoja na kuishi maisha marefu. Magonjwa mengi ya hatari kama vile magonjwa ya moyo, kisukari, shinikizo la damu, aina fulani za saratani na mengineyo yanachangiwa sana na maisha ya deko ambayo hatimaye huishia katika unene usiotakiwa. Nilishangaa kugundua kwamba mwanamke huyu mzee ambaye hakupata “bahati” ya kuingia katika darasa la kizungu na kusoma vitabu alikuwa analifahamu jambo hili vyema. Tulikubaliana na ilibidi “raha za mjini” nilizokuwa najaribu kumpa pale Dar es salaam nimpelekee kule kule kijijini kwake.
Mwaka 2001 alikuja huku Marekani kutembea na nilimpeleka kwa daktari kufanyiwa uchunguzi. Nilishangaa daktari alipowaita wenzake kuja kuona matokeo ya baadhi ya vipimo. Alituambia kwamba alikuwa hajawahi kuona mtu mzee namna ile ambaye alikuwa salama vile. Walipomuuliza alikuwa anakula chakula gani aliwajibu bila kusita “bugali”. Niliwafafanulia ugali ni nini na walishangaa kugundua kwamba ni wanga “carbohydrates” ambazo hapa Marekani kila mtaalamu wa lishe atakwambia usile. Ambacho hawakujua hawa madaktari ni kwamba huyu mwanamke mzee alikuwa anafanya kazi zaidi ya masaa matano kila siku tangu akiwa mtoto mdogo mpaka sasa. Tena chakula anachokula ni cha asili kabisa na hakina aina yo yote ya kemikali!Na kijijini kwetu kuna ajuza wengi ambao ni wazee zaidi kuliko mama na wako salama – hakuna dementia, hakuna Azheimer, hakuna saratani, hakuna kuvunjika mifupa hovyo hovyo, hakuna……
Je, kizazi cha sasa kinachoshinda kikitazama televisheni kitaweza kweli kuishi miaka mingi (bila magonjwa) kama kizazi hiki kinachomaliza muda wake? Kizazi cha sasa kinachokula vyakula vilivyobadilishwa na kujazwa kemikali na homoni za kila aina kitaweza kusafiri safari ndefu ya maisha kama hiki kinachomaliza muda wake? Hebu kizazi kipya na kijifunze yaliyo mema kutoka kizazi hiki kinachoaga kungaliko na muda bado.
Makala haya yametoka katika gazeti la Kwanza Jamii la leo - 20/10/2009
Mwalimu Nyerere na JangwaLake la Kiitikadi
(Ati, ni Nani Hasa Alikuwa Mfuasi wa Itikadi ya Mwalimu?)
Na Dkt. Masangu Matondo Nzuzullima
Katika diwani ya Karibu Ndani (Euphrase Kezilahabi, DUP, 1988:27) kuna shairi liitwalo “Azimio”. Beti chache za shairi hilo zinasema hivi:
Azimio sasa ni
Mabaki ya chakula
Kwenye sharubu za bepari
Kalamu inayovuja
Katika mfuko wa mwanafunzi
Vumbi zito
Baada ya ng’ombe kupita
Kilichosalia sasa
Ni punje za ulezi
Zilizosambazwa jangwani
Na mpandaji kipofu
Hivi ndivyo Kezilahabi – ajulikanaye pia kama Shaaban Robert wa Pili – alivyoliona Azimio la Arusha mwaka 1988. Nimelikumbuka shairi hili wakati nikitafakari Historia ya nchi yangu Tanzania hasa katika kipindi hiki ambapo nchi hii nzuri inaadhimisha miaka 10 tangu muasisi wake atoweke hapa duniani. Ni kweli Mwalimu alisambaza ulezi wake wa Ujamaa na Kujitegemea jangwani? Kama ni kweli, ina maana Mwalimu hakuwa na mfuasi wa kweli hata mmoja katika genge lake la Makomredi waliokuwa wakiimba ahadi za usawa wa binadamu? Ni nani hasa alikuwa mfuasi wa kweli wa itikadi kombozi za Mwalimu Nyerere? Ni Komredi Kingunge Ngombare Mwiru? Ni Edward Moringe Sokoinne? Ni Dr. Salim Ahmed Salim? Ni Rais Benjamin William Mkapa? Ni Mfaume Rashid Kawawa (Simba wa Vita)? Ni Rais Ali Hassan Mwinyi? Ni Jaji Sinde Warioba? Ni Oscar Kambona? Ni John Samwel Malechela? Ni Bibi Titi Mohamed? Ni Edward Lowasa? Ni Nani?
Msukumo hasa wa kuandika makala hii fupi niliupata kutokana na visa vifananavyo vilivyotokea kwangu mwenyewe na dada Subi Sabato wa nukta77.blogspot.com. Katika kuadhimisha miaka 10 ya kifo cha Mwalimu Nyerere niliweka mkusanyiko wa video 17 za Mwalimu Nyerere katika blogu yangu (matondo.blogspot.com). Subi Sabato pia alifanya hivyo hivyo katika blogu yake. Haukupita muda mrefu nilipata barua kutoka kwa watu waliokuwa wakijiita watumishi wa serikali wakinitaka niziondoe video za Mwalimu Nyerere katika blogu yangu mara moja kwani eti sikuwa na hati miliki na kwa hivyo nilikuwa navunja sheria. Waliendelea kunitisha kwamba nisipofanya hivyo basi sheria kali zingechukuliwa dhidi yangu. Subi Sabato naye alipata vitisho kama hivyo. Jambo hili lilinishangaza sana na nilijiuliza maswali mengi ambayo mpaka leo sijapata majibu na ndiyo maana naandika makala hii. Ina maana kuna mtu anamiliki hotuba za Mwalimu Nyerere?Niliwauliza watishaji wangu wanieleze aliko mmiliki wa hati miliki wa hotuba hizi ili niweze kuwasiliana naye lakini mpaka leo sijapata jibu. Mimi nilikuwa ninadhani kwamba hotuba za Mwalimu ni hazina ya taifa na Watanzania wote tuna haki ya kuzisikiliza bila kutishwa na mtu. Nilichukulia mfano wa hapa Marekani ambapo sheria za hati miliki ni kali sana lakini hotuba nyingi za marais wao ziko mtandaoni na ukienda katika maktaba za maraisi hao utaweza kuzisikiliza bure. Ni hazina ya taifa lao. Ni mali ya wote. Ni kumbukumbu ya historia ya nchi yao. Hotuba hizi hazimilikiwi na mtu! Hata hotuba nyingi za Rais Obama tayari zipo mtandaoni! Kuna tovuti nyingi zenye hotuba hizi na mojawapo nzuri ni hii hapa.
Mpaka nitakapopata ufafanuzi wa kina kuhusu ni nani hasa mmiliki wa hotuba za Mwalimu Nyerere, ninashawishika kuamini kwamba kuna kundi la watu ambao wanakerwa, kutishwa na kukoseshwa amani na hotuba za Mwalimu kwani wamegeuka kuwa wasaliti. Hawa inawezekana walikuwa ni watu wa karibu sana kwa Mwalimu na walijifanya kuwa “ardhi yenye rutuba” kwa mawazo na itikadi zake kumbe kwa ndani walikuwa ni “majangwa” tu yasiyootesha wala kustawisha cho chote. Ni mbwa mwitu waliokuwa wamevaa mavazi bandia ya “ukomredi” huku wakiimba na kudumisha “fikra sahihi za Mwalimu” kikasuku tu huku kimatendo wakiwa wamekakawana jangwani. Na baada ya Mwalimu kuondoka sasa wanajaribu kila wawezalo kufanya mawazo yake kombozi yasiwafikie Watanzania huku wakitumaini kwamba kwa njia hii hatimaye pengine Mwalimu ataweza kusahaulika.
Katika hotuba zake nyingi unaweza kumsikia Mwalimu akikemea rushwa na ufisadi; na utulivu wake wa akili, falsafa komavu na uwezo wa kuona mbali, kuonya na kutabiri mambo unaonekana waziwazi. Anasema waziwazi kabisa kwamba rushwa ikiachwa iendelee itaweza siku moja kuutikisa “msingi” wa nyumba (Tanzania). Mwalimu, pamoja na mapungufu yake yote, alitambua kwamba rushwa na utajiri wa kupindukia wa watu wachache kwa upande mmoja, na umasikini na uhohehahe wa asilimia 100 kwa walio wengi kwa upande mwingine siku moja utaitikisa Tanzania kwani ipo siku hawa wasio na kitu watachoka na kusema “liwalo na liwe”.Na hili likitokea hakuna jeshi litakaloweza kurekebisha mambo. Watu wakiamua wameamua na Historia imejaa mifano tele inayoonyesha kwamba nguvu za umma ni kama sunami. Badala ya kujaribu kurekebisha mambo na kuchukua ushauri wa Mwalimu kama vile mbuni asiye na upeo, kundi hili la “wanajangwa” inaonekana limeamua kuficha kichwa mchangani likiamini kwamba kutokomeza mawazo ya Mwalimu pengine ndiyo njia ya mkato ya kuendeleza “jangwa” lao wanalojaribu sana kuhakikisha kwamba linabakia kuwa jangwa. Kundi hili kwa hakika linajidanganya!
Hali hii inaibua hoja nyingine. Kutokana na “ujangwa” huu ambao sasa unaonekana waziwazi, haishangazi kuona kwamba sera nyingi za Mwalimu zilishindwa na kusema kweli inashangaza kidogo kuona kwamba baadhi ya sera zake zilifanikiwa mf. Elimu.
Historia inatuambia kwamba viongozi wengi waliofanikiwa ni wale ambao walikuwa na wafuasi wa kweli, wafuasi ambao walikuwa tayari hata kupoteza maisha yao ili kulinda na kutetea itikadi na harakati zilizoanzishwa na viongozi wao. Na hapa sizungumzii madikteta waliolazimisha itikadi zao kwa wafuasi wao kwa mkono wa chuma na kumwaga damu. Mara nyingi Historia huwa haina huruma na watu wa aina hii bali kuwatupa katika shimo lake la takataka. Huko ndiko waliko akina Mobutu Sese Seko Kuku Ngbendu wa Zabanga, Jenerali Bokasa, Jenerali Field Marshal Idd Amin Dada na wengineo wa aina hiyo.
Viongozi ambao hawakupanda mbegu zao katika “jangwa” mara nyingi hawakuwa hata na haja ya kuandika mawazo yao. Wafuasi wao wa kweli walifanya hivyo. Yesu Kristo hakuandika kitabu cho chote lakini wafuasi wake wa kweli walifanya hivyo. Buddha pia hakuandika kitabu cho chote. Wafuasi wake wa kweli walifanya hivyo. Lao-Tzu (mwanzilishi wa Taoism) pia hakuandika kitabu cho chote. Wafuasi wake wa kweli walifanya hivyo. Ferdinand de Saussure – mwanaisimu wa Uswisi ambaye anatambuliwa kamababa wa Isimu ya kisasa hakuandika kitabu cho chote pia wakati wa uhai wake. Wanafunzi wake walikusanya “notisi” na mihadhara yake aliyokuwa akiitoa wakati wa uhai wake na kuandika kitabu ambacho kilibadilisha kabisa mkondo mzima wa taaluma ya Isimu. Historia ina mifano mingi ya watu wa aina hii. Ni vigumu mno kwa kiongozi kufanikiwa kama amezungukwa na “jangwa” kama inavyobainika sasa kwa Mwalimu Nyerere.
Mwalimu Nyerere ataendelea kuenziwa na Watanzania, Waafrika na wapenda amani kokote duniani na juhudi za kundi hili linalojaribu kuzima mawazo yake linapoteza muda wake bure. Pamoja na makosa yake yote na kushindwa kwa sera yake ya msingi ya Ujamaa na Kujitegemea Watanzania wanaendelea kumuenzi na kumheshimu kiongozi huyu kwa msimamo wake na kutotetereka katika kutekeleza kile alichokiamini kwamba kilikuwa na maslahi kwa watu wake. Mwalimu Nyerere alihubiri na kutenda alichokihubiri na karibu kila kitu alichokitenda kilikuwa ni kitu ambacho aliamini kabisa kwamba kilikuwa ni kwa maslahi ya taifa lakechanga. Jambo hili linawavutia sana Watanzania hasa wakiangalia maisha yake ya uadilifu aliyoishi – yeye pamoja na familia yake. Ni kwa sababu hii mimi naamini kwamba Nyerere na itikadi yake vitadumu!
Pamoja na “ujangwa” uliopo, wakati sasa umefika wa kumaliza ukiritimba katika hotuba (na vitu vingine ambavyo ni hadhina ya taifa letu). Hotuba za Mwalimu Nyerere siyo mali ya Redio Tanzania, mtu wala shirika au kikundi cha watu bali ni mali yetu sote. Ni wakati sasa wa kuziweka hotuba hizi katika mtandao. Hebu tuwe na tovuti maalumu yenye hotuba zote za viongozi wetu wote kuanzia Mwalimu Nyerere, Rais Mwinyi, Rais Mkapa na rais wetu wa sasa Rais Kikwete. Tovuti hiyo itangazwe na itunzwe vizuri kwani itakuwa mojawapo ya hazina muhimu sana kwetu kama Taifa kwa wakati huu na vizazi vijavyo. Wiki ijayo nitazungumzia kosa kubwa kuliko yote la Mwalimu Nyerere!
Wakati wengine wanasota miaka 6-10 (kwa hapa Marekani) kupata shahada za uzamivu (PhDs) "waheshimiwa" hawa wao waliamua kupita njia za mkato, wakaudanganya umma na kujipatia madaraka tena makubwa sana (na nyeti). Watachukuliwa hatua yo yote au ni "siasa" tu mtindo mmoja?
MAWAZIRI
(1) Dk. Mary Nagu (Viwanda, Biashara na Masoko)
(2) Dk. Diodurus Kamala (Ushirikiano wa Afrika Mashariki)
(3) Dk. Makongoro Mahanga (Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana)
(4) Dk. David Mathayo David (Kilimo, Chakula na Ushirika)
(5) Dk. Emmanuel Nchimbi (Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa-JKT)
WABUNGE (1) William Lukuvi (Ismani-CCM) (2) Victor Mwambalaswa (Lupa-CCM)
Nimeiona hii video katika CNN. Eti kuna wasiwasi kwamba kombe la dunia mwaka kesho litaifanya biashara ya ukahaba kushamiri zaidi Afrika Kusini. Hii ni haki kweli au ni kwa sababu kombe hili linafanyika barani Afrika kwa hivyo ni lazima hawa jamaa wachonge? Kwa kuwa ukahaba ni tatizo la dunia nzima, je, ulikuwa tatizo pia hata katika nchi zingine ambako kombe hili limeshawahi kushindaniwa? Au pengine hali ya ukahaba Afrika Kusini ni mbaya zaidi kuliko sehemu zingine duniani? Nimetatanishwa!
Mtu na babake wametoa kali ya mwaka kule Alabama. Baba ana miaka 37, mtoto wake wa kiume ana miaka 19. Kwanza walianza wakazitwika bia mpaka wakawa njwii halafu wakaamua kwenda kuvunja nyumba ili kuiba usiku wa manane. Kweli wakafanikiwa na wakaiba funguo za gari, dola karibia 200 na vito vyenye thamani inayokaribia dola 100 wakati wenye nyumba wakiwa wamelala.
Wakati wanajaribu kuondoka soo likabumburuka. Wenye nyumba wakaamka. Kwa akili za haraka haraka jamaa wakajibanza sehemu na hatimaye wakajificha chini ya kitanda katika chumba cha kulala. Soo likapoa. Baadaye baba akafanikiwa kuchepuka na kumuacha mtoto mvunguni mwa kitanda. Kumbe mtoto akawa amezimika mle mvunguni kutokana na kilevi.
Basi wenyeji wakalala kama kawaida mpaka asubuhi. Ndipo mama mwenye nyumba akashtukia ishu. Kuchungulia mvunguni mwa kitanda akamkuta mtoto mwizi akiwa ameutandika usingizi bila wasiwasi. Akakimbia kwenda kumwita jirani. Jirani alipokuwa basi mambo yakachangamka zaidi kwani yule kijana mwizi aliyekuwa amezimika mvunguni ni mjukuu wake. Polisi wakaitwa. Mwizi kuamshwa akawa anamuulizia baba yake. Polisi wakaondoka naye kwenda kumchukua baba yake na wote haooo korokoroni. Tangu hapo pombe siyo supu ati!
Mimi huwa sipendi kusafiri wa ndege na huwa napanda ndege tu kwa kuwa hakuna njia nyingine ya kusafiri kwa haraka zaidi. Mwaka 2006 kindege cha Precision Air kilihangaika kweli kutua pale Ibadakuli Shinyanga na ingawa nilikuwa naendelea mpaka Mwanza niliomba nishukie hapo hapo kwani sikutaka tena kwenda kupata mateso katika kutua kule Mwanza. Jamaa walinikubalia kushuka kwa shingo upande. Ningekuwa kwenye ndege kama hii sijui ingekuwaje. Kuna mwingine anayeogopa kusafiri kwa ndege au niko peke yangu? Watu wa utambuzi mna suluhisho kuhusu tatizo hili?
Katika kuadhimisha kumbukumbu ya miaka 10 tangu Muasisi wa Taifa letu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere atutoke, hizi hapa video zake mbalimbali. Japo zina urefu tofauti tofauti na zingine hazizidi hata dakika moja, kwa pamoja zinaonyesha falsafa yake tetezi na misimamo isiyolegalega ya Mwalimu. Natoa shukrani kwa wadau mliojitolea kuzitundika video hizi katika Youtube na Google Video. Kwa hotuba zaidi za Mwalimu Nyerere tembelea http://nukta77.blogspot.com. Mungu ibariki TANZANIA!
Tarehe 15 Septemba, 2009 wanyongaji katika jimbo la Ohio kule Marekani walihangaika kwa zaidi ya masaa mawili wakijaribu kumnyonga muuaji, mbakaji na mteka nyara aitwaye Romell Broom (pichani) aliyekuwa amehukumiwa kunyongwa mpaka kufa kwa njia ya sindano ya sumu. Kutokana na matumizi yake ya madawa ya kulevya kwa muda mrefu, wanyongaji walishindwa kupata mshipa wa damu katika mikono yake ili kupitisha sumu ambayo hudhoofisha kwanza mwili na baadaye mapafu na moyo na hatimaye kusababisha kifo. Pamoja na mnyongwaji kujaribu kuwasaidia wanyongaji wake kwa kulala ubavu ubavu katika meza ya kunyongea na kujaribu kukunja ngumi ili kutunisha mishipa ya damu, wanyongaji hao hawakufanikiwa na baada ya masaa mawili Gavana wa jimbo la Ohio Ted Strickland aliamru unyongaji huo usimamishwe.
Walitaka kumnyonga tena baada ya wiki moja lakini wanasheria wake wakawa tayari wameshakata rufaa na kesi hiyo bado inaunguruma mahakamani. Na Romell Broom bado yupo tu anadunda. Kweli kama siku zako hazijafika hapa duniani binadamu hata wafanyeje ni bure! Kwa habari zaidi soma hapa. Mwenyewe anaeleza hapa yaliyomsibu siku ya Septemba 15, 2009 alipokutana na kifo uso kwa uso.
Jana asubuhi katika viwanja vya St. Peter Square kule Vatican Papa Benedict XVI alimtangaza "Baba" Damien De Veuster (January 3, 1840–April 15, 1889) kuwa Mtakatifu. "Baba" Damien De Veuster anakuwa Mtakatifu wa kwanza kutoka jimbo la Hawaii. Nilitembelea Hawaii mwaka wa 2005 kwa wiki mbili na Molokai -mahali alipoishi kwa miaka mingi akiwahudumia wagonjwa wa ukoma mpaka alipofariki (kwa ukoma pia) - ni mojawapo ya vivutio vya utalii.
Kama tunavyojua, "watakatifu" hawa (ambao ni lazima wawe wameshakufa) katika kanisa la kikatoliki huombwa na kuabudiwa; na inasemekana wana uwezo wa kutenda miujiza. Ili kutangazwa mtakatifu inabidi angalau miujiza miwili ya kiuponyaji itokee na iambatishwe moja kwa moja na anayetaka kutakatifishwa. Huu ndiyo utaratibu ambao Mwalimu Nyerere itabidi afuate kama kweli kanisa la kikatoliki linataka kumfanya kuwa Mtakatifu.
Swali langu ni hili:Mbona Waafrika wakisali na kuomba kwa mababu zao waliowatangulia wanaambiwa kwamba wanaabudu mizimu na wakiwaabudu hawa watu "waliotakatifishwa" na kanisa ni sawa?
Katika vyuo vikuu vingi (na hata shule za msingi, sekondari na vyuo vinginevyo) hapa Marekani kuna tuzo linaloitwa "Teacher of the Year Award" Tuzo hili nadra hutolewa kwa mwalimu ambaye ameonyesha uwezo, ubunifu, mafanikio na njia za kipekee katika kufundisha. Mimi nami nililipata tuzo hili hapa Chuo Kikuu cha Florida mwaka wa masomo wa 2004-2005.
Ili kulipata tuzo hili ni utaratibu mrefu na uchaguzi wake hufanywa kwa uangalifu sana. Mbali na kupendekezwa, inabidi wanafunzi wako waandike barua wakieleza kwa kina jinsi ufundishaji wako ulivyowabadilisha na ni kwa nini wanafikiri kwamba unastahili kupata zawadi. Inabidi waseme ni kwa jinsi gani ufundishaji wako uko tofauti (na bora zaidi) na wa walimu wengine ambao wameshawahi kuwafundisha. Pia msimamizi wako (mkuu wa idara/kitengo) pamoja na walimu wenzako ni lazima waandike barua kukuunga mkono (watatembelea madarasa yako ili kujionea wenyewe jinsi unavyofundisha kabla hawajaandika barua zao). Halafu mwenyewe inakulazimu uandike insha ndefu kujieleza jinsi ufundishaji wako ulivyo tofauti na walimu wengine, falsafa inayokuongoza darasani na mtazamo wako mzima kuhusu nafasi ya mwalimu darasani na katika jamii kwa ujumla. Ni lazima pia uambatishe silabasi zote za masomo uliyowahi kufundisha, mifano ya mazoezi na mitihani ya mihula, "handouts" na vikorokocho vingine vingi. Halafu kamati maalumu iliyo chini ya "Dean" inakaa kupitia walimu wote waliopendekezwa na kufanya uteuzi wa mwisho.
Kwa upande wangu wanafunzi wenyewe walijikusanya wakashauriana wakaandika barua, wakawatafuta na wanafunzi wangu wa zamani nao wakaleta barua zao na kisha wakapeleka pendekezo lao katika kamati teuzi. Nilipata bahati ya kusoma baadhi ya barua zao na nilishangazwa na mambo ambayo waliyaeleza. Nilivutiwa na kuguswa mno!
Mbali na kupata bango la kumbukumbu (plaque), mshindi pia unapata cheki ya dola 5,000, unahongereshwa rasmi siku ya mahafali ya wanafunzi (na ukitaka unaweza kutoa hotuba) na unakaribishwa katika dhifa maalumu pamoja na rais wa chuo pamoja na viongozi wengine. Kwa ujumla hii ni siku nzuri ambayo mwalimu unaona kwamba juhudi zako pamoja na kipaji chako cha uelimishaji kweli kinaheshimiwa na kuthaminiwa. Inafurahisha na kutia moyo sana!
Mimi naamini kwamba huu ni utaratibu mzuri sana katika kuwaonyesha walimu wetu kwamba tunawajali na kuuthamini mchango wao na sioni ubaya wo wote kama nasi tukianzisha utaratibu kama huu (tena bila upendeleo wo wote) kwa walimu wetu katika ngazi mbalimbali.
Mwalimu wa binti yangu aliyeko darasa la pili alituambia hivi wazazi tuliokuwa tumekusanyika kumhongeresha (pamoja na kumpelekea zawadi) baada ya kushinda tuzo hili mwaka jana katika shule yake ".....Nitajibidisha zaidi mwaka ujao na wanafunzi wangu wataona mambo mapya na kujifunza kwa urahisi zaidi" Hili ndilo lengo hasa la tuzo hili - kuwapa motisha walimu kwa kuwaonyesha kwamba tunathamini na kuheshimu mchango wao - hasa wale wenye vipaji vya pekee na wanaojitolea sana katika kuelimisha watoto wetu!
Na siku moja natamani kurudi nyumbani na kutumia kipaji changu na mambo ambayo nimejifunza huku katika kuelimisha taifa langu!
Mwanafunzi huyu hakuelewa inawezekanaje mtu anatumia mamilioni ya dola za umma kujijengea makao makuu ya kifahari kama yale wakati watu wengi katika nchi yake hawana huduma za msingi kabisa kama chakula, maji, matibabu, elimu na usafiri? Aliendelea kudai kwamba watu kama Mobutu kimsingi siyo binadamu kwani, kwa maoni yake, hakuna binadamu ambaye anaweza kufanya yale aliyoyaona kule Kongo na akabakia kuitwa binadamu.
Alipoondoka nilibaki nikifiriki hasa sisi binadamu ni nani na nini hasa kinachotufanya tuitwe binadamu. Ati, wana hisia na utu gani akina “Mobutu” wetu (ambao ni wengi sana barani Afrika) ambao hawana ubinadamu na wanachojali ni kunenepesha matumbo yao – wakiwaibia watu masikini na kuwasikinisha kabisa bila kujali cho chote? Ni kweli watu hawa wana furaha, hisia za ridhiko, mafanikio na utu? Huwa wanafikiri nini wakiona watoto wanasomea chini tena katika majengo mabovu wakati pesa za kununulia madawati na kujengea majengo ya shule wamezificha katika akaunti zao za siri? Huwa wanajisikiaje watoto mamilioni wanapokufa na malaria wakati pesa za kununulia vyandarua na dawa za malaria wamezitumia kujengea majumba ya kifahari? Huwa wanajisikiaje wakiwaona akina mama wakitembea maili sita kwenda kutafuta maji wakati pesa zilizotengwa kwa shughuli hiyo wamezitumia kujinunulia maghari ya gharama kubwa na kupeleka watoto wao nje kusoma? Wanajisikiaje? Mafisadi wana ubinadamu wowote? Ati, mafisadi ni binadamu?
Kwa habari kuhusu Gbadolite soma hapa. Hata Mtume Onesmo N. Ndegi wa Living Water Center Makuti Kawe Dar es salaam haelewi kabisa!
Katika makala yangu fupi yenye kichwa Kwa nini wanaume (wa Kisukuma) hufariki mapema sana? ilibainika wazi kwamba mojawapo ya sababu ya jumla ya sisi wanaume kufariki mapema ni kutopenda kwetu kwenda hospitalini. Mpaka tukakubali kwenda hospitalini basi hapo ni lazima tuwe wagonjwa kwelikweli. Hapo ulipo hebu jiulize, ni lini ulikwenda kufanyiwa uchunguzi wa afya yako kwa mara ya mwisho? Hata kwa sisi ambao tuko huku ughaibuni ambako kusema kweli huduma za afya ni nzuri bado tunasubiri mpaka tuwe wagonjwa kabisa kabisa ndiyo twende hospitalini. Nimesoma uchunguzi wa afya ya Rais JK hapa chini na kuona kuwa ni jambo la maana sana kwa mtu kukaa ukijua kwamba uko salama. Wanawake pia inabidi mtusaidie katika jambo hili hata kama ikibidi mtumie zile mbinu zilizopendekezwa na Aristophanes katika tamthiliya yake ya Lysistrata. Tujijali, mtujali, tujaliane, TUOKOANE!
Mimi naitwa Dk. Peter Mfisi, ni mmoja wa madaktari wa Mhe. Rais. Nipo Ikulu. Nimekuwa na Mhe. Rais tangu wakati wa kampeni mwaka 2005 mpaka sasa. Mwenzangu ni Dk. Mohamedi Janabi ambaye ni daktari bingwa wa maradhi ya moyo katika Hospitali Kuu ya Taifa Muhimbili. Nimewaiteni waandishi wa habari kufafanua masuala muhimu kuhusu afya ya Mhe. Rais kufuatia tukio la Jumapili iliyopita, Oktoba 4, 2009, pale Mwanza.
Tukio hilo limeleta mshtuko kwa watu wengi na kuendelea kuwa jambo linalozua mjadala kuhusu hali ya afya ya Mhe. Rais. Naelewa sababu ya wananchi kuwa na hofu na kuwapo kwa mjadala miongoni mwao. Rais ndiyo kiongozi wetu mkuu katika taifa na hivyo kuwa mwenye afya njema ndiyo matakwa ya kila mwananchi.
Naelewa fika kuwa kutokana na kiapo changu cha udaktari na maadili yangu ya kazi siruhusiwi kutoa hadharani undani wa habari yoyote inayohusu mgonjwa ninayemtibu bila ridhaa yake. Hata hivyo, kwa kuwa huyo ni Rais wa nchi, na suala la afya yake ni kwa maslahi ya taifa na umma wa Watanzania kwa jumla, na kwa kuwa yeye ameridhia kutolewa kwa habari za afya yake ili watu wajue ukweli na kuondoa hofu, nimeamua kufanya hivyo.
Kama sote tujuavyo, Jumapili iliyopita, Oktoba 4, 2009 mwaka huu, Mhe. Rais Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa anashiriki katika sherehe za miaka 100 ya Kanisa la Africa Inland Church Tanzania (AICT) kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza, aliishiwa nguvu na kulazimika kwenda kwenye chumba cha mapumziko.
Baada ya mapumziko ya dakika 10 hivi, Mhe. Rais alirejea kwenye shughuli hiyo na kuendelea kushirikiana na waumini wa AICT hadi mwisho wa ratiba yake. Ninapenda kusisitiza kuwa tukio la Mwanza limetokana na Mhe. Rais kuzidiwa na uchovu, na wala siyo kwa sababu nyingine yoyote ya kiafya. Wakati tukio hilo linatokea nilikuwepo, nilichukua vipimo muhimu kama daktari anavyotakiwa kufanya linapotokea tukio kama lile kwa mtu. Vipimo vyote vilithibitisha kuwa Mhe. Rais hakuwa na matatizo yoyote ya kiafya ambayo yangeweza kuhusishwa kuwa chanzo cha tukio lile.
Pressure yake ilikuwa 130/85mmhg ambayo ni kiwango cha kawaida kwa mtu wa umri wake. Mapigo ya moyo wake yalikuwa 76 kwa dakika ambayo pia ni ya kawaida. Sukari kwenye damu ilikuwa 5.5mmol/l ambayo nayo ilikuwa ya kiwango cha kawaida. Joto la mwili lilikuwa digrii 37.5 centigrade ambalo ni la kawaida. Mhe. Rais pia hakuwa na kiungo chochote kilichoonekana kutetereka, jambo ambalo lilithibitisha kuwa hakupata kiharusi.
Kutokana na matokeo hayo, sikuona hatari yoyote ya yeye kuendelea kushiriki katika sherehe hiyo muhimu kwa wakati huo. Ndiyo maana niliruhusu aendelee kushiriki sherehe zile mpaka alipomaliza na kuondoka. Baada ya kurudi Dar es Salaam siku ile niliwasiliana na madaktari wanzangu wa hapa nchini na nje ya nchi ambao tumekuwa tunashirikiana nao katika kuchunguza na kufuatilia afya ya Mhe. Rais. Wote hao baada ya kuwasimulia kilichotokea na matokeo ya vipimo nilivyomfanyia Mhe. Rais, kwa tafakuri zao hawakuwa na wasiwasi wowote kuwa tukio hilo lilisababishwa na jambo jingine lolote, isipokuwa uchovu. Imani yao inatokana na ukweli kuwa wanaifahamu vizuri hali ya afya ya Mhe. Rais kwa kuwa wanahusika katika kuifuatilia mara kwa mara. Mmoja wao alimuona Mhe. Rais siku moja kabla ya kuondoka New York ambapo alipata nafasi ya kuchunguza afya yake.
Mimi na mwenzangu Dk. Mohammed Janabi, ndiyo wenye dhamana ya kuiangalia afya ya Mhe. Rais Kikwete kila siku. Tumekuwa tunafanya hivyo kwa zamu na wakati mwingine kwa pamoja, inapobidi kufanya hivyo. Katika kufuatilia hali ya afya ya Mhe. Rais tumekuwa pia tukimfanyia uchunguzi wa afya yake kwa vipindi maalum hapa nchini na nje ya nchi kwa vipimo ambavyo hapa nchini havipo. Napenda kuwahakikishia wananchi wenzagu kuwa katika miaka hii minne Mhe. Rais wetu amefanyiwa uchunguzi wa kina wa afya yake. Nadiriki kusema kuwa hakuna kipimo ambacho hatujapata kukifanya katika uchunguzi wa mambo muhimu ya afya yake.
Kwa sababu ya kuwatoa hofu wananchi na kwa vile mwenyewe anaridhia tufanye hivyo napenda kuwapa ufafanuzi kuhusu hali ya afya ya Mhe. Rais. Katika hali ya kawaida nisingefanya hivyo kwa sababu maadili ya kazi ya udaktari yanakataza. Naamini madaktari wenzangu wataelewa mazingira niliyokuwa nayo. Katika kufuatilia afya ya rais tumekuwa tunaangalia na kuchunguza mambo yafuatayo.
(a) Blood Pressure:Tunafuatilia kwa karibu sana hali ya nguvu ya msukumo wa damu (blood pressure). Tunampima mara kwa mara na mwenyewe tumempa mashine ya kujipima kila siku na anafanya hivyo. Kwa jumla pressure yake iko kwenye viwango vya kawaida. Aidha, uzito wake wa mwili unaendena ipasavyo na urefu wake. Mhe. Rais ni mtu mwenye mazoea ya kufanya mazoezi na yuko makini katika chakula anachokula. Sisi tunahusika kwa ukamilifu na kuelekeza kuhusu chakula anachokula. Hatuna matatuzi na Mhe. Rais kwa jambo hilo. Ana nidhamu ya kujipima pamoja na mazoezi na chakula.
(b) Moyo: Tumekuwa tunafuatilia kwa karibu hali ya afya ya moyo wake. Tumemfanyia vipimo kama vya ECHO, ECG na vinginevyo, na hatujabaini kuwepo tatizo lolote.
(c) Ubongo:Mwaka uliopita, 2008, Mhe. Rais tulimfanyia uchunguzi wa afya ya ubongo wake katika Hospitali ya Taifa Muhimbili hapa Dar es Salaam. Tulitumia kipimo cha CT – Scan na matokeo yameonyesha kuwa hana matatizo. (d) Ini, Figo, Bandama, Kongosho: Mhe. Rais Kikwete kila mwaka tunapomfanyia uchunguzi wa jumla wa afya yake tumekuwa tunamfanyia kuchunguza viungo vyake muhimu vya tumboni kama vile ini, figo, bandama na kongosho. Tumekuwa tunafanya hivyo kwa kutumia kipimo cha ultra sound na kwa kupima damu yake kwa kutumia vipimo muhimu. Uchunguzi huo umebaini kuwa viungo vyote hivyo ni salama na vinafanya kazi vizuri.
(e) Mfumo wa njia ya Chakula: Mfumo mzima wa njia ya chakula (alimentary canal), yaani koromeo la chakula, tumbo, utumbo mdogo na utumbo mkubwa nao tumeufanyia uchunguzi wa kina kama kuna tatizo lolote katika kipindi cha miaka miwili hii. Mwaka 2007, tulimfanyia kipimo cha colonoscopy mjini Paris, Ufaransa, kuchunguza hali ya afya ya utumbo mkubwa. Matokeo ya uchunguzi yalionyesha kuwa utumbo wake mpana uko salama kabisa na hakuna matatizo yeyote. Daktari bingwa aliyemfanyia uchunguzi huo ameshauri kuwa Mhe. Rais hahitaji kufanya kipimo hicho tena mpaka baada ya miaka saba. Nakumbuka pia daktari huyo alimtania Mhe. Rais kuwa angefurahi kuazima utumbo wake.
Wiki mbili zilizopita, Mhe. Rais akiwa mjini New York, Marekani, alifanyiwa kipimo cha endoscopy kuchunguza kuanzia koromeo la chakula, tumbo, na utumbo mdogo. Matokeo ya uchunguzi huo yametoa majibu mazuri kuwa yako salama. Makusudio ya kufanya vipimo hivi viwili ni kuchunguza maradhi ya kansa na viashiria vya ugonjwa huo. Bahati nzuri hana maradhi hayo na wala hakuna dalili yoyote iliyoonyesha kuwapo viashiria vya kansa.
(f) Tezi la Shingo (Thyroid Glands): Aidha, wakati wa safari yake hivi karibuni majuzi mjini New York, Marekani, Mhe. Rais tulimfanyia uchunguzi wa afya ya tezi la shingo pamoja na kiwango chake cha utoaji wa homoni. Matokeo ya vipimo vyote vilivyofanyika yameonyesha kuwa hakuna matatizo yoyote.
(g) Tezi la Kibofu (Prostate): Septemba, mwaka huu, 2009, tulifanya uchunguzi wa hali ya afya ya tezi la kibofu (prostate) kwa kutumia mashine maalum na kwa kuchunguza damu yake. Vipimo vyote hivyo vimeonyesha hali si mbaya. Tezi lake lina ukubwa wa kawaida na hata vipimo vya viashiria vya kansa ya tezi hilo (PSA) tunavyofanya kwenye damu vilikuwa katika kiwango cha kawaida. Mhe. Rais hana matatizo ya prostate. (h) Macho, Masikio na Pua:Tumeshamfanyia vipimo vya macho, masikio na pua na vyote viko salama. Mhe. Rais anavaa mawani lakini hayo si maradhi. Watu wengi baada ya kufikia umri wa miaka 40 si ajabu huhitaji mawani. Tunapofanya uchunguzi wa macho, ukiacha ile ya kuchunguza uwezo wa kuona, tunaangalia pressure ya macho na hali ya viungo vya nje na ndani ya jicho. Mhe. Rais hana matatizo yoyote.
(i) Damu: Tumekuwa tunamfanyia Mhe. Rais uchunguzi wa damu yake kwa vipimo mbalimbali vinavyotumika kutambua maradhi mbalimbali yahusuyo damu yenyewe na mwili mzima wa mwanadamu. Tumekuwa tunafanya hivyo kila baada ya miezi sita au panapojitokeza ulazima wa kufanya hivyo. Tumekuwa tunafanya hivyo hapa nchini na hata nchi za nje kwa nia ya kulinganisha matokeo yetu na kwa vipimo ambavyo sisi hatunavyo. Matokeo ya uchunguzi wetu yameonyesha kuwa Mhe. Rais yuko salama. Hana maradhi ya damu au kisukari, wala ukimwi, au ya wingi wa mafuta (cholesterol), ama ya kiwango cha madini, au ya tezi la kibofu, wala ya tezi la shingo, au ya ini, au ya homoni mbalimbali zilizoko mwilini na mengine n.k. Jambo pekee linalojitokeza ni kwamba Mhe. Rais ana damu nyingi. Hivyo, tumekuwa tunamshauri kupunguza damu kwa kuchangia Benki ya Damu.
Tunashukuru amekuwa anafanya hivyo karibu kila baada ya miezi sita. Damu nyingi inaweza kuwa na madhara mwilini lakini Mhe. Rais hajafikia kiwango cha kuwa ni tatizo la kiafya. Pia tunamshukuru kwa kuwa mwepesi kukubali kupunguza damu ambayo tunaitumia kuokoa maisha ya watu wengine. Hakuna hofu yoyote. Napenda kusema wazi watu wote wasikie na kwa ukweli kwamba mimi na daktari mwenzangu yaani Dr. Mohamed Janabi hali ya afya ya Rais silo jambo linalotutia shaka wala kutusumbua au kutunyima usingizi.
Tatizo pekee ambalo limekuwa likimsumbua Mhe. Rais mara kwa mara ni maumivu ya shingo yanayotokana na kuumia zamani utotoni na wakati wa ujana. Kuumia huko ni kwa baadhi ya pingili za uti wa mgongo, sehemu ya shingo (cervical spine), kuathirika na kumsababishia maumivu. Mara nyingi matatizo ya namna hiyo huwapata wanamichezo na wanajeshi. Kutokana na shughuli wazifanyazo. Kuumia siyo jambo la kustaajabisha.
Tutakumbuka kuwa Mhe. Rais amekuwa mwana michezo hususan mchezaji wa basketball, mpira wa miguu na hata riadha wakati wa ujana wake. Pia alikuwa mwanajeshi. Ili kutambua vizuri tatizo la shingo ili tujue namna ya kumpatia tiba tumeshamfanyia vipimo vyote muhimu vya uti wa mgongo toka juu mpaka chini. Tumetumia x-ray, CT – Scan na MRI-Scan. Pia ameshaonwa na madaktari bingwa wa upasuaji wa mishipa ya fahamu hapa nchini na nje. Pamoja na kuwepo athari katika shingo, madaktari hao kwa dhati wameshauri kuwa kwa sasa maumivu yake hayahitaji upasuaji isipokuwa mazoezi ya viungo. Mhe. Rais amefundishwa mazoezi anayotakiwa kuyafanya na amekuwa anayafanya kwa nidhamu ya hali ya juu. Matokeo yake ni kupata nafuu kubwa. Ndiyo maana siku hizo haonekani kunyoosha shingo mara kwa mara kama ilivyokuwa zamani kwa wale wanaokumbuka. Tunafuatilia kwa karibu sana hali ya shingo yake. Tunamfanyia vipimo vya MRI na kuonana na madaktari bingwa mara kwa mara.
Mwisho
Napenda kabla ya kumalizia nisisitize tena kwa kusema kuwa mimi na daktari mwenzangu hatuna mashaka na hali ya afya ya Mhe. Rais. Afya yake ni nzuri, hana maradhi yanayotishia maisha yake au kupunguza uwezo wake wa kulitumikia taifa na watu wake. Pia maoni yetu hayo ndiyo maoni ya madaktari wa ndani na wa nje waliowahi kuhusika na uchunguzi wa afya yake. Napenda pia kuwahakikishia kuwa, sisi madaktari wake, hatutachoka kufuatilia kwa karibu na kwa umakini mwenendo wa afya ya Mhe. Rais ili tujue mapema kama kuna jambo la kushughulikia. Kwa hili lililotokea, tutaendelea kuchunguza kama jambo lolote lililojificha ambalo hatujalibaini.
Kwa sasa napenda kurudia kusema kuwa hakuna ushahidi wa kitaalamu wa kusema kuwa kulikuwa na sababu nyingine zaidi ya uchovu. Rais aliondoka New York Septemba tarehe 30 saa nane ya usiku kwa saa ya hapa Dar es Salaam kuanza safari ya kurudi nyumbani. Aliwasili nyumbani saa saba ya usiku wa tarehe 1 Oktoba. Njiani alisimama London na Nairobi kuunganisha ndege. Hivyo basi, alisafiri saa 24 bila ya kulala vizuri. Isitoshe hata kwenye ndege alitumia muda mwingi akifanya kazi. Asubuhi na mapema siku ya Oktoba 2, aliondoka Dar es Salaam kwenda Arusha kufungua mkutano wa Wabunge wa Jumuiya ya Madola saa nne asubuhi. Baadae jioni yake alishiriki kwenye hafla ya chakula cha jioni alichowaandalia wabunge. Rais aliondoka saa sita usiku kwenda kulala. Hatuna hakika alilala saa ngapi kwani najua akiwa na kazi huchelewa sana kulala. Tarehe 3 Oktoba, 2009 alikuwa na mikutano mfululizo na viongozi na wananchi pale Arusha kabla ya kuondoka majira ya alasiri kwenda Mwanza. Alipofika Mwanza alikuwa na mazungumzo na wenyeji wake usiku ule mpaka saa nne ya usiku. Tulipofuatilia tuligundua kuwa hata siku hiyo nayo alichelewa sana kulala kwani walipondoka wageni wake yeye aliendelea kushughulikia hotuba yake mpaka karibu na alfajiri. Katika mazingira hayo kupata matatizo ya mwili kuchoka sana, na hata kukataa kuendelea kutumika, na kutaka kupumzika kama ilivyotokea si jambo la ajabu.
Mwisho kabisa napenda kuwahakikishia kuwa Rais yuko salama. Afya yake ni nzuri na haina shaka yoyote. Uchovu uliokithiri ndicho chanzo cha yaliyotokea Mwanza siku ile ya tarehe 4 Oktoba, 2009. Mimi na wenzangu katika Ofisi Binafsi ya Rais (OBR) tumejifunza na tumeazimia kuwa waangalifu zaidi katika kupanga ratiba ya kazi ya Rais.
Dr. Peter Mfisi
Ikulu, Dar es Salaam Daktari wa Rais 08 Oktoba, 20
Nchi nyingi za Kiafrika (ikiwemo Tanzania) ni madampo tu ya kutupia bidhaa zisizofaa (na za bandia) kutoka nchi za Kimagharibi na CHINA. Kuanzia vyakula, madawa, vipodozi na sasa ATM. Watu mpaka wanauza dawa za Maralia za bandia! Mpaka kondomu za bandia! Wanaoingiza bidhaa hizi hawajui kwamba ni mbovu? Kama wanajua ni kweli tumekuwa wakatili kiasi kwamba mtu unauza dawa za Malaria au kondomu za bandia huku unajua kabisa kwamba kwa kufanya hivyo unaweza kuwa unahatarisha maisha ya wenzako moja kwa moja? Mamlaka inayohusika na suala hili inafanya kazi gani?
Serikali imesema mashine nyingi za kutolea fedha benki (ATM), ni mbovu kwa kuwa huingizwa nchini kutoka nje baada ya kuonekana huko hazifai. Imesema hatua hiyo inasababisha kuwepo wimbi la watu kuiba fedha za wenzao kupitia mashine hizo bila wenyewe kujua.
Kauli hiyo ilitolewa jana jijini Dar es Salaam na Naibu Waziri wa Fedha na Uchumi, Jeremiah Sumari, alipokuwa akijibu maswali ya wabunge katika kikao cha Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Fedha na Uchumi. Sumari alisema kuwepo kwa mashine hizo ni hatari kwa usalama wa fedha za wananchi.
Alifafanua kuwa kuna nchi moja ambayo hakuitaja iliwahi kuhamisha mashine zake zilizokuwa mbovu na kuzipeleka nchi nyingine na kwamba tukio hilo linaonyesha kuwa hata hapa nchini ziliingizwa. Alishazishauri benki kuchukua tahadhari ili kuepusha wimbi la wizi kupitia ATM.
Hivi karibuni, Jeshi la Polisi liliwakamata raia wawili wa Bulgaria kwa tuhuma za kuiba kiasi cha Sh. milioni 70 jijini Dar es Salaam kupitia mashine hizo bila kutumia kadi. Wameufunguliwa mashitaka kortini.
Mbali na matukio ya wizi, baadhi ya ATM zimekuwa zikilalamikiwa na wateja wa benki kutokana na kuharibika mara kwa mara na wakati mwingine kutokuwa na mtandao, hivyo kuwasababishia usumbufu wa kutopata huduma.
Akizungumzia Benki ya Posta Tanzania ambayo serikali inamiliki asilimia 81 ya hisa, alikiri kuwa inahitajika sheria itakayoibadilisha kuwa kampuni ili iweze kufanya kazi kwa kushindana. Sumari alikuwa akijibu hoja mbalimbali za wabunge waliokuwa wakijadili utendaji wa benki hiyo.
Uongozi wa benki hiyo uliwaeleza wabunge kuwa unakabiliwa tatizo la mtaji mdogo, jambo ambalo linawafanya washindwe kufikia malengo waliyojiwekea. Wakichangia katika kikao hicho baadhi ya wabunge walisema bila sheria kufanyiwa marekebisho itakuwa vigumu benki hiyo kuweza kufanikisha malengo yake.
Mwenyekiti wa kamati hiyo, Dk. Abdallah Kigoda, alishauri mabadiliko hayo yafanyike haraka na serikali iache kutumia neno "ipo kwenye mchakato" kwani hali hiyo inakatisha tamaa.
Alisema neno mchakato halina mwisho na halisemi ni lini kazi husika au itaanza kufanyika, kauli ambayo iliungwa mkono na wabunge wengi. Kwa upande wake mbunge wa Wawi (CUF), Hamad Rashid Mohamed, alisema wananchi wamechoshwa na neno "mchakato" ambalo serikali inapenda kulitumia kwa kuwa halionyeshi ni lini itafanya kile inachokusudia kukifanya.
Aliishauri serikali kuuza hisa zake zote za Benki ya Posta na kujitoa katika biashara. Aidha, aliutaka uongozi wa Benki ya Posta kuacha kulalamika badala yake ufanye kazi kwa kushindana na watu wengine. Vikao vya kamati hiyo vinaendelea leo katika ofisi ndogo ya Bunge, jijini Dar es Salaam.
Hili ni swali ambalo waliulizwa washiriki wa shindano moja la urembo hapa Marekani. "Mrembo" mmoja aliwavunja mbavu watazamaji alipojibu bila kusita "remote control". Mimi pia nilicheka lakini baada ya kufikiri niliona kwamba pengine sikupaswa au sikuwa na haki ya kufanya hivyo. Pengine televisheni na remote control ni vitu vya muhimu sana katika maisha na utamaduni wa "mrembo" huyu. Sisi ni nani mpaka tumcheke?
Ati, swali hilo ungeulizwa wewe ungejibu nini? Mimi ningechukua jibu la mwalimu Mkude - mwalimu wangu wa Historia wa darasa la tano pale Sima Primary School (Bariadi mjini) aliyetufundisha kwamba MOTO pengine ndiyo ugunduzi muhimu kabisa kuliko mwingine wo wote ambao umeshafanywa na binadamu. Na nisingeshangaa pia kama ningechekwa kwa kutoa jibu kama hili!
"There aren't no answer. There ain't going to be any answer. There NEVER has been an answer. That's the answer."Gertrude Stein (1874 - 1946)
(1) "Inawezekana tatizo la paka kwa panya lingekwisha kama paka angefungiwa kengele shingoni: taabu ni kumpata panya wa kuifanya kazi hiyo.Na panya watakuwa wajinga sana wakidhani kuwa paka watajifunga au watafungana kengele shingoni!" Mwl. J. K. Nyerere (April 13, 1922 - October 14, 1999)
(2) "If you see a snake, just kill it - don't appoint a committee on snakes"Rose Perot - Mgombea uraisi wa Marekani 1992 na 1996 (1930 - )
(3) "Nobody can make you feel inferior without your consent"Eleanor Roosevelt - Mke wa FDR - rais wa Marekani (1884 - 1962)
(4) "Even if you are on the right track, you will get run over, if you just sit there"Will Rogers (1979 - 1935)
(5) "The most potent weapon in the hands of the oppressor is the mind of the oppressed" - Steve Biko - mpigania uhuru wa Afrika Kusini (1946-1977)
(6) "Before I was married I had three theories about raising children. Now I have three children and no theories" John Wilmot (1647 - 1680)
(7) "Wise men talk because they have something to say, fools talk because they have to say something"Plato (427 - 348)
SAVE ALBINO BENEFIT CONCERT
-
Blogu hii inapenda kuungana na *ALBINO FULANI* na washiriki wote katika
onesho hili maalum la kuwachangia ndugu zetu wenye matatizo ya ngozi
(ALBINO). Lic...
JK mwenyekiti mpya EAC
-
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki aliyemaliza muda wake Rais Paul
Kagame wa Rwanda akimkabidhi mwenyekiti mpya wa jumuiya hiyo Rais Jakaya
Mrisho k...
SCHOLARSHIP FORUM
-
*Napenda kuwatangazia ndugu wadau wote kuhusu maboresho niliyoweka katika
mtandao kuhusiana na mambo ya scholarships. *
*Nimeanzisha SCHOLARSHIP FORUM amb...
Obama amjibu mwana blog
-
President Obama's Responses to Yoani Sanchez's Questions
* *
* *
* *
* *
*Thank you for this opportunity to exchange views with you and your readers
...
Tutafute pazuri katika ndoa zetu.
-
Tumeona juu ya migogoro katika ndoa na visa na mikasa vya kukaribisha sijui
nani ili asuruhishe huku wakiwa na upendeleo na hivyo kuharibu zaidi.
Kumbuk...
HAPPY BIRTHDAY MALAYA WANGU!
-
[Tahadhari: hii ni barua ya Mheshimiwa MUME WA MTU!]
Kwa Mpenzi KIMADA!
Leo ni siku ya KUZALIWA KWAKO MPENZI na nakutakia MAISHA MAREFU na mafanikio
kat...
Ni kukosa muda ama kukosa kipaumbele?
-
Kimya cha blogu hii hakikutarajiwa ila huenda ni matokeo ya uzembe. Ni wazi
bado sijaweza kushika mbili bila kuponyokwa na kimoja. Na nasikitika sana
kwamb...
MAREKANI KUNA NJAA!!!
-
- Nakumbuka mwaka 2001 mama alipokuja kunitembelea wakati ule nikiwa bado
mwanafunzi katika Chuo Kikuu cha California, Los Angeles (UCLA). Alisha...
Tangazo la Scholarship Forum
-
Napenda kuwatangazia ndugu wadau wote kuhusu maboresho niliyoweka katika
mtandao kuhusiana na mambo ya scholarships.
Nimeanzisha SCHOLARSHIP FORUM ambayo...
Kombe la dunia lawasili nchini
-
Kombe la Dunia la fifa na Coca-Cola limewasili jioni hii na kupelekwa moja
kwa moja kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam. Kombe hilo liliwasili ...
Mwananchi Mimi! .........katika msimu mpya
-
mwananchi mimi nikipaka rangi ngao tayari kwa kuzitia maandishi ili zitumike
kwenye mashindano ya mpira baina ya shule za msingi kata ya Lupembe Njombe
m...
RIPOTI YA IDADI YA WATU DUNIANI
-
*Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira Dk Batilda Burian
akizinduwa Ripoti ya Idadi ya watu Duniani Kulia Mwakilishi wa (UNFPA)
Nchini Tanzania ...
NIKAPIGIWA “EMCHEKU”
-
* Usiku ndio muda muafaka
*
Ni usiku wa saa tatu hivi, niko kijijini kwa bibi Koero, na tuko jikoni
tunaota moto, huku akinisimulia simulizi mbalimbali juu...
THE MIRIAM.... "MIRIAM MAKEBA"
-
Wadau kama tunavyojua leo ni siku ya MIRIAM MAKEBA, leo ametimiza mwaka
mmoja kamili tangu afariki dunia, na kwa kumuenzi mama yetu ninawaletea
historia ...
HANDSOME ALIYEITIKISA KENYA-SEHEMU YA MWISHO.....
-
*Simon Matheri Ikere
*
*Mwili wa Simon Matheri baada ya kuuawa *
*
*
Ndugu wasomaji wa Blog hii, nimekuwa nikipokea ujumbe kupitia simu yangu ya
kiganjani...
SERIKALI IKIKIRI KUSHINDWA 'IPUMZIKE'
-
*RAIS APUMZIKIA KARIBU NA MIZOGA YA
MIFUGO NA WAKULIMA WENYE NJAA*
*Na Ndimara Tegambwage*
SERIKALI imesema isilaumiwe kwa ukame au vifo vya mifugo nchin...
Ukosefu wa UZALENDO, sumu ya Mafanikio Tanzania.
-
Tanzania ni nchi ambayo imebarikiwa kwa kuwa na rasilimali za kutosha kabisa
ambazo zikitumika vizuri zinaweza kubadilisha hali mbaya ya uchumi na
umasikin...
UK BORDER FORCE
-
Kama utafanikiwa kutembelea video hiyo hapo juu, utaweza kujionea ni jinsi
gani umaskini unavyoweza kuwa hatari kwa maisha ya wahamiaji kutoka
nchi/mab...
Maisha
-
Maisha kweli ni fumbo,lilogumu kufumbua,
Leo lakupiga kumbo,kesho wachekelea,
Punde yezaenda kombo,sharti kujikwamua,
Maisha ndivyo yalivyo,ya kesho huwezi j...
KIBANO SOMALIA
-
*Askari wa Jumuia ya Ulaya wakionyesha manjonjo yao ya jinsi ya kupambana na
wasomali wanaoteka meli katika bahari ya deep nje ya Afrika Mashariki
m...
-
WATU WANANANIJOKI
KUPATA MAGAZETI VIZURI KWASUKUMA NAMLIPA JAMAA 2000
GHARAMA ZA USAFIRI WA MUFUTA JUU YANGU MIMI
ASUBUHI KAMA KUMBILI NDIO HAUNA USUMBUFO
KI...
Nukuu kutoka Busanda
-
“*Shahada zote ambazo wananchi wanazo kwa mujibu wa sheria ni mali ya NEC,
sasa inakuwaje chama fulani kipite na kuandikisha upya majina na namba
zake...h...
2010 NAHISI WATU WATAKIMBIA TAALUMA ZAO!
-
*Ushindani utakuwa mkubwa
*
Ndugu wasomaji wa blog hii, kwanza samahani kwa kutoonekana katika kibaraza
hiki kwa muda mrefu kidogo. Hii nikutokana na mlundi...