Wednesday, November 11, 2009

"MSWAHILI" ANAPOFURAHIA MKE WAKE KUPATA BWANA WA KIZUNGU!

  • Katuni hii imenikumbusha mambo mawili: Kwanza suala la unene. Kitamaduni unene ulikuwa ni jambo la kujivunia na sidhani kama ulikuwa na madhara makubwa kama tunavyoambiwa sasa. Kila mtu alikuwa na ndoto ya kunenepa na vitambi vilionekana kama ishara ya kufanikiwa kimaisha. Watu walikuwa wanafanya kazi sana na tulikuwa tunakula vyakula vya kiasili - siyo kama sasa ambapo utandawazi umetuvuruga kabisa. Soma hapa, hapa na hapa kuhusu hili suala.
  • Pili: tabia yetu ya kutukuza wazungu, uzungu na vitu vyao vyote. Japo utawala wao uliisha, kisaikolojia jamaa bado wametuminya kweli kweli! Niliwahi kulalamika kuhusu suala hili hapa. Natumaini hatutafikia hii hatua aliyofikia huyu "Mswahili" mwenzetu kwenye katuni.

WAHAYA NA SENENE ZAO...

  • Ninapenda senene. Nilikuwa nawapenda sana wakati ule nikisoma kule Kahororo Bukoba.
  • Nilikuwa sijui kwamba ni chakula kizuri kilichokamilika mpaka nilipokutana na ukweli huu kutoka "Totally useless facts"
  • Totally useful fact: A pound of grasshoppers is three times as nutritious as a pound of beef!

Tuesday, November 10, 2009

WANAMUZIKI WA KIZAZI KIPYA - TUMIENI LUGHA ZENU ZA MAMA KAMA ALIVYOFANYA MTOTO WA DANDU!

  • Igeni mfano wa Mtoto wa Dandu, Saida Karoli na Mr Ebbo!

Niliwahi kuandika kwa kifupi juu ya matumizi ya Kisukuma katika nyimbo za Mtoto wa Dandu. Katika maakala hii fupi (ambayo imetoka katika gazeti la Kwanza Jamii la leo 10/11/2009), ninatoa wito kwa wasanii wa kizazi kipya kuiga mfano wa Mtoto wa Dandu, Saida Karoli na Mr Ebbo na kuimba katika lugha zao za mama au hata kutia vionjo vya "kikabila" katika nyimbo zao. Kwa kufanya hivi watakuwa wanatoa mchango wao chanya katika vita vinavyoendelea duniani kote kujaribu kuzitetea lugha za kienyeji ambazo ziko katika hatihati ya kuangamizwa na utandawazi.
*****************************************************************************

Wanamuziki wa Kizazi Kipya – Tumieni Lugha Zenu za Mama kama Alivyofanya Mtoto wa

Mtoto wa Dandu (Cool James)

Na Dkt. Masangu Matondo Nzuzullima

James Maligisa Dandu a.k.a Mtoto wa Dandu a.k.a Cool James a.k.a Ng'wanamalia a.k.a CJ Massive a.k.a Ng'wanawapelana a.k.a Nzokaihenge alikuwa na kipaji cha hali ya juu katika muziki. Ndiyo maana muziki wake ungali unapendwa sana miaka saba sasa tangu aage dunia kwa ajali ya gari tarehe 27/8/2002. Sikupata bahati ya kumwona lakini yeye pamoja na Saida Kalori na Mr Ebbo pengine ndiyo waimbaji wa kizazi kipya ambao kwa kiasi kikubwa wameweza kuzitukuza lugha zao za mama katika nyimbo zao - na hivyo kutupilia mbali ile dhana kwamba kizazi kipya hakiwezi kuguswa na nyimbo zenye ladha ya kikabila. Mtoto wa Dandu japo hakuimba katika Kisukuma moja kwa moja kama afanyavyo Saida Karoli, hapa na pale hakuisahau lugha yake ya mama iliyomkuza na kumlea kule Mwanza (Kisukuma). Hapa ni baadhi ya mifano tu ya matumizi ya Kisukuma katika nyimbo za mwanamuziki huyu mashuhuri aliyeondoka akiwa bado mchanga.

Jina lake mara nyingi alipenda kujiita Nzokaihenge yaani nyoka mwenye makengeza (nyoka makengeza). Alikuwa akijiita pia Ng'wanawapelana yaani mtoto mwenye hasira. Ni kawaida ya Wasukuma kujisifu na hapa ndicho alichokuwa akikifanya Mtoto wa Dandu. Ati, umeshawahi kuona nyoka mwenye makengeza maishani mwako? Unadra wa nyoka wa aina hii ndiyo ujumbe aliokuwa akitaka kuuwasilisha. Kipaji chake cha kipekee katika muziki kilikuwa nadra na muziki wake unaonyesha hivyo mpaka leo. Alipenda pia kujiita Ng'wanamalia - mtoto wa Maria. Hii inaonyesha kwamba pengine jina la mama yake ni Maria (Wasukuma hawana sauti " r" na hivyo mara nyingi huitamka kama "l" - kinyume na Wakurya)

Korasi mashuhuri inayosikika katika nyimbo zake nyingi inasema hivi:

Ng'wanamalia Kolobelaga lukumo lwane.
Jaga Ng'wigulya.
Jaga Ubagisha shikamoo abakolobela ng'weli...

Tafsiri

Mtoto wa Maria Umashuhuri wangu acha uenee sehemu zote
Uende juu zaidi

Uende ukiwasalimia shikamoo waliokwishasonga mbele Mashariki.


Kwingineko mara kwa mara anasikika akisema:

Nabiza wa galama.
Nulunagaja gubugeni nadiko gwigashiji gogo mpagi sumbi lya ng’hana

Tafsiri

Nimeshakuwa mtu wa thamani (heshima)
Hata nikienda ugenini siwezi kukalia gogo
Inabidi nipewe kiti kizuri cha kukalia

Inavyoonekana pia alikuwa ni mtu wa kutoa shukrani. Katika baadhi ya nyimbo zake anaonekana akimsifia na kumshukuru Jumanne Kishimba - tajiri mkubwa kule Mwanza na mmiliki wa duka kubwa la Imalaseko Supamaketi jijini Dar es salaam. Anasema hivi:

Jumanne Kishimba
Ulinamoyo gwape giti buluba
Hangi okumuka mpaga Bulaya

Tafsiri

Jumanne Kishimba
Una roho nyeupe mithili ya pamba
Tena umeshajulikana mpaka Ulaya

Akijisifu kidogo kama ilivyo kawaida ya Wasukuma anasema hivi:

Omasala adabunagwa nigo
Natemelwa bugota bonzoka ihenge

Tafsiri

Mtu mwenye akili haelemewi na mzigo (msemo wa Kisukuma)
Nimezindikwa na (madawa ya) nyoka mwenye makengeza

Huyu ndiye Mtoto wa Dandu ambaye hakuusahau utamaduni wake. Huyu ndiye Nyokamakengeza ambaye hakuionea aibu lugha yake ya mama. Huyu ndiye Mtoto wa Maria ambaye hakuuonea aibu Usukuma wake. Huyu ndiye Cool James ambaye alikuwa anatambua kwamba asingeweza kuwa “cool” bila kuwa na utamaduni wake mwenyewe.

Hebu fikiria kama wanamuziki wengi wa kizazi kipya wangeiga mfano wa Saida Karoli, Mr Ebbo na Mtoto wa Dandu, wakaimba nyimbo katika lugha zao za mama (Saida Karoli - Kihaya) au kuingiza vipengele vya lugha zao za mama katika nyimbo zao kama Mtoto wa Dandu (Kisukuma) na Mr Ebbo (Kimasai). Hatua hii ingesaidia sana kukikumbusha kizazi hiki kilichopumbazwa na “usasa” kwamba lugha zao za mama zipo, zina hadhi kama lugha nyingine yo yote na zina manufaa ya kimatumizi hata katika ulimwengu huu wa kisasa. Kwa hivyo dhana ya kwamba lugha hizi ni za kizamani, zimeshapitwa na wakati na hakuna sababu ya kujifunza au kuzizungumza tena haina ukweli wo wote. Ingefurahisha kama nini kama wanamuziki hawa wangetimiza wajibu huu wa kitamaduni na kuziunga mkono lugha zetu za asili katika wakati huu zinapopita katika mikikimikiki ya kudharauliwa na kuonwa kwamba hazifai tena.

Kimsingi huu ni wito wangu kwa waimbaji wa kizazi kipya - tumieni lugha zenu za mama katika nyimbo zenu. Kwa kufanya hivyo mtakuwa mnatoa mchango wenu wa thamani sana katika kuzipa uhai lugha zenu zilizowakuza na kuwalea, lugha ambazo zimo hatarini kufa baada ya vizazi vichache vijavyo kama mtaendelea kuzidharau, kuzionea aibu na kuziona kuwa hazina faida wala nafasi katika ulimwengu wa kisasa.

Mungu aendelee kumpumzisha salama Mtoto wa Dandu a.k.a Cool James a.k.a Ng'wanamalia a.k.a Ng'wanawapelana a.k.a Nzokaihenge a.k.a CJ Massive. Muziki wake kwa hakika utadumu!

Niandikie: profesamatondo@gmail.com
Nisome: matondo.blogspot.com
*****************************************************************************
Je, sasa unaweza kuvisikia vipengele vya Kisukuma nilivyovirejelea hapo juu katika nyimbo hizi za mtoto wa Dandu?



Monday, November 9, 2009

MISA ZA MBWA ILI KUVUTIA WAUMINI WAPYA MAKANISANI

  • Kwa watu wengi wa nchi za Magharibi mbwa ni sehemu ya familia na ana haki sawa na memba mwingine ye yote katika familia. Mbwa anaweza kuwa na bima ya afya na hata kuachiwa urithi; na anapofariki basi familia nzima huomboleza na kumzika kwa gharama kubwa.
  • Ili kuvutia waumini wapya, hivi karibuni makanisa kadhaa hapa Marekani yameanzisha misa maalum kwa ajili ya mbwa. Misa hizi zinadumu kwa nusu saa ambapo mbwa huombewa wakiwa wamejilaza vitandani huku wakifaidi vitafunwa mbalimbali. Kwa habari zaidi kuhusu habari hii gonga hapa.
  • Kwetu sisi Waafrika jambo hili linaonekana kama vile utani na sijui Wakristo wana maoni gani kuhusu misa za aina hii. Kazi kweli kweli!

NJIA MBILI BORA ZA KUMSHINDA MPINZANI WAKO KATIKA UGOMVI WA NGUMI

(1) Usipigane - hii ndiyo njia bora kuliko zote!

(2) Kama ni lazima upigane, zingatia siri hii. Ukiona unazidiwa - mtegee mpinzani wako anaporusha ngumi na wewe rusha hapo hapo tena kwa haraka ya kufumba na kufumbua. Hii ina matokeo matatu: Kwanza ngumi yake inaweza kukupata kwanza na kukufletisha kabla ya kwako haijatua usoni mwake (epuka hili lisitokee). Pili - ngumi yako inaweza kumpata kwanza na kumfletisha kabla ya kwake haijatua kidevuni mwako (hakikisha hili linatokea). Tatu - ngumi yake na yako zinaweka kutua kwa wakati mmoja na wote mkafletishana (na hii siyo mbaya sana). Nilifundishwa siri hii zamani sana. Tazama video hapa chini (dakika 1:18).

Saturday, November 7, 2009

UTAFITI: UNENE UNASABABISHA AINA NYINGI ZA KANSA KULIKO ILIVYODHANIWA

  • Mbali na kuwa chanzo kikuu cha magonjwa ya moyo, watafiti sasa wanasema kwamba unene ukiwemo ule wa futufutu (obesity) ni kisababishi kikubwa cha aina mbalimbali za kansa. Kwa mfano, watafiti sasa wanasema kwamba:
  • Unene unasababisha asilimia 49 ya kansa za mfuko wa uzazi, ikifuatiwa na asilimia 35 ya kansa za matumbo. Unene pia unasababisha asilimia 28 ya kansa za kongosho (pancreatic cancer), asilimia 24 ya kansa za figo, asilimia 21 ya kansa za kibofu cha mkojo, asilimia 17 ya kansa za matiti na asilimia 9 ya kansa za utumbo mkubwa (colorectal cancer)
  • Mbaya zaidi - watu wanene wanaongoza kwa kufa na kansa kwa sababu mara nyingi wanapopata kansa, kansa zao huwa hazitibiki kwa urahisi kama za wenzao wembamba
  • Mimi nadhani kwamba utafiti huu haukuzingatia sababu zingine zinazosababisha kansa yakiwemo mazingira na mfumo wa maisha ya watu. Nyumbani tuna/tulikuwa na watu wanene lakini kutokana na tabia ya watu kufanya kazi sana pamoja na kula vyakula vya kiasili (ambavyo havijabadilishwa kisayansi ikiwemo kutiwa mahomoni ya bandia, mbolea kali na madawa mengine) hata Shirika la Afya Duniani linakiri kwamba Afrika lilikuwa ni bara lenye wagonjwa wachache kabisa wa kansa. Na halafu utandawazi mpya ukaja.
  • Leo hii tumebadilisha maisha yetu, tunakula vyakula vile vile tunavyoletewa kutoka nchi za Magharibi na mfumo wetu wa maisha umebadilika. Matokeo yake sasa kuna mripuko wa kansa za kila aina na unene - jambo ambalo miaka michache tu liliyopita ilikuwa jambo la kujivunia - sasa linaonekana kuwa ni jambo la hatari! (Tazama pia hapa na hapa)
  • Isome ripoti kamili hapa na tazama video hapo chini kuhusu jambo hili la hatari.






Thursday, November 5, 2009

MPARE ANAPOJARIBU KUIENZI LUGHA YAKE

KUNUNUA MAUA WARIDI (ROSES) - KIELELEZO CHA MAPENZI AU MATOKEO YA KUSUTWA NA DHAMIRI?

  • Pengine hili ni swali la kipuuzi lakini imebidi niliulize kutokana na kisa kilichonipata jana.
  • Baada ya kutoka kazini nilipita dukani kununua mboga na nikaona maua waridi (roses) mazuri sana. Dazeni moja ilikuwa inauzwa dola 6.99 tena bado freshi kabisa na yamefungwa na kurembwa vizuri. Bei ya kawaida kwa maua kama haya ni dola 13.99 - 29.99.
  • Basi nikanunua dazeni moja ili kumpelekea mama watoto wangu.
  • Nilipotoka nje nikakutana na mwanaume Mmarekani mweusi ambaye alikuwa ameambatana na wanawake wawili.
  • Wale wanawake wakanisifia kwa kusema "Nice roses. She is going to be very happy today"
  • Yule mwanaume yeye akanitupia swali "Bro, what did you do?" Wale wanawake wawili wakaanza kucheka.

Ilinichukua muda kidogo kumwelewa lakini nilipopambazukiwa nilielewa alikuwa anamaanisha nini: mtu unamnunulia maua umpendaye wakati umemkosea na unataka kuomba msamaha. Wakati huo nilikuwa karibu na gari langu na sikupata muda wa kumjibu muuliza swali ambaye tayari alikuwa ameshaingia dukani.


Katika kipindi kimoja cha televisheni niliwahi kusikia wanasaikolojia wakisema kwamba mwanaume anayetembea nje ya ndoa/penzi ana uwezekano mkubwa zaidi wa kumnunulia mke/mpenzi wake "orijino" maua kutokana na kusutwa na dhamiri "sense of guilty". Wanasaikolojia hawa walitoa ushauri kwa wake/wasichana kufanya uchunguzi mara moja kama waume/wapenzi wao wataanza kuwapa zawadi na hata kuwanunulia maua wakati si kawaida yao. Hii inaweza kuwa ni matokeo ya ule msuto wa dhamiri.

Kule usukumani, ilikuwa lazima kumnunulia umpendaye zawadi - ndogo au kubwa - kulingana na uwezo wako. Kanga, hereni, viatu, "chachandu"- kitu cho chote ambacho kingemfanya ajisikie kwamba unampenda na kumjali. Nadhani, mbali na kuhongeresha, maua (waridi) pia yanatimiza lengo lilelile kama hizi zawadi za Kisukuma.

Kwa wanaume: Kwa nini mnanunua maua?

Kwa wanawake: Kama mpenzi/mume hana kawaida ya kukuletea zawadi/maua na mara moja anaanza kufanya hivyo, utajisikiaje? Ni kweli utaingiwa na wasiwasi?

KISWAHILI KIPYA - KUFULIA NI NINI?

Wakati mwingine sisi tulioko ughaibuni Kiswahili kipya kinatupiga chenga. Mnamaanisha nini siku hizi mnaposema eti Kanumba amefulia? Natumaini si tusi (la nguoni) au neno baya!

Tuesday, November 3, 2009

PROFESA/MKUU WA IDARA AACHIA NGAZI KWA TUHUMA ZA KUFANYA MAPENZI NA WANAFUNZI WAKE

  • Profesa mmoja mwanaume ambaye pia alikuwa mkuu wa idara mojawapo hapa chuoni ameachia ngazi kwa tuhuma za kufanya mapenzi na wanafunzi wake.
  • Inasemekana kwamba alikuwa nao wengi kwa mpigo na mpaka sasa wasichana watatu wameandika barua kuelezea jinsi walivyolaghaiwa naye.
  • Alikuwa akiwatumia wanafunzi wake picha zake za uchi kwa kutumia simu yake ya mkononi.
  • Alikuwa akilipwa dola 106,000 kwa mwaka.
  • Wanafunzi wake wa zamani wamtetea na kusema kwamba ni mmojawapo wa maprofesa wazuri sana - ingawa alipenda mno kuongelea mambo yake binafsi pamoja na familia yake.
  • Swali: Vipi tungekuwa na kasheria kama haka kule nyumbani? Mnakumbuka yale mambo ya mabinti "kushikwa" na hata "kudisco" wakimzembea Profesa? (sijui sasa kama mambo haya bado yapo yanatendeka au pengine utandawazi umeyamaliza!)
  • Kwa habari zaidi kuhusu hii ishu soma hapa na hapa

Monday, November 2, 2009

WANASIASA WA AFRIKA: IGENI MFANO WA JENERALI PERVEZ MUSHARRAF WA PAKISTAN

  • Imegundulika hivi karibuni kwamba kati ya dola bilioni 6.6 ambazo Marekani iliipatia Pakistan ili kuisaidia kupambana na magaidi wa Kitaliban na al-Qaida, ni dola 500 tu zilizotumika kwa lengo hilo.
  • Badala yake, rais aliyepita wa nchi hiyo, Jenerali Pervez Musharraf, alitumia kiasi kikubwa cha pesa hizo kujaribu kuinua uchumi wa nchi yake uliokuwa ukididimia. Pesa zingine zilitumika kuimarisha majeshi ya Pakistan (ambayo daima ipo katika hatihati ya vita dhidi ya jirani yake India).
  • Kilichonivutia katika ripoti hii ni kwamba hakuna panapotajwa kwamba Musharraf aliiba pesa hizi na kuzificha kwa manufaa yake binafsi - jambo ambalo pengine tungelitegemea kwa viongozi wengi wa Waafrika.
  • Badala yake, kiongozi huyu wa kijeshi, aliweka maslahi ya nchi yake mbele na kuamua kuzitumia pesa hizo kuinua uchumi wa nchi yake pamoja na kuimarisha majeshi yake ukiwemo ule mradi tata wa mabomu ya Nyuklia.
  • Ati, Afrika leo tungekuwa wapi kama viongozi wetu wangetumia pesa za misaada na mikopo (ambazo tumekuwa tukipewa/tukikopa tangu uhuru) kwa kuendeleza nchi zao badala ya kukimbilia kuzificha katika mabenki ya Uswizi?
  • Pamoja na matatizo yake yote, pamoja na udikteta wake wote - kwa hili namuunga mkono Jenerali Pervez Musharraf na huu ni mfano wa kuigwa na viongozi wa Afrika!

INGEKUWA TANZANIA HII TUNGESEMA NI USHIRIKINA!

=> Tazama vizuri mkono wa kushoto - kuna popo!
  • Jana hapa Marekani ilikuwa ni sikukuu ya Halloween- sikukuu ya kipagani iambatanayo na mambo ya kishetani shetani japo inasherehekewa pia na "Wakristo".
  • Basi jana katika mchezo wa mpira wa kikapu wa NBA kati ya San Antonio Spurs na Sacramento Kings kilitokea kisa cha kushangaza.
  • Mchezo ulipoanza, na bila kutegemea, alitokea popo ambaye alianza kukatiza uwanja kutokea goli hadi goli. Kidogo kulitokea mtafaruku huku wachezaji wakijaribu kumkwepa popo huyo. Mchezo ulisimamishwa kwa muda.
  • Popo huyo alipokuwa akijaribu kukatiza tena uwanjani, Manu Ginobili, mchezaji wa San Antonio Spurs kwa kasi ya kutisha alimtandika kwa kutumia mkono wake wa kushoto.
  • Popo alidondoka chini, Manu Ginobili akamwokota na kumpatia mfanyakazi aliyekuweko, akatia "sanitizer" mikononi na gemu likaendelea.
  • Matokeo: San Antonio Spurs 113, Sacramento Kings 94.
  • Ingekuwa nyumbani si ajabu hii ingesemwa kuwa ni kazi ya "kamati ya wazee" kumbe...
  • Tazama video hapa chini kumwona Ginobili akimfanyizia popo huyu mwenye bahati mbaya.
  • Baadaye alipata chanjo ya kuzuia vijidudu na aliwaonya watoto wasijaribu kuwaua popo kama alivyofanya kwani inaweza kuwa ni hatari.

Saturday, October 31, 2009

MGENI WANGU KARIBU NYUMBANI, LAKINI.....

Eti, utajisikiaje ukitembelea familia yenye mkeka wenye maandishi kama haya mlangoni?

Friday, October 30, 2009

UKIWA ROMA FANYA KAMA........

Ni Madame Secretary Hillary Clinton huyu akiwa Pakistan jana



NINA WASIWASI NA SHULE ZA SEKONDARI ZA KATA

Lengo letu ni zuri sana. Kila kata iwe na shule yake ya sekondari. Lakini tumejiandaaje? Kuna walimu wa kutosha katika shule hizi? Kuna vitabu? Kuna maabara? Mazingira kwa ujumla yakoje? Watoto kweli wanapata elimu kama inavyotakiwa? Picha hii ya mama mpishi wa shule imenitatanisha!

Thursday, October 29, 2009

KICHEKO NI TIBA - KUTOKA WAVUTI.COM

Matani kutoka Kenya kutoka tovuti mpya ya Wavuti.com (zamani nukta77.blogspot.com). Kama unavyoweza kuona kuna Ki-sheng hapa na pale; na sarufi na hasa upatanisho wa kisarufi na ngeli za majina zimeparaganyika (mf. ukikunywa maziwa inafika...). Nawapenda Wakenya kwa sababu wao hawatilii maanani sana mambo kama haya ya usanifu wa lugha kama tunavyofanya sisi Watanzania. Nimeandika makala yenye kurasa 25 inayoitwa "Kiswahili Sanifu au Kiswahili cha Tanzania?: Matatizo ya Usanifishaji katika Kiswahili Sanifu" Ikichapishwa nitawapa "link" hapa kwa wanaopenda haya mambo ya lugha. Watanzania - tunayo haki ya kudai kwamba Kiswahili chetu ndicho sanifu kabisa na kile cha Wakenya na hata kile cha Demokrasia ya Kongo (ambacho wenyewe wanadai kwamba ni sanifu pia) si sanifu?
*************************************************************************

1. Ati wee ni m-black mpaka ukiingia kwa dinga (gari), dirisha zinakuwa tinted!

2. Kwenu kuchafu mpaka mende zinatema mate, ati ‘THU’ hii hao (HOUSE) ni noma.

3. Vile wewe mfupi, ukipigwa picha ya passport inatokea full.

4. Kwenu nyi wakristu hata dogi zenu zikiona mwizi anaiba, zinawaambia “wee iba tu Mungu anakuona.”

5. Ati hao (house) yenu ina gate lakini hakuna fence.

6. We’ ni mshort mpaka ukikalia kwa pavement (sakafuni) miguu ina hang kwa hewa.

7. We mjinga mpaka uli-fail blood test.

8. Wewe ni mblack mpaka mosquito ikitaka kukuuma lazima itumie torch.

9. We ni mrefu mpaka ukikunywa maziwa inafika kwa tumbo ikiwa mala (MGANDO/MTINDI).

10. Wewe ni mweusi ukikanyanga makaa unawacha footprint za black kwa makaa.

11. Nyanyako (bibi yako) mzee mpaka chawa za nywele yake hutembea na bakora.

12. Ati nyinyi ni wengi nyumbani kwenu yaani buda (baba) yenu hajui majina mpaka huwaaddress kama wananchi. (KAMA RAISI ANAPOTOA HOTUBA)

13. TV yenyu ni Ndogo lazima ufunge jicho moja ndio uone picha.

14. Wewe mblack mpaka unasweat soot.

15. Wewe mnono mpaka ukivaa yellow watoto wanafikiria ni schoolbus.

16. Manzii (mpenzi) wako ni m ugly mpaka alikataliwa ku act horror (movie ya kutisha) Hollywood.

17. Nyumba yenyu ni ndogo mpaka lazima utoke nje kuchange mind.

18. Kwenyu nyinyi ni wengi mpaka kwa hao (house) kuna round-about.

19. Kwenyu nyinyi ni wadaft (WAJINGA) mpaka kupata driving license ilibidi mpelekwe boarding school.

20. Nywele za watoto wenyu ni ngumu mpaka mnazitumianga kama steel wool.

21. Mko wengi kwa hao (house) mpaka kuna rush hours na kukinyesha kunakuwa na jam.

22. Wewe ni mshort mpaka ukishuka kutoka kwa zile vitanda double decker lazima utumie parachute.

23. Ati TV yenu ni ndogo hadi wasee wa news huanza kwa kusema ...ati munatuona jamani?

24. Sistaako ni ugly mpaka monkey ikampatia ndizi.

25. We mblack mpaka ukikutana na mzungu afternoon anakushow good evening?

26. Ngombe yenu mzee mpaka inatoanga yogurt.

27. Kwenu kumekauka mpaka ngombe yenu hutoa milk powder.

28. Wee ni mzee mpaka ukiumwa na mosquito zinatema mate

29. Paka yenu noma mpaka iki shika panya inaitisha chumvi, fork na pilipili.

30. Kwenu nyinyi ni wengi mpaka mkipigwa family photo wengine wanatokea kama wame hang (ning’inia) kwa frame.

31. TV yenu ndogo mpaka wasee wa News (watangazaji wa habari) wamepiga magoti.

32. We mrefu mpaka ukianza kuvaa underwear mbichi by the time ifike kwa magoti imekauka.

33. Nyumba yenu ni chafu mpaka cockroach huvaa slippers (malapa).

34. Budako (baba yako) ni fala, alienda ku-buy ngombe akaona ikikojoa akasema, sitaki hiyo, imetoboka

RIPOTI YA USAWA WA KIJINSIA DUNIANI - TANZANIA TUNARUDI NYUMA?

Ripoti mpya inayoonyesha usawa wa kijinsia duniani imetoka na nchi za Skandinavia bado zinaongoza (#1-Iceland, #2-Finland, #3-Norway, #4-Sweden). Kwa Afrika, Afrika Kusini (nafasi ya 6) na Lesotho (nafasi ya 10) ndizo nchi pekee za Kiafrika zilizomo katika kumi bora. Kwa Afrika Mashariki Uganda ndiyo inaongoza (nafasi ya 40), Tanzania imeshika nafasi ya 73 wakati Kenya ni ya 98. Marekani - ambako wanawake bado "wanabaguliwa" hasa katika suala la usawa wa mishahara, ajira, pamoja na mambo mengine - imeshika nafasi ya 31. Nchi ya mwisho ni Yemen (#134) ikifuatiwa na Chad (#133) na Pakistan (#132).

Baadhi ya vigezo muhimu vilivyozingatiwa katika uandaaji wa ripoti hii ni pamoja na usawa katika ushiriki wa shughuli za kiuchumi, usawa katika upatikanaji wa elimu ya viwango vyote, usawa katika upatikanaji wa huduma za afya na usawa katika ushiriki wa masuala ya kisiasa. Unaweza kuisoma ripoti kamili hapa na orodha ya nchi zote inapatikana hapa. Tovuti ya World Economic Forum ambayo huchapisha ripoti hii inapatikana hapa.

Jambo la kushangaza ni kwamba ripoti hii inaonyesha kwamba Tanzania inarudi nyuma katika juhudi zake za kuleta usawa wa kijinsia. Mwaka 2006 ilichukua nafasi ya 24, mwaka 2007 (nafasi ya 34), mwaka 2008 (nafasi ya 38) na mwaka huu (nafasi ya 73). Hii ni kweli?

Hapa chini ni Saadia Zahidi - mmojawapo wa waandaji wa ripoti hii akielezea jinsi walivyoweza kuiandaa.



Swali: Nchi za Skandinavia pia ndizo zinaongoza kwa kuwa na talaka nyingi duniani. Je, kuna uhusiano kati ya usawa wa kijinsia na kiwango cha talaka au pengine hii imetokea kibahati tu?

Tuesday, October 27, 2009

RUSHWA WAKATI WA UCHAGUZI: NI KOSA LA WAGOMBEA AU WAPIGA KURA?

Tumefika mahali sasa – pengine kutokana na umasikini uliokithiri na ukosefu wa elimu-elimishi – wapiga kura wengi sasa wanafikiri kwamba rushwa wakati wa uchaguzi ni HAKI YAO. Ni ukweli ulio wazi kwamba bila kutoa rushwa huwezi kuukwaa udiwani na hasa ubunge. Nilikuwa nyumbani wakati wa uchaguzi mkuu uliopita na kimsingi nilichokiona hakikuwa “demokrasia” bali mashindano ya kutoa rushwa – kuanzia magunia ya chumvi, sukari, mabati, kanga, vitenge, baisikeli na wajanja waliweza kupata mpaka pikipiki, mitaji ya kufanyia biashara na hata kujengewa nyumba kabisa. Mzee wa vijisenti alikujulikana kwa kufanya iliyokuwa inaitwa “kufuru”. Ni kwa sababu hii sikushangaa sana niliposikia kwamba alikuwa akiandamwa na kashfa mbalimbali za ufisadi. Mabilioni ya shilingi aliyokuwa akiyamwaga wakati wa “kufuru” zake inabidi yalipwe kwani hakuna cha bure hapa duniani.


Basi kama hivi ndivyo, tumlaumu nani katika hili sakata la rushwa wakati wa uchaguzi? Tumlaumu mgombea ubunge ambaye anajua kwamba bila rushwa hatachaguliwa hata kama awe na sera nzuri namna gani, au mpiga kura ambaye hatoi kura yake bila kupewa sukari? Nini suluhisho la mduara huu usio na fundo? Hii kweli ni demokrasia?

Saturday, October 24, 2009

NYIMBO ZA KISUKUMA/KINYAMWEZI HIZI HAPA


UTAFITI: UBAGUZI (WA RANGI) HUANZIA UTOTONI

  • Watoto wenye umri wa miezi sita tu huanza kubagua.
  • Hata sisi weusi tunawabagua wenye rangi tofauti.
  • Inavyoonekana kila mtu ni mbaguzi.
  • Cha kushangaza ni kwamba, sisi weusi pia tunabaguana sisi kwa sisi.
  • Soma makala hapa.

Friday, October 23, 2009

JK HAPA UMEGONGA POINTI!

Kutoka gazeti la Tazama la Jumanne Oktoba 20, 2009 via Mjengwa.

WANASAIKOLOJIA: MASHOGA NA WASAGAJI HAWAWEZI KUBADILIKA AU KUBADILISHWA

Chama cha Wanasaikolojia wa Wamarakeni kimetoa tamko kikiwaonya wanasaikolojia na wafanyakazi wanaojishughulisha na afya ya akili kuacha mara moja kuwaambia wateja wao mashoga na wasagaji kwamba eti wanaweza kubadilika na kuachana kabisa na tabia hiyo. Wanasaikolojia hao wamepinga kwa kina “reparative therapy” – aina ya tiba ya kisaikolojia inayopendekezwa na kikundi kidogo cha wanasaikolojia (ambao wanaungwa mkono na wahafidhina wa Kikristo) ambao wanaamini kwamba mashoga na wasagaji wanaweza kubadilika/kubadilishwa. Kutokana na utafiti ambao wamefanya, wanasaikolojia hawa wanadai kwamba mashoga na wasagaji wakilazimishwa kubadilika wanaweza kutumbukia katika msongo wa mawazo na hata kuamua kujiua.


Dini imetajwa kuwa ndiyo chanzo kikuu cha mashoga na wasagaji kutaka kuachana na mtindo huo wa maisha ambao unapingwa sana na makanisa mengi ya kikristo. Badala ya kuwalazimisha kuachana kabisa na tabia hiyo wanasaikolojia wanapendekeza kwamba ni bora mashoga na wasagaji washauriwe kuishi maisha ya kutofanya mapenzi kabisa au kuhamia makanisa ambayo hayakatazi tabia hiyo.


Ushauri huu wa wanasaikolojia umepingwa vikali sana na Exodus International - mkusanyiko wa makanisa ya kilokole ambayo yanaamini kwamba nguvu za Yesu zinaweza kuvunja “minyororo” ya ushoga na usagaji. Raisi wa shirika hilo aitwaye Alan Chambers mwenyewe ni shahidi mzuri kwani nguvu za Yesu zilimfanya yeye mwenyewe azishinde tamaa zisizotakiwa za kufanya mapenzi ya jinsia moja alizokuwa nazo.


Tafiti mbalimbali zimeonyesha kwamba pamoja na athari za kimazingira, pengine ushoga na usagaji ni tabia ambayo mtu anazaliwa nayo hivyo haiwezi kubadilishwa kirahisi. Wengine wanakwenda mbali hadi kudai kwamba tabia hii itazamwe kama ugonjwa na ianze kutafutiwa tiba kama magonjwa mengine ya kawaida. Watu wa utambuzi mnasemaje kuhusu suala hili na ubadilishaji wa tabia kwa ujumla?


Kwa habari zaidi gonga hapa na unaweza kusoma maoni ya wasomaji. Ted Haggard anayerejerewa mara kwa mara na watoa maoni alikuwa ni mchungaji wa kilokole mashuhuri sana hapa Marekani na ndiye alikuwa kiongozi wa chama chao cha kitaifa kijulikanacho kama "National Association of Evangelicals". Alivuliwa madaraka yote Novemba 2006 baada ya kubainika kwamba alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na malaya mmoja wa kiume!

Thursday, October 22, 2009

KUCHEKA NI TIBA

HEBU TUKIRUHUSU KIZAZI KINACHOMALIZA MUDA WAKE KITUFUNDISHE KABLA HAKIJATOWEKA

Niliiona picha hii katika blogu ya Mjengwa na ikanikumbusha mama yangu mzazi. Ingawa yeye ni mzee sana lakini bado analima kishamba chake kidogo, anakwenda kutafuta kuni, kuchota maji kwenye kindoo chake, kuosha vyombo na kufanya kazi zingine kama kawaida. Ukimwambia akae apumzike basi mtagombana vibaya sana. Kipindi fulani nilijaribu kumleta Dar es salaam eti apumzike lakini haikuwezekana. Nilipomuuliza ni kwa nini alikuwa hataki kukaa mjini ambako kuna kitu jibu lake lilinishangaza. “Maisha gani haya ya kukaa tu bila kufanya kazi?

Jibu hili kidogo lilinishangaza kwani huyu ni mwanamke ambaye tangu nipate ufahamu wa kuelewa mambo sijawahi kumwona amepitisha siku bila kufanya kazi isipokuwa pengine akiwa mgonjwa – tena mgonjwa wa kweli kweli. Nilijaribu kutaka anieleze kulikuwa na ubaya gani kupumzika kidogo Dar es salaam baada ya miaka yote ile ya kufanya kazi. Jibu lake kwa swali hili lilinishangaza zaidi. Alidai kwamba akiacha kufanya kazi basi atakufa na sikujua kama alikuwa anatania ama la!

Tafiti mbalimbali zimeonyesha kwamba kufanya mazoezi mara kwa mara pengine ndiyo jambo la muhimu kuliko yote katika kulinda afya zetu pamoja na kuishi maisha marefu. Magonjwa mengi ya hatari kama vile magonjwa ya moyo, kisukari, shinikizo la damu, aina fulani za saratani na mengineyo yanachangiwa sana na maisha ya deko ambayo hatimaye huishia katika unene usiotakiwa. Nilishangaa kugundua kwamba mwanamke huyu mzee ambaye hakupata “bahati” ya kuingia katika darasa la kizungu na kusoma vitabu alikuwa analifahamu jambo hili vyema. Tulikubaliana na ilibidi “raha za mjini” nilizokuwa najaribu kumpa pale Dar es salaam nimpelekee kule kule kijijini kwake.

Mwaka 2001 alikuja huku Marekani kutembea na nilimpeleka kwa daktari kufanyiwa uchunguzi. Nilishangaa daktari alipowaita wenzake kuja kuona matokeo ya baadhi ya vipimo. Alituambia kwamba alikuwa hajawahi kuona mtu mzee namna ile ambaye alikuwa salama vile. Walipomuuliza alikuwa anakula chakula gani aliwajibu bila kusita “bugali”. Niliwafafanulia ugali ni nini na walishangaa kugundua kwamba ni wanga “carbohydrates” ambazo hapa Marekani kila mtaalamu wa lishe atakwambia usile. Ambacho hawakujua hawa madaktari ni kwamba huyu mwanamke mzee alikuwa anafanya kazi zaidi ya masaa matano kila siku tangu akiwa mtoto mdogo mpaka sasa. Tena chakula anachokula ni cha asili kabisa na hakina aina yo yote ya kemikali! Na kijijini kwetu kuna ajuza wengi ambao ni wazee zaidi kuliko mama na wako salama – hakuna dementia, hakuna Azheimer, hakuna saratani, hakuna kuvunjika mifupa hovyo hovyo, hakuna……

Je, kizazi cha sasa kinachoshinda kikitazama televisheni kitaweza kweli kuishi miaka mingi (bila magonjwa) kama kizazi hiki kinachomaliza muda wake? Kizazi cha sasa kinachokula vyakula vilivyobadilishwa na kujazwa kemikali na homoni za kila aina kitaweza kusafiri safari ndefu ya maisha kama hiki kinachomaliza muda wake? Hebu kizazi kipya na kijifunze yaliyo mema kutoka kizazi hiki kinachoaga kungaliko na muda bado.

Tuesday, October 20, 2009

MWALIMU NYERERE NA JANGWA LAKE LA KIITIKADI

Makala haya yametoka katika gazeti la Kwanza Jamii la leo - 20/10/2009

Mwalimu Nyerere na Jangwa Lake la Kiitikadi


(Ati, ni Nani Hasa Alikuwa Mfuasi wa Itikadi ya Mwalimu?)


Na Dkt. Masangu Matondo Nzuzullima


Katika diwani ya Karibu Ndani (Euphrase Kezilahabi, DUP, 1988:27) kuna shairi liitwalo “Azimio”. Beti chache za shairi hilo zinasema hivi:


Azimio sasa ni

Mabaki ya chakula

Kwenye sharubu za bepari

Kalamu inayovuja

Katika mfuko wa mwanafunzi

Vumbi zito

Baada ya ng’ombe kupita

Kilichosalia sasa

Ni punje za ulezi

Zilizosambazwa jangwani

Na mpandaji kipofu


Hivi ndivyo Kezilahabi – ajulikanaye pia kama Shaaban Robert wa Pili – alivyoliona Azimio la Arusha mwaka 1988. Nimelikumbuka shairi hili wakati nikitafakari Historia ya nchi yangu Tanzania hasa katika kipindi hiki ambapo nchi hii nzuri inaadhimisha miaka 10 tangu muasisi wake atoweke hapa duniani. Ni kweli Mwalimu alisambaza ulezi wake wa Ujamaa na Kujitegemea jangwani? Kama ni kweli, ina maana Mwalimu hakuwa na mfuasi wa kweli hata mmoja katika genge lake la Makomredi waliokuwa wakiimba ahadi za usawa wa binadamu? Ni nani hasa alikuwa mfuasi wa kweli wa itikadi kombozi za Mwalimu Nyerere? Ni Komredi Kingunge Ngombare Mwiru? Ni Edward Moringe Sokoinne? Ni Dr. Salim Ahmed Salim? Ni Rais Benjamin William Mkapa? Ni Mfaume Rashid Kawawa (Simba wa Vita)? Ni Rais Ali Hassan Mwinyi? Ni Jaji Sinde Warioba? Ni Oscar Kambona? Ni John Samwel Malechela? Ni Bibi Titi Mohamed? Ni Edward Lowasa? Ni Nani?


Msukumo hasa wa kuandika makala hii fupi niliupata kutokana na visa vifananavyo vilivyotokea kwangu mwenyewe na dada Subi Sabato wa nukta77.blogspot.com. Katika kuadhimisha miaka 10 ya kifo cha Mwalimu Nyerere niliweka mkusanyiko wa video 17 za Mwalimu Nyerere katika blogu yangu (matondo.blogspot.com). Subi Sabato pia alifanya hivyo hivyo katika blogu yake. Haukupita muda mrefu nilipata barua kutoka kwa watu waliokuwa wakijiita watumishi wa serikali wakinitaka niziondoe video za Mwalimu Nyerere katika blogu yangu mara moja kwani eti sikuwa na hati miliki na kwa hivyo nilikuwa navunja sheria. Waliendelea kunitisha kwamba nisipofanya hivyo basi sheria kali zingechukuliwa dhidi yangu. Subi Sabato naye alipata vitisho kama hivyo. Jambo hili lilinishangaza sana na nilijiuliza maswali mengi ambayo mpaka leo sijapata majibu na ndiyo maana naandika makala hii. Ina maana kuna mtu anamiliki hotuba za Mwalimu Nyerere? Niliwauliza watishaji wangu wanieleze aliko mmiliki wa hati miliki wa hotuba hizi ili niweze kuwasiliana naye lakini mpaka leo sijapata jibu. Mimi nilikuwa ninadhani kwamba hotuba za Mwalimu ni hazina ya taifa na Watanzania wote tuna haki ya kuzisikiliza bila kutishwa na mtu. Nilichukulia mfano wa hapa Marekani ambapo sheria za hati miliki ni kali sana lakini hotuba nyingi za marais wao ziko mtandaoni na ukienda katika maktaba za maraisi hao utaweza kuzisikiliza bure. Ni hazina ya taifa lao. Ni mali ya wote. Ni kumbukumbu ya historia ya nchi yao. Hotuba hizi hazimilikiwi na mtu! Hata hotuba nyingi za Rais Obama tayari zipo mtandaoni! Kuna tovuti nyingi zenye hotuba hizi na mojawapo nzuri ni hii hapa.


Mpaka nitakapopata ufafanuzi wa kina kuhusu ni nani hasa mmiliki wa hotuba za Mwalimu Nyerere, ninashawishika kuamini kwamba kuna kundi la watu ambao wanakerwa, kutishwa na kukoseshwa amani na hotuba za Mwalimu kwani wamegeuka kuwa wasaliti. Hawa inawezekana walikuwa ni watu wa karibu sana kwa Mwalimu na walijifanya kuwa “ardhi yenye rutuba” kwa mawazo na itikadi zake kumbe kwa ndani walikuwa ni “majangwa” tu yasiyootesha wala kustawisha cho chote. Ni mbwa mwitu waliokuwa wamevaa mavazi bandia ya “ukomredi” huku wakiimba na kudumisha “fikra sahihi za Mwalimu” kikasuku tu huku kimatendo wakiwa wamekakawana jangwani. Na baada ya Mwalimu kuondoka sasa wanajaribu kila wawezalo kufanya mawazo yake kombozi yasiwafikie Watanzania huku wakitumaini kwamba kwa njia hii hatimaye pengine Mwalimu ataweza kusahaulika.


Katika hotuba zake nyingi unaweza kumsikia Mwalimu akikemea rushwa na ufisadi; na utulivu wake wa akili, falsafa komavu na uwezo wa kuona mbali, kuonya na kutabiri mambo unaonekana waziwazi. Anasema waziwazi kabisa kwamba rushwa ikiachwa iendelee itaweza siku moja kuutikisa “msingi” wa nyumba (Tanzania). Mwalimu, pamoja na mapungufu yake yote, alitambua kwamba rushwa na utajiri wa kupindukia wa watu wachache kwa upande mmoja, na umasikini na uhohehahe wa asilimia 100 kwa walio wengi kwa upande mwingine siku moja utaitikisa Tanzania kwani ipo siku hawa wasio na kitu watachoka na kusema “liwalo na liwe”. Na hili likitokea hakuna jeshi litakaloweza kurekebisha mambo. Watu wakiamua wameamua na Historia imejaa mifano tele inayoonyesha kwamba nguvu za umma ni kama sunami. Badala ya kujaribu kurekebisha mambo na kuchukua ushauri wa Mwalimu kama vile mbuni asiye na upeo, kundi hili la “wanajangwa” inaonekana limeamua kuficha kichwa mchangani likiamini kwamba kutokomeza mawazo ya Mwalimu pengine ndiyo njia ya mkato ya kuendeleza “jangwa” lao wanalojaribu sana kuhakikisha kwamba linabakia kuwa jangwa. Kundi hili kwa hakika linajidanganya!


Hali hii inaibua hoja nyingine. Kutokana na “ujangwa” huu ambao sasa unaonekana waziwazi, haishangazi kuona kwamba sera nyingi za Mwalimu zilishindwa na kusema kweli inashangaza kidogo kuona kwamba baadhi ya sera zake zilifanikiwa mf. Elimu.


Historia inatuambia kwamba viongozi wengi waliofanikiwa ni wale ambao walikuwa na wafuasi wa kweli, wafuasi ambao walikuwa tayari hata kupoteza maisha yao ili kulinda na kutetea itikadi na harakati zilizoanzishwa na viongozi wao. Na hapa sizungumzii madikteta waliolazimisha itikadi zao kwa wafuasi wao kwa mkono wa chuma na kumwaga damu. Mara nyingi Historia huwa haina huruma na watu wa aina hii bali kuwatupa katika shimo lake la takataka. Huko ndiko waliko akina Mobutu Sese Seko Kuku Ngbendu wa Zabanga, Jenerali Bokasa, Jenerali Field Marshal Idd Amin Dada na wengineo wa aina hiyo.


Viongozi ambao hawakupanda mbegu zao katika “jangwa” mara nyingi hawakuwa hata na haja ya kuandika mawazo yao. Wafuasi wao wa kweli walifanya hivyo. Yesu Kristo hakuandika kitabu cho chote lakini wafuasi wake wa kweli walifanya hivyo. Buddha pia hakuandika kitabu cho chote. Wafuasi wake wa kweli walifanya hivyo. Lao-Tzu (mwanzilishi wa Taoism) pia hakuandika kitabu cho chote. Wafuasi wake wa kweli walifanya hivyo. Ferdinand de Saussure – mwanaisimu wa Uswisi ambaye anatambuliwa kama baba wa Isimu ya kisasa hakuandika kitabu cho chote pia wakati wa uhai wake. Wanafunzi wake walikusanya “notisi” na mihadhara yake aliyokuwa akiitoa wakati wa uhai wake na kuandika kitabu ambacho kilibadilisha kabisa mkondo mzima wa taaluma ya Isimu. Historia ina mifano mingi ya watu wa aina hii. Ni vigumu mno kwa kiongozi kufanikiwa kama amezungukwa na “jangwa” kama inavyobainika sasa kwa Mwalimu Nyerere.


Mwalimu Nyerere ataendelea kuenziwa na Watanzania, Waafrika na wapenda amani kokote duniani na juhudi za kundi hili linalojaribu kuzima mawazo yake linapoteza muda wake bure. Pamoja na makosa yake yote na kushindwa kwa sera yake ya msingi ya Ujamaa na Kujitegemea Watanzania wanaendelea kumuenzi na kumheshimu kiongozi huyu kwa msimamo wake na kutotetereka katika kutekeleza kile alichokiamini kwamba kilikuwa na maslahi kwa watu wake. Mwalimu Nyerere alihubiri na kutenda alichokihubiri na karibu kila kitu alichokitenda kilikuwa ni kitu ambacho aliamini kabisa kwamba kilikuwa ni kwa maslahi ya taifa lake changa. Jambo hili linawavutia sana Watanzania hasa wakiangalia maisha yake ya uadilifu aliyoishi – yeye pamoja na familia yake. Ni kwa sababu hii mimi naamini kwamba Nyerere na itikadi yake vitadumu!


Pamoja na “ujangwa” uliopo, wakati sasa umefika wa kumaliza ukiritimba katika hotuba (na vitu vingine ambavyo ni hadhina ya taifa letu). Hotuba za Mwalimu Nyerere siyo mali ya Redio Tanzania, mtu wala shirika au kikundi cha watu bali ni mali yetu sote. Ni wakati sasa wa kuziweka hotuba hizi katika mtandao. Hebu tuwe na tovuti maalumu yenye hotuba zote za viongozi wetu wote kuanzia Mwalimu Nyerere, Rais Mwinyi, Rais Mkapa na rais wetu wa sasa Rais Kikwete. Tovuti hiyo itangazwe na itunzwe vizuri kwani itakuwa mojawapo ya hazina muhimu sana kwetu kama Taifa kwa wakati huu na vizazi vijavyo. Wiki ijayo nitazungumzia kosa kubwa kuliko yote la Mwalimu Nyerere!


Niandikie: profesamatondo@gmail.com

Nisome: matondo.blogspot.com

Monday, October 19, 2009

TOTALLY USELESS FACTS.....

....You spend seven years of your life in the bathroom...

MAWAZIRI NA WABUNGE WENYE VYETI VYA KUGHUSHI


Wakati wengine wanasota miaka 6-10 (kwa hapa Marekani) kupata shahada za uzamivu (PhDs) "waheshimiwa" hawa wao waliamua kupita njia za mkato, wakaudanganya umma na kujipatia madaraka tena makubwa sana (na nyeti). Watachukuliwa hatua yo yote au ni "siasa" tu mtindo mmoja?

MAWAZIRI

(1) Dk. Mary Nagu (Viwanda, Biashara na Masoko)

(2) Dk. Diodurus Kamala (Ushirikiano wa Afrika Mashariki)

(3) Dk. Makongoro Mahanga (Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana)

(4) Dk. David Mathayo David (Kilimo, Chakula na Ushirika)

(5) Dk. Emmanuel Nchimbi (Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa-JKT)


WABUNGE

(1) William Lukuvi (Ismani-CCM)

(2) Victor Mwambalaswa (Lupa-CCM)


(3) Dk. Raphael Chegeni (Busega-CCM)

Kwa habari kamili soma hapa.

Sunday, October 18, 2009

UKAHABA AFRIKA KUSINI NA KOMBE LA DUNIA MWAKA KESHO (VIDEO)

Nimeiona hii video katika CNN. Eti kuna wasiwasi kwamba kombe la dunia mwaka kesho litaifanya biashara ya ukahaba kushamiri zaidi Afrika Kusini. Hii ni haki kweli au ni kwa sababu kombe hili linafanyika barani Afrika kwa hivyo ni lazima hawa jamaa wachonge? Kwa kuwa ukahaba ni tatizo la dunia nzima, je, ulikuwa tatizo pia hata katika nchi zingine ambako kombe hili limeshawahi kushindaniwa? Au pengine hali ya ukahaba Afrika Kusini ni mbaya zaidi kuliko sehemu zingine duniani? Nimetatanishwa!

Friday, October 16, 2009

KAMWE USINYWE POMBE NA KWENDA KUIBA

Mtu na babake wametoa kali ya mwaka kule Alabama. Baba ana miaka 37, mtoto wake wa kiume ana miaka 19. Kwanza walianza wakazitwika bia mpaka wakawa njwii halafu wakaamua kwenda kuvunja nyumba ili kuiba usiku wa manane. Kweli wakafanikiwa na wakaiba funguo za gari, dola karibia 200 na vito vyenye thamani inayokaribia dola 100 wakati wenye nyumba wakiwa wamelala.

Wakati wanajaribu kuondoka soo likabumburuka. Wenye nyumba wakaamka. Kwa akili za haraka haraka jamaa wakajibanza sehemu na hatimaye wakajificha chini ya kitanda katika chumba cha kulala. Soo likapoa. Baadaye baba akafanikiwa kuchepuka na kumuacha mtoto mvunguni mwa kitanda. Kumbe mtoto akawa amezimika mle mvunguni kutokana na kilevi.

Basi wenyeji wakalala kama kawaida mpaka asubuhi. Ndipo mama mwenye nyumba akashtukia ishu. Kuchungulia mvunguni mwa kitanda akamkuta mtoto mwizi akiwa ameutandika usingizi bila wasiwasi. Akakimbia kwenda kumwita jirani. Jirani alipokuwa basi mambo yakachangamka zaidi kwani yule kijana mwizi aliyekuwa amezimika mvunguni ni mjukuu wake. Polisi wakaitwa. Mwizi kuamshwa akawa anamuulizia baba yake. Polisi wakaondoka naye kwenda kumchukua baba yake na wote haooo korokoroni. Tangu hapo pombe siyo supu ati!

Itazame hii ishu hapa.

KWA MLIOKUWEKO: MNAZIKUMBUKA IMANI NA AHADI ZA MWANATANU?


Kumbe bado hazijabadilika na bado nazikumbuka karibu zote kwa kichwa. Duh!


IMANI YA CCM


  • Binadamu wote ni Sawa
  • Kila mtu anastahili heshima ya kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake
  • Ujamaa na kujitegemea ndiyo njia pekee ya kujenga jamii ya watu walio sawa na huru


AHADI ZA WANACHAMA WA CHAMA CHA MAPINDUZI


(1) Binadamu wote ni ndugu zangu na Afrika ni moja

(2) Nitaitumikia nchi yangu na watu wake wote

(3) Nitajitolera nafsi yangu kuondosha umaskini, ujinga, magonjwa na dhuluma.

(4) Rushwa ni adui wa haki, sitapokea wala kutoa rushwa.

(5) Cheo ni dhamana, sitatumia cheo changu wala cha mtu mwingine kwa faida yangu.

(6) Nitajielimisha kwa kadri ya uwezo wangu na kuitumia elimu yangu kwa faida ya wote.

(7) Nitashjirikiana na wenzangu wote kujenga nchi yetu.

(8) Nitasema kweli daima, fitina kwangu mwiko.

(9) Nitakuwa mwanachama mwaminifu wa CCM na raia mwema wa Tanzania na Afrika.

Thursday, October 15, 2009

HUYU RUBANI VIPI?

Mimi huwa sipendi kusafiri wa ndege na huwa napanda ndege tu kwa kuwa hakuna njia nyingine ya kusafiri kwa haraka zaidi. Mwaka 2006 kindege cha Precision Air kilihangaika kweli kutua pale Ibadakuli Shinyanga na ingawa nilikuwa naendelea mpaka Mwanza niliomba nishukie hapo hapo kwani sikutaka tena kwenda kupata mateso katika kutua kule Mwanza. Jamaa walinikubalia kushuka kwa shingo upande. Ningekuwa kwenye ndege kama hii sijui ingekuwaje. Kuna mwingine anayeogopa kusafiri kwa ndege au niko peke yangu? Watu wa utambuzi mna suluhisho kuhusu tatizo hili?



Tuesday, October 13, 2009

VIDEO MBALIMBALI ZA MWALIMU NYERERE HIZI HAPA

Katika kuadhimisha kumbukumbu ya miaka 10 tangu Muasisi wa Taifa letu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere atutoke, hizi hapa video zake mbalimbali. Japo zina urefu tofauti tofauti na zingine hazizidi hata dakika moja, kwa pamoja zinaonyesha falsafa yake tetezi na misimamo isiyolegalega ya Mwalimu. Natoa shukrani kwa wadau mliojitolea kuzitundika video hizi katika Youtube na Google Video. Kwa hotuba zaidi za Mwalimu Nyerere tembelea http://nukta77.blogspot.com. Mungu ibariki TANZANIA!

ANAKIRI SERIKALI YAKE ILIFANYA MAKOSA


CHIMWAGA 1995 (Nukta 77)


MUUNGANO




RUSHWA


UBAGUZI WA RANGI


MAZINGIRA


WALIMU




KODI


LINALOWEZEKANA LEO LISINGOJE KESHO


MIKOPO NA MADENI


NCHI YETU HAINA DINI (UNAWEZA KUISHIA 1:25)


HOTUBA KATIKA KIINGEREZA






KAMA SIKU ZAKO HAZIJAFIKA .....

Tarehe 15 Septemba, 2009 wanyongaji katika jimbo la Ohio kule Marekani walihangaika kwa zaidi ya masaa mawili wakijaribu kumnyonga muuaji, mbakaji na mteka nyara aitwaye Romell Broom (pichani) aliyekuwa amehukumiwa kunyongwa mpaka kufa kwa njia ya sindano ya sumu. Kutokana na matumizi yake ya madawa ya kulevya kwa muda mrefu, wanyongaji walishindwa kupata mshipa wa damu katika mikono yake ili kupitisha sumu ambayo hudhoofisha kwanza mwili na baadaye mapafu na moyo na hatimaye kusababisha kifo. Pamoja na mnyongwaji kujaribu kuwasaidia wanyongaji wake kwa kulala ubavu ubavu katika meza ya kunyongea na kujaribu kukunja ngumi ili kutunisha mishipa ya damu, wanyongaji hao hawakufanikiwa na baada ya masaa mawili Gavana wa jimbo la Ohio Ted Strickland aliamru unyongaji huo usimamishwe.

Walitaka kumnyonga tena baada ya wiki moja lakini wanasheria wake wakawa tayari wameshakata rufaa na kesi hiyo bado inaunguruma mahakamani. Na Romell Broom bado yupo tu anadunda. Kweli kama siku zako hazijafika hapa duniani binadamu hata wafanyeje ni bure! Kwa habari zaidi soma hapa. Mwenyewe anaeleza hapa yaliyomsibu siku ya Septemba 15, 2009 alipokutana na kifo uso kwa uso.

Monday, October 12, 2009

OBAMA KAZI ANAYO - JAMAA WANAFURAHIA ANAPOSHINDWA NA KUKASIRIKA ANAPOSHINDA

KWA NINI WAAFRIKA "TUNAKATAZWA" KUABUDU MABABU ZETU WALIOTUTANGULIA?

Jana asubuhi katika viwanja vya St. Peter Square kule Vatican Papa Benedict XVI alimtangaza "Baba" Damien De Veuster (January 3, 1840–April 15, 1889) kuwa Mtakatifu. "Baba" Damien De Veuster anakuwa Mtakatifu wa kwanza kutoka jimbo la Hawaii. Nilitembelea Hawaii mwaka wa 2005 kwa wiki mbili na Molokai -mahali alipoishi kwa miaka mingi akiwahudumia wagonjwa wa ukoma mpaka alipofariki (kwa ukoma pia) - ni mojawapo ya vivutio vya utalii.

Kama tunavyojua, "watakatifu" hawa (ambao ni lazima wawe wameshakufa) katika kanisa la kikatoliki huombwa na kuabudiwa; na inasemekana wana uwezo wa kutenda miujiza. Ili kutangazwa mtakatifu inabidi angalau miujiza miwili ya kiuponyaji itokee na iambatishwe moja kwa moja na anayetaka kutakatifishwa. Huu ndiyo utaratibu ambao Mwalimu Nyerere itabidi afuate kama kweli kanisa la kikatoliki linataka kumfanya kuwa Mtakatifu.

Swali langu ni hili: Mbona Waafrika wakisali na kuomba kwa mababu zao waliowatangulia wanaambiwa kwamba wanaabudu mizimu na wakiwaabudu hawa watu "waliotakatifishwa" na kanisa ni sawa?

NAKUMBUKA SIKU NILIYOTUNUKIWA ZAWADI KWA KUWA MWALIMU BORA WA MWAKA!

Katika vyuo vikuu vingi (na hata shule za msingi, sekondari na vyuo vinginevyo) hapa Marekani kuna tuzo linaloitwa "Teacher of the Year Award" Tuzo hili nadra hutolewa kwa mwalimu ambaye ameonyesha uwezo, ubunifu, mafanikio na njia za kipekee katika kufundisha. Mimi nami nililipata tuzo hili hapa Chuo Kikuu cha Florida mwaka wa masomo wa 2004-2005.

Ili kulipata tuzo hili ni utaratibu mrefu na uchaguzi wake hufanywa kwa uangalifu sana. Mbali na kupendekezwa, inabidi wanafunzi wako waandike barua wakieleza kwa kina jinsi ufundishaji wako ulivyowabadilisha na ni kwa nini wanafikiri kwamba unastahili kupata zawadi. Inabidi waseme ni kwa jinsi gani ufundishaji wako uko tofauti (na bora zaidi) na wa walimu wengine ambao wameshawahi kuwafundisha. Pia msimamizi wako (mkuu wa idara/kitengo) pamoja na walimu wenzako ni lazima waandike barua kukuunga mkono (watatembelea madarasa yako ili kujionea wenyewe jinsi unavyofundisha kabla hawajaandika barua zao). Halafu mwenyewe inakulazimu uandike insha ndefu kujieleza jinsi ufundishaji wako ulivyo tofauti na walimu wengine, falsafa inayokuongoza darasani na mtazamo wako mzima kuhusu nafasi ya mwalimu darasani na katika jamii kwa ujumla. Ni lazima pia uambatishe silabasi zote za masomo uliyowahi kufundisha, mifano ya mazoezi na mitihani ya mihula, "handouts" na vikorokocho vingine vingi. Halafu kamati maalumu iliyo chini ya "Dean" inakaa kupitia walimu wote waliopendekezwa na kufanya uteuzi wa mwisho.

Kwa upande wangu wanafunzi wenyewe walijikusanya wakashauriana wakaandika barua, wakawatafuta na wanafunzi wangu wa zamani nao wakaleta barua zao na kisha wakapeleka pendekezo lao katika kamati teuzi. Nilipata bahati ya kusoma baadhi ya barua zao na nilishangazwa na mambo ambayo waliyaeleza. Nilivutiwa na kuguswa mno!

Mbali na kupata bango la kumbukumbu (plaque), mshindi pia unapata cheki ya dola 5,000, unahongereshwa rasmi siku ya mahafali ya wanafunzi (na ukitaka unaweza kutoa hotuba) na unakaribishwa katika dhifa maalumu pamoja na rais wa chuo pamoja na viongozi wengine. Kwa ujumla hii ni siku nzuri ambayo mwalimu unaona kwamba juhudi zako pamoja na kipaji chako cha uelimishaji kweli kinaheshimiwa na kuthaminiwa. Inafurahisha na kutia moyo sana!

Mimi naamini kwamba huu ni utaratibu mzuri sana katika kuwaonyesha walimu wetu kwamba tunawajali na kuuthamini mchango wao na sioni ubaya wo wote kama nasi tukianzisha utaratibu kama huu (tena bila upendeleo wo wote) kwa walimu wetu katika ngazi mbalimbali.

Mwalimu wa binti yangu aliyeko darasa la pili alituambia hivi wazazi tuliokuwa tumekusanyika kumhongeresha (pamoja na kumpelekea zawadi) baada ya kushinda tuzo hili mwaka jana katika shule yake ".....Nitajibidisha zaidi mwaka ujao na wanafunzi wangu wataona mambo mapya na kujifunza kwa urahisi zaidi" Hili ndilo lengo hasa la tuzo hili - kuwapa motisha walimu kwa kuwaonyesha kwamba tunathamini na kuheshimu mchango wao - hasa wale wenye vipaji vya pekee na wanaojitolea sana katika kuelimisha watoto wetu!

Na siku moja natamani kurudi nyumbani na kutumia kipaji changu na mambo ambayo nimejifunza huku katika kuelimisha taifa langu!

ATI, MAFISADI NAO NI BINADAMU?

Niliulizwa swali hili na mwanafunzi anayesomea shahada ya uzamifu (Ph.D) katika Anthropolojia. Mwanafunzi huyu anafanya utafiti wake katika Jamhuru ya Kidemokrasia ya Kongo na alipokuwa huko wakati wa kiangazi mwaka jana alipata bahati ya kutembelea Gbadolite – yaliyokuwa makao makuu na makazi ya aliyekuwa raisi wa Zaire marehemu Mobutu Sésé Seko Nkuku Ngbendu wa Za Banga (Tafsiri - The all-powerful warrior who, because of his endurance and inflexible will to win, will go from conquest to conquest, leaving fire in his wake).

Mwanafunzi huyu hakuelewa inawezekanaje mtu anatumia mamilioni ya dola za umma kujijengea makao makuu ya kifahari kama yale wakati watu wengi katika nchi yake hawana huduma za msingi kabisa kama chakula, maji, matibabu, elimu na usafiri? Aliendelea kudai kwamba watu kama Mobutu kimsingi siyo binadamu kwani, kwa maoni yake, hakuna binadamu ambaye anaweza kufanya yale aliyoyaona kule Kongo na akabakia kuitwa binadamu.

Alipoondoka nilibaki nikifiriki hasa sisi binadamu ni nani na nini hasa kinachotufanya tuitwe binadamu. Ati, wana hisia na utu gani akina “Mobutu” wetu (ambao ni wengi sana barani Afrika) ambao hawana ubinadamu na wanachojali ni kunenepesha matumbo yao – wakiwaibia watu masikini na kuwasikinisha kabisa bila kujali cho chote? Ni kweli watu hawa wana furaha, hisia za ridhiko, mafanikio na utu? Huwa wanafikiri nini wakiona watoto wanasomea chini tena katika majengo mabovu wakati pesa za kununulia madawati na kujengea majengo ya shule wamezificha katika akaunti zao za siri? Huwa wanajisikiaje watoto mamilioni wanapokufa na malaria wakati pesa za kununulia vyandarua na dawa za malaria wamezitumia kujengea majumba ya kifahari? Huwa wanajisikiaje wakiwaona akina mama wakitembea maili sita kwenda kutafuta maji wakati pesa zilizotengwa kwa shughuli hiyo wamezitumia kujinunulia maghari ya gharama kubwa na kupeleka watoto wao nje kusoma? Wanajisikiaje? Mafisadi wana ubinadamu wowote? Ati, mafisadi ni binadamu?

Kwa habari kuhusu Gbadolite soma hapa. Hata Mtume Onesmo N. Ndegi wa Living Water Center Makuti Kawe Dar es salaam haelewi kabisa!

Friday, October 9, 2009

WITO KWA WANAUME WENZANGU - TUWE KAMA J.K (TUWE NA TABIA YA KUPIMA NA KUCHUNGUZA AFYA ZETU MARA KWA MARA)

Katika makala yangu fupi yenye kichwa Kwa nini wanaume (wa Kisukuma) hufariki mapema sana? ilibainika wazi kwamba mojawapo ya sababu ya jumla ya sisi wanaume kufariki mapema ni kutopenda kwetu kwenda hospitalini. Mpaka tukakubali kwenda hospitalini basi hapo ni lazima tuwe wagonjwa kwelikweli. Hapo ulipo hebu jiulize, ni lini ulikwenda kufanyiwa uchunguzi wa afya yako kwa mara ya mwisho? Hata kwa sisi ambao tuko huku ughaibuni ambako kusema kweli huduma za afya ni nzuri bado tunasubiri mpaka tuwe wagonjwa kabisa kabisa ndiyo twende hospitalini. Nimesoma uchunguzi wa afya ya Rais JK hapa chini na kuona kuwa ni jambo la maana sana kwa mtu kukaa ukijua kwamba uko salama. Wanawake pia inabidi mtusaidie katika jambo hili hata kama ikibidi mtumie zile mbinu zilizopendekezwa na Aristophanes katika tamthiliya yake ya Lysistrata. Tujijali, mtujali, tujaliane, TUOKOANE!

**************************************************************


DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA


Telephone: 255-22-2114512, 2116898
E-mail: press@ikulu.go.tz
Fax: 255-22-2113425

PRESIDENT’S OFFICE,

THE STATE HOUSE,

P.O. BOX 9120,

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


Mimi naitwa Dk. Peter Mfisi, ni mmoja wa madaktari wa Mhe. Rais. Nipo Ikulu. Nimekuwa na Mhe. Rais tangu wakati wa kampeni mwaka 2005 mpaka sasa. Mwenzangu ni Dk. Mohamedi Janabi ambaye ni daktari bingwa wa maradhi ya moyo katika Hospitali Kuu ya Taifa Muhimbili.

Nimewaiteni waandishi wa habari kufafanua masuala muhimu kuhusu afya ya Mhe. Rais kufuatia tukio la Jumapili iliyopita, Oktoba 4, 2009, pale Mwanza.

Tukio hilo limeleta mshtuko kwa watu wengi na kuendelea kuwa jambo linalozua mjadala kuhusu hali ya afya ya Mhe. Rais. Naelewa sababu ya wananchi kuwa na hofu na kuwapo kwa mjadala miongoni mwao. Rais ndiyo kiongozi wetu mkuu katika taifa na hivyo kuwa mwenye afya njema ndiyo matakwa ya kila mwananchi.


Naelewa fika kuwa kutokana na kiapo changu cha udaktari na maadili yangu ya kazi siruhusiwi kutoa hadharani undani wa habari yoyote inayohusu mgonjwa ninayemtibu bila ridhaa yake.

Hata hivyo, kwa kuwa huyo ni Rais wa nchi, na suala la afya yake ni kwa maslahi ya taifa na umma wa Watanzania kwa jumla, na kwa kuwa yeye ameridhia kutolewa kwa habari za afya yake ili watu wajue ukweli na kuondoa hofu, nimeamua kufanya hivyo.

Kama sote tujuavyo, Jumapili iliyopita, Oktoba 4, 2009 mwaka huu, Mhe. Rais Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa anashiriki katika sherehe za miaka 100 ya Kanisa la Africa Inland Church Tanzania (AICT) kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza, aliishiwa nguvu na kulazimika kwenda kwenye chumba cha mapumziko.


Baada ya mapumziko ya dakika 10 hivi, Mhe. Rais alirejea kwenye shughuli hiyo na kuendelea kushirikiana na waumini wa AICT hadi mwisho wa ratiba yake.

Ninapenda kusisitiza kuwa tukio la Mwanza limetokana na Mhe. Rais kuzidiwa na uchovu, na wala siyo kwa sababu nyingine yoyote ya kiafya. Wakati tukio hilo linatokea nilikuwepo, nilichukua vipimo muhimu kama daktari anavyotakiwa kufanya linapotokea tukio kama lile kwa mtu. Vipimo vyote vilithibitisha kuwa Mhe. Rais hakuwa na matatizo yoyote ya kiafya ambayo yangeweza kuhusishwa kuwa chanzo cha tukio lile.

Pressure yake ilikuwa 130/85mmhg ambayo ni kiwango cha kawaida kwa mtu wa umri wake. Mapigo ya moyo wake yalikuwa 76 kwa dakika ambayo pia ni ya kawaida. Sukari kwenye damu ilikuwa 5.5mmol/l ambayo nayo ilikuwa ya kiwango cha kawaida. Joto la mwili lilikuwa digrii 37.5 centigrade ambalo ni la kawaida. Mhe. Rais pia hakuwa na kiungo chochote kilichoonekana kutetereka, jambo ambalo lilithibitisha kuwa hakupata kiharusi.


Kutokana na matokeo hayo, sikuona hatari yoyote ya yeye kuendelea kushiriki katika sherehe hiyo muhimu kwa wakati huo. Ndiyo maana niliruhusu aendelee kushiriki sherehe zile mpaka alipomaliza na kuondoka.

Baada ya kurudi Dar es Salaam siku ile niliwasiliana na madaktari wanzangu wa hapa nchini na nje ya nchi ambao tumekuwa tunashirikiana nao katika kuchunguza na kufuatilia afya ya Mhe. Rais. Wote hao baada ya kuwasimulia kilichotokea na matokeo ya vipimo nilivyomfanyia Mhe. Rais, kwa tafakuri zao hawakuwa na wasiwasi wowote kuwa tukio hilo lilisababishwa na jambo jingine lolote, isipokuwa uchovu. Imani yao inatokana na ukweli kuwa wanaifahamu vizuri hali ya afya ya Mhe. Rais kwa kuwa wanahusika katika kuifuatilia mara kwa mara. Mmoja wao alimuona Mhe. Rais siku moja kabla ya kuondoka New York ambapo alipata nafasi ya kuchunguza afya yake.


Mimi na mwenzangu Dk. Mohammed Janabi, ndiyo wenye dhamana ya kuiangalia afya ya Mhe. Rais Kikwete kila siku. Tumekuwa tunafanya hivyo kwa zamu na wakati mwingine kwa pamoja, inapobidi kufanya hivyo. Katika kufuatilia hali ya afya ya Mhe. Rais tumekuwa pia tukimfanyia uchunguzi wa afya yake kwa vipindi maalum hapa nchini na nje ya nchi kwa vipimo ambavyo hapa nchini havipo. Napenda kuwahakikishia wananchi wenzagu kuwa katika miaka hii minne Mhe. Rais wetu amefanyiwa uchunguzi wa kina wa afya yake. Nadiriki kusema kuwa hakuna kipimo ambacho hatujapata kukifanya katika uchunguzi wa mambo muhimu ya afya yake.

Kwa sababu ya kuwatoa hofu wananchi na kwa vile mwenyewe anaridhia tufanye hivyo napenda kuwapa ufafanuzi kuhusu hali ya afya ya Mhe. Rais. Katika hali ya kawaida nisingefanya hivyo kwa sababu maadili ya kazi ya udaktari yanakataza. Naamini madaktari wenzangu wataelewa mazingira niliyokuwa nayo. Katika kufuatilia afya ya rais tumekuwa tunaangalia na kuchunguza mambo yafuatayo.

(a) Blood Pressure: Tunafuatilia kwa karibu sana hali ya nguvu ya msukumo wa damu (blood pressure). Tunampima mara kwa mara na mwenyewe tumempa mashine ya kujipima kila siku na anafanya hivyo. Kwa jumla pressure yake iko kwenye viwango vya kawaida. Aidha, uzito wake wa mwili unaendena ipasavyo na urefu wake. Mhe. Rais ni mtu mwenye mazoea ya kufanya mazoezi na yuko makini katika chakula anachokula. Sisi tunahusika kwa ukamilifu na kuelekeza kuhusu chakula anachokula. Hatuna matatuzi na Mhe. Rais kwa jambo hilo. Ana nidhamu ya kujipima pamoja na mazoezi na chakula.

(b) Moyo: Tumekuwa tunafuatilia kwa karibu hali ya afya ya moyo wake. Tumemfanyia vipimo kama vya ECHO, ECG na vinginevyo, na hatujabaini kuwepo tatizo lolote.

(c) Ubongo: Mwaka uliopita, 2008, Mhe. Rais tulimfanyia uchunguzi wa afya ya ubongo wake katika Hospitali ya Taifa Muhimbili hapa Dar es Salaam. Tulitumia kipimo cha CT – Scan na matokeo yameonyesha kuwa hana matatizo.

(d) Ini, Figo, Bandama, Kongosho: Mhe. Rais Kikwete kila mwaka tunapomfanyia uchunguzi wa jumla wa afya yake tumekuwa tunamfanyia kuchunguza viungo vyake muhimu vya tumboni kama vile ini, figo, bandama na kongosho. Tumekuwa tunafanya hivyo kwa kutumia kipimo cha ultra sound na kwa kupima damu yake kwa kutumia vipimo muhimu. Uchunguzi huo umebaini kuwa viungo vyote hivyo ni salama na vinafanya kazi vizuri.

(e) Mfumo wa njia ya Chakula: Mfumo mzima wa njia ya chakula (alimentary canal), yaani koromeo la chakula, tumbo, utumbo mdogo na utumbo mkubwa nao tumeufanyia uchunguzi wa kina kama kuna tatizo lolote katika kipindi cha miaka miwili hii. Mwaka 2007, tulimfanyia kipimo cha colonoscopy mjini Paris, Ufaransa, kuchunguza hali ya afya ya utumbo mkubwa. Matokeo ya uchunguzi yalionyesha kuwa utumbo wake mpana uko salama kabisa na hakuna matatizo yeyote. Daktari bingwa aliyemfanyia uchunguzi huo ameshauri kuwa Mhe. Rais hahitaji kufanya kipimo hicho tena mpaka baada ya miaka saba. Nakumbuka pia daktari huyo alimtania Mhe. Rais kuwa angefurahi kuazima utumbo wake.

Wiki mbili zilizopita, Mhe. Rais akiwa mjini New York, Marekani, alifanyiwa kipimo cha endoscopy kuchunguza kuanzia koromeo la chakula, tumbo, na utumbo mdogo. Matokeo ya uchunguzi huo yametoa majibu mazuri kuwa yako salama. Makusudio ya kufanya vipimo hivi viwili ni kuchunguza maradhi ya kansa na viashiria vya ugonjwa huo. Bahati nzuri hana maradhi hayo na wala hakuna dalili yoyote iliyoonyesha kuwapo viashiria vya kansa.

(f) Tezi la Shingo (Thyroid Glands): Aidha, wakati wa safari yake hivi karibuni majuzi mjini New York, Marekani, Mhe. Rais tulimfanyia uchunguzi wa afya ya tezi la shingo pamoja na kiwango chake cha utoaji wa homoni. Matokeo ya vipimo vyote vilivyofanyika yameonyesha kuwa hakuna matatizo yoyote.

(g) Tezi la Kibofu (Prostate): Septemba, mwaka huu, 2009, tulifanya uchunguzi wa hali ya afya ya tezi la kibofu (prostate) kwa kutumia mashine maalum na kwa kuchunguza damu yake. Vipimo vyote hivyo vimeonyesha hali si mbaya. Tezi lake lina ukubwa wa kawaida na hata vipimo vya viashiria vya kansa ya tezi hilo (PSA) tunavyofanya kwenye damu vilikuwa katika kiwango cha kawaida. Mhe. Rais hana matatizo ya prostate.

(h) Macho, Masikio na Pua: Tumeshamfanyia vipimo vya macho, masikio na pua na vyote viko salama. Mhe. Rais anavaa mawani lakini hayo si maradhi. Watu wengi baada ya kufikia umri wa miaka 40 si ajabu huhitaji mawani. Tunapofanya uchunguzi wa macho, ukiacha ile ya kuchunguza uwezo wa kuona, tunaangalia pressure ya macho na hali ya viungo vya nje na ndani ya jicho. Mhe. Rais hana matatizo yoyote.

(i) Damu: Tumekuwa tunamfanyia Mhe. Rais uchunguzi wa damu yake kwa vipimo mbalimbali vinavyotumika kutambua maradhi mbalimbali yahusuyo damu yenyewe na mwili mzima wa mwanadamu. Tumekuwa tunafanya hivyo kila baada ya miezi sita au panapojitokeza ulazima wa kufanya hivyo. Tumekuwa tunafanya hivyo hapa nchini na hata nchi za nje kwa nia ya kulinganisha matokeo yetu na kwa vipimo ambavyo sisi hatunavyo. Matokeo ya uchunguzi wetu yameonyesha kuwa Mhe. Rais yuko salama. Hana maradhi ya damu au kisukari, wala ukimwi, au ya wingi wa mafuta (cholesterol), ama ya kiwango cha madini, au ya tezi la kibofu, wala ya tezi la shingo, au ya ini, au ya homoni mbalimbali zilizoko mwilini na mengine n.k. Jambo pekee linalojitokeza ni kwamba Mhe. Rais ana damu nyingi. Hivyo, tumekuwa tunamshauri kupunguza damu kwa kuchangia Benki ya Damu.

Tunashukuru amekuwa anafanya hivyo karibu kila baada ya miezi sita. Damu nyingi inaweza kuwa na madhara mwilini lakini Mhe. Rais hajafikia kiwango cha kuwa ni tatizo la kiafya. Pia tunamshukuru kwa kuwa mwepesi kukubali kupunguza damu ambayo tunaitumia kuokoa maisha ya watu wengine. Hakuna hofu yoyote.

Napenda kusema wazi watu wote wasikie na kwa ukweli kwamba mimi na daktari mwenzangu yaani Dr. Mohamed Janabi hali ya afya ya Rais silo jambo linalotutia shaka wala kutusumbua au kutunyima usingizi.

Tatizo pekee ambalo limekuwa likimsumbua Mhe. Rais mara kwa mara ni maumivu ya shingo yanayotokana na kuumia zamani utotoni na wakati wa ujana. Kuumia huko ni kwa baadhi ya pingili za uti wa mgongo, sehemu ya shingo (cervical spine), kuathirika na kumsababishia maumivu. Mara nyingi matatizo ya namna hiyo huwapata wanamichezo na wanajeshi. Kutokana na shughuli wazifanyazo. Kuumia siyo jambo la kustaajabisha.

Tutakumbuka kuwa Mhe. Rais amekuwa mwana michezo hususan mchezaji wa basketball, mpira wa miguu na hata riadha wakati wa ujana wake. Pia alikuwa mwanajeshi. Ili kutambua vizuri tatizo la shingo ili tujue namna ya kumpatia tiba tumeshamfanyia vipimo vyote muhimu vya uti wa mgongo toka juu mpaka chini. Tumetumia x-ray, CT – Scan na MRI-Scan. Pia ameshaonwa na madaktari bingwa wa upasuaji wa mishipa ya fahamu hapa nchini na nje. Pamoja na kuwepo athari katika shingo, madaktari hao kwa dhati wameshauri kuwa kwa sasa maumivu yake hayahitaji upasuaji isipokuwa mazoezi ya viungo. Mhe. Rais amefundishwa mazoezi anayotakiwa kuyafanya na amekuwa anayafanya kwa nidhamu ya hali ya juu. Matokeo yake ni kupata nafuu kubwa. Ndiyo maana siku hizo haonekani kunyoosha shingo mara kwa mara kama ilivyokuwa zamani kwa wale wanaokumbuka. Tunafuatilia kwa karibu sana hali ya shingo yake. Tunamfanyia vipimo vya MRI na kuonana na madaktari bingwa mara kwa mara.

Mwisho

Napenda kabla ya kumalizia nisisitize tena kwa kusema kuwa mimi na daktari mwenzangu hatuna mashaka na hali ya afya ya Mhe. Rais. Afya yake ni nzuri, hana maradhi yanayotishia maisha yake au kupunguza uwezo wake wa kulitumikia taifa na watu wake. Pia maoni yetu hayo ndiyo maoni ya madaktari wa ndani na wa nje waliowahi kuhusika na uchunguzi wa afya yake.

Napenda pia kuwahakikishia kuwa, sisi madaktari wake, hatutachoka kufuatilia kwa karibu na kwa umakini mwenendo wa afya ya Mhe. Rais ili tujue mapema kama kuna jambo la kushughulikia. Kwa hili lililotokea, tutaendelea kuchunguza kama jambo lolote lililojificha ambalo hatujalibaini.

Kwa sasa napenda kurudia kusema kuwa hakuna ushahidi wa kitaalamu wa kusema kuwa kulikuwa na sababu nyingine zaidi ya uchovu. Rais aliondoka New York Septemba tarehe 30 saa nane ya usiku kwa saa ya hapa Dar es Salaam kuanza safari ya kurudi nyumbani. Aliwasili nyumbani saa saba ya usiku wa tarehe 1 Oktoba. Njiani alisimama London na Nairobi kuunganisha ndege. Hivyo basi, alisafiri saa 24 bila ya kulala vizuri. Isitoshe hata kwenye ndege alitumia muda mwingi akifanya kazi. Asubuhi na mapema siku ya Oktoba 2, aliondoka Dar es Salaam kwenda Arusha kufungua mkutano wa Wabunge wa Jumuiya ya Madola saa nne asubuhi. Baadae jioni yake alishiriki kwenye hafla ya chakula cha jioni alichowaandalia wabunge. Rais aliondoka saa sita usiku kwenda kulala. Hatuna hakika alilala saa ngapi kwani najua akiwa na kazi huchelewa sana kulala. Tarehe 3 Oktoba, 2009 alikuwa na mikutano mfululizo na viongozi na wananchi pale Arusha kabla ya kuondoka majira ya alasiri kwenda Mwanza. Alipofika Mwanza alikuwa na mazungumzo na wenyeji wake usiku ule mpaka saa nne ya usiku. Tulipofuatilia tuligundua kuwa hata siku hiyo nayo alichelewa sana kulala kwani walipondoka wageni wake yeye aliendelea kushughulikia hotuba yake mpaka karibu na alfajiri. Katika mazingira hayo kupata matatizo ya mwili kuchoka sana, na hata kukataa kuendelea kutumika, na kutaka kupumzika kama ilivyotokea si jambo la ajabu.

Mwisho kabisa napenda kuwahakikishia kuwa Rais yuko salama. Afya yake ni nzuri na haina shaka yoyote. Uchovu uliokithiri ndicho chanzo cha yaliyotokea Mwanza siku ile ya tarehe 4 Oktoba, 2009. Mimi na wenzangu katika Ofisi Binafsi ya Rais (OBR) tumejifunza na tumeazimia kuwa waangalifu zaidi katika kupanga ratiba ya kazi ya Rais.


Dr. Peter Mfisi
Ikulu, Dar es Salaam

Daktari wa Rais 08 Oktoba, 20

ATM NYINGI NCHINI HAZIFAI - WAZIRI

Nchi nyingi za Kiafrika (ikiwemo Tanzania) ni madampo tu ya kutupia bidhaa zisizofaa (na za bandia) kutoka nchi za Kimagharibi na CHINA. Kuanzia vyakula, madawa, vipodozi na sasa ATM. Watu mpaka wanauza dawa za Maralia za bandia! Mpaka kondomu za bandia! Wanaoingiza bidhaa hizi hawajui kwamba ni mbovu? Kama wanajua ni kweli tumekuwa wakatili kiasi kwamba mtu unauza dawa za Malaria au kondomu za bandia huku unajua kabisa kwamba kwa kufanya hivyo unaweza kuwa unahatarisha maisha ya wenzako moja kwa moja? Mamlaka inayohusika na suala hili inafanya kazi gani?
============================================================

ATM NYINGI NCHINI HAZIFAI - WAZIRI

Na Richard Makore



Naibu Waziri wa Fedha na Uchumi, Jeremiah Sumari.

Serikali imesema mashine nyingi za kutolea fedha benki (ATM), ni mbovu kwa kuwa huingizwa nchini kutoka nje baada ya kuonekana huko hazifai. Imesema hatua hiyo inasababisha kuwepo wimbi la watu kuiba fedha za wenzao kupitia mashine hizo bila wenyewe kujua.

Kauli hiyo ilitolewa jana jijini Dar es Salaam na Naibu Waziri wa Fedha na Uchumi, Jeremiah Sumari, alipokuwa akijibu maswali ya wabunge katika kikao cha Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Fedha na Uchumi. Sumari alisema kuwepo kwa mashine hizo ni hatari kwa usalama wa fedha za wananchi.

Alifafanua kuwa kuna nchi moja ambayo hakuitaja iliwahi kuhamisha mashine zake zilizokuwa mbovu na kuzipeleka nchi nyingine na kwamba tukio hilo linaonyesha kuwa hata hapa nchini ziliingizwa. Alishazishauri benki kuchukua tahadhari ili kuepusha wimbi la wizi kupitia ATM.

Hivi karibuni, Jeshi la Polisi liliwakamata raia wawili wa Bulgaria kwa tuhuma za kuiba kiasi cha Sh. milioni 70 jijini Dar es Salaam kupitia mashine hizo bila kutumia kadi. Wameufunguliwa mashitaka kortini.

Mbali na matukio ya wizi, baadhi ya ATM zimekuwa zikilalamikiwa na wateja wa benki kutokana na kuharibika mara kwa mara na wakati mwingine kutokuwa na mtandao, hivyo kuwasababishia usumbufu wa kutopata huduma.

Akizungumzia Benki ya Posta Tanzania ambayo serikali inamiliki asilimia 81 ya hisa, alikiri kuwa inahitajika sheria itakayoibadilisha kuwa kampuni ili iweze kufanya kazi kwa kushindana. Sumari alikuwa akijibu hoja mbalimbali za wabunge waliokuwa wakijadili utendaji wa benki hiyo.

Uongozi wa benki hiyo uliwaeleza wabunge kuwa unakabiliwa tatizo la mtaji mdogo, jambo ambalo linawafanya washindwe kufikia malengo waliyojiwekea. Wakichangia katika kikao hicho baadhi ya wabunge walisema bila sheria kufanyiwa marekebisho itakuwa vigumu benki hiyo kuweza kufanikisha malengo yake.

Mwenyekiti wa kamati hiyo, Dk. Abdallah Kigoda, alishauri mabadiliko hayo yafanyike haraka na serikali iache kutumia neno "ipo kwenye mchakato" kwani hali hiyo inakatisha tamaa.

Alisema neno mchakato halina mwisho na halisemi ni lini kazi husika au itaanza kufanyika, kauli ambayo iliungwa mkono na wabunge wengi. Kwa upande wake mbunge wa Wawi (CUF), Hamad Rashid Mohamed, alisema wananchi wamechoshwa na neno "mchakato" ambalo serikali inapenda kulitumia kwa kuwa halionyeshi ni lini itafanya kile inachokusudia kukifanya.

Aliishauri serikali kuuza hisa zake zote za Benki ya Posta na kujitoa katika biashara. Aidha, aliutaka uongozi wa Benki ya Posta kuacha kulalamika badala yake ufanye kazi kwa kushindana na watu wengine. Vikao vya kamati hiyo vinaendelea leo katika ofisi ndogo ya Bunge, jijini Dar es Salaam.

CHANZO: NIPASHE

Wednesday, October 7, 2009

"WHAT DO YOU CONSIDER TO BE THE MOST IMPORTANT HUMAN INVENTION?"

Hili ni swali ambalo waliulizwa washiriki wa shindano moja la urembo hapa Marekani. "Mrembo" mmoja aliwavunja mbavu watazamaji alipojibu bila kusita "remote control". Mimi pia nilicheka lakini baada ya kufikiri niliona kwamba pengine sikupaswa au sikuwa na haki ya kufanya hivyo. Pengine televisheni na remote control ni vitu vya muhimu sana katika maisha na utamaduni wa "mrembo" huyu. Sisi ni nani mpaka tumcheke?

Ati, swali hilo ungeulizwa wewe ungejibu nini? Mimi ningechukua jibu la mwalimu Mkude - mwalimu wangu wa Historia wa darasa la tano pale Sima Primary School (Bariadi mjini) aliyetufundisha kwamba MOTO pengine ndiyo ugunduzi muhimu kabisa kuliko mwingine wo wote ambao umeshafanywa na binadamu. Na nisingeshangaa pia kama ningechekwa kwa kutoa jibu kama hili!

Tuesday, October 6, 2009

TUNAPOKUNWA NA KIIMBWACHO WAKATI HATUJUI KIIMBWACHO

Ati, inatokeaje tunavutiwa na nyimbo ambazo wakati mwingine zimeimbwa katika lugha tusizozifahamu? Kwa nini tupende miziki ya Kongo wakati wengi wetu wala hatufahamu kinachoimbwa? Kwa mfano mimi napenda sana nyimbo za Marehemu Madilu MultiSysteme na sielewi HASA ni kwa nini!







Monday, October 5, 2009

KWA NINI WANAUME (WA KISUKUMA) HUFARIKI MAPEMA SANA?

Ni ukweli karibu dunia nzima kwamba wanaume hufa mapema zaidi kuliko wanawake. Katika mataifa yaliyoendelea (ambako umri wa kuishi kwa wastani ni zaidi ya miaka 75) wanawake huishi kati ya miaka 5-10 zaidi ya wanaume. Na katika watu wenye umri wa miaka 100, asilimia 85 ni wanawake. Wanawake wa Japan ndiyo watu ambao huishi miaka mingi zaidi hapa duniani (wastani wa miaka 86.05!)

Nilikuwa nafikiria leo kuhusu jambo hili na nikakumbuka hali ilivyo kule Usukumani. Wanaume wa Kisukuma hufa mapema sana - pengine wakiwa na umri kati ya miaka 50-60 tu. Kijijini kwetu kule Bariadi (kwa Bwana Mapesa na Mzee wa vijisenti), kwa mfano, wazee wa kiume wote wameshafariki na mwanaume ambaye naweza kusema ni mzee kabisa pale kijijini pengine ana miaka 55 hivi au zaidi kidogo. Hali ni hiyo hiyo hata katika vijiji vya jirani ambavyo navifahamu vizuri. Hata watu wanapostaafu wanaogopa kurudi vijijini kwa kuhofia kufa mapema.

Kwa upande mwingine, viajuza ambavyo vimefiwa na waume zao zamani bado vipo vingi sana. Jambo la kusikitisha ni kwamba kwa kiasi fulani jambo hili limehusishwa na imani za kishirikina na watu wanaamini kwamba wanaume wengi pengine huuawa na wake zao watoto waliozaa pamoja wakikua. Matokeo yake ni kwamba viajuza hivi navyo huishia kushukiwa kuwa ni vichawi na hivyo kutengwa na jamii na wakati mwingine huishia kucharangwa mapanga. Mkoa wa Shinyanga ndiyo unaongoza kwa mauaji ya vikongwe kutokana na imani hizi za kishirikina.

Mikoa mingine na hasa vijijini hali ikoje? Kwa nini wanaume (wa Kisukuma) hufa mapema vile? Wanajamii mna maoni gani kuhusu suala hili?

Saturday, October 3, 2009

ATI, AFRIKA ILIYOZOEA KUOMBAOMBA NA KUSAIDIWA, IMEPATA NINI KUTOKA KWA OBAMA?

Kuchaguliwa kwa Obama kuwa rais wa arobaini na nne wa Marekani kulipokelewa kwa vifijo na nderemo nyingi barani Afrika. Kulikuwa na matumaini makubwa kwamba Afrika sasa ilikuwa imepata "mkombozi" na mtetezi katika jukwaa la kiuchumi la dunia. Wengi waliamini kwamba kijana huyu machachari mwenye asili ya Kijaluo pengine alikuwa ndiye chanzo cha mwanzo wa kutatuliwa kwa matatizo mengi ya kiuchumi barani Afrika. Kama kawaida ya Waafrika, tulimwona Obama kama mtu wa kutusaidia na kutukomboa. "Mesiya" wetu alikuwa amefika. Oh, bahati iliyoje!

Safari ya kwanza ya Obama barani Afrika ilikuwa Ghana - taifa la kwanza barani Afrika kupata uhuru likiwa chini ya mmojawapo wa viongozi wa Kiafrika wanaoheshimika sana - Kwame Nkrumah. Naona viongozi wengi wa Afrika na Waafrika wengi walivunjika moyo Obama aliposhindwa kuahidi misaada kemkem kwa bara la Afrika. Akiwa Ghana Obama (kimsingi) aliwaambia Waafrika kwamba ukombozi ulikuwa mikononi mwao wenyewe na misaada ya Marekani (kama ipo) itaelekezwa kwa nchi zile ambazo zinajibidisha kujiendeleza zenyewe, nchi zinazoheshimu demokrasia, haki za binadamu kwa raia wake na zenye uongozi bora unaojitahidi kupambana na ufisadi. Kwa Waafrika waliozoea kuombaomba, rushwa na kupewa vya bure pamoja na kukopeshwa (wakisahau kwamba daima kukopa harusi lakini kulipa matanga), maneno haya ya Obama yalionekana kama msumari wa moto.

Obama ni raisi wa Marekani na daima ataweka maslahi ya nchi yake mbele. Kama alivyosema Mwalimu Nyerere wakati akiwahamasisha Watanzania kumtandika Idd Amin katika vita vya Kagera "nia tunayo...uwezo tunao" na tukiamua kutumia raslimali zetu vizuri tunaweza kutatua matatizo mengi tu yanayotukabili bila kutegemea misaada kutoka nje. Kwa hakika, jukumu la kujikomboa ni letu sisi wenyewe!

Sijui kama Waafrika tulimsikiliza vizuri na kumwelewa Obama, au tulivunjika moyo kwamba hakutupa misaada na mikopo (ambayo bila uongozi bora nayo huishia katika mifuko ya wachache). Waafrika wengi pengine wangali bado wanajiuliza...Obama ameitendea nini Afrika wakati tayari ameshaionyesha (au niseme ameshaikumbusha) njia ambayo kwayo inabidi kupitia ili hatimaye iweze kuifikia nchi yake ya ahadi. “Development depends upon good governance”

Hapa chini ni baadhi ya nukuu za Obama kutoka katika hotuba yake ya Ghana:

“Development depends upon good governance”

“It is easy to point fingers, and to pin the blame for these problems on others,”

“You have the power to hold your leaders accountable and to build institutions that serve the people.”

“America will not seek to impose any system of government on any other nation,” “What we will do is increase assistance for responsible individuals and institutions, with a focus on supporting good governance.”

“The purpose of foreign assistance must be creating the conditions where it is no longer needed. America can also do more to promote trade and investment. Wealthy nations must open their doors to goods and services from Africa in a meaningful way.”

Friday, October 2, 2009

MASIKINI MKAPA - MARA JOTO, MARA BARIDI.....PRESHA INAPANDA NA KUSHUKA!

Thursday, October 1, 2009

HII AKAUNTI NDIYO ILIMWAGIWA DOLA MILIONI 700 NA RAIS BUSH?




ATI, MWAKA 2012 NDIYO UTAKUWA "MWISHO WA DUNIA"?

Kituo cha runinga cha History Channel cha hapa Marekani kimeanzisha kipindi kipya kiitwacho Nostradamus-effect. Nostradamus alikuwa mtabiri maarufu wa Kifaransa ambaye wataalamu wengi wa mambo ya utabiri wanadai kwamba alitabiri kwa usahihi kabisa, mbali na mambo mengine, kuzuka kwa Alexander the Great, Adolf Hitler, mashambulizi ya Septemba 11 na hata urais wa Obama. Kwa habari zaidi kuhusu kipindi hiki tembelea hapa.

Katika kipindi cha Nostradamus-effect cha wiki jana wataalamu mbalimbali wa Anthropolojia, Fizikia, Historia, Haidrofizikia na taaluma mbalimbali walijadili kwa kina utabiri maarufu wa Nostradamus kwamba dunia itagharikishwa kwa maji na moto ifikapo mwaka 2012. Walitaja kwamba pengine hili si jambo la kushangaza sana ukizingatia kuyeyuka kwa kasi kwa barafu kunakotokea sasa katika pembe ya kaskazini ya dunia. Athari za tukio hili hazifahamiki na binadamu anaonekana hajali. Wengine walisema kwamba mabomu machache tu ya Atomiki yakiripuka (ama kwa makusudi au kwa bahati mbaya) basi dunia nzima inaweza kugharikishwa na mawingu ya miali hatari kabisa ya atomiki.

Jambo la kushangaza ni kwamba hata kalenda ya Wamaya (ambao himaya yao kubwa na yenye nguvu na maendeleo ya juu ya kisayansi na kiteknolojia iliangamia kutokana na sababu ambazo hazijulikani mpaka leo) inatabiri kwamba dunia itafikia mwisho wake mwaka 2012. Inaaminika kwamba Wamaya (Mayans) walikuwa na uwezo mkubwa wa utabiri na kalenda yao imeonyeshwa kwamba iliweza kutabiri kwa usahihi matukio mbalimbali yakiwemo kupatwa kwa jua, miripuko mikubwa ya volkeno, vita n.k. Cha ajabu ni kwamba hawakuweza kutabiri kuangamia kwa dola lao wenyewe.


Sijui kama wasiwasi huu ni wa kweli au ni yale yale ya Y2K (mnakumbuka?). Lakini ukiwasikiliza vizuri wanasayansi hawa, karibu wote wanakubaliana kwamba dunia itakumbwa na misukosuko ya kimazingira ambayo itasababishwa hasa na mabadiliko ya haraka ya hali ya hewa na mambo mengineyo ingawa hawajui misukosuko hii itatokea lini. Kuna haja ya kuwa wasiwasi?

Wednesday, September 30, 2009

ATI, WATOTO WA KIMAREKANI WANA AKILI KULIKO WATOTO WA KIAFRIKA?

Mwaka huu nimejitolea kufundisha wanafunzi wa darasa la tatu katika shule moja ya msingi (darasa la kwanza mpaka darasa la tano). Niliamua kufanya hivi ili niweze, mbali na mambo mengine, kujifunza na kuuelewa vizuri mfumo wa elimu wa hawa wenzetu "walioendelea" na kusema kweli nimeona, nimejifunza na kushangazwa na mengi.

(1) Shule zao nyingi zina karibu vitu vyote vya muhimu ambavyo vinawawezesha wanafunzi kujifunza kwa vitendo. Kuna maabara nzuri, chumba cha kompyuta na vitu vingine muhimu.

(2) Elimu yao inamakinikia zaidi vitendo na wanafunzi wanasisitizwa sana kufanya majaribio yao wenyewe ama wakiwa shuleni au nyumbani wakisaidiwa na wazazi wao. Tafiti mbalimbali zimeonyesha kwamba wanafunzi hujifunza vizuri zaidi wanaposhirikishwa kivitendo katika kujifunza. Elimu ya kukariri kwa kweli imeshapitwa na wakati na haimsaidii mtoto kujifunza hadi kufikia upeo wake kiakili.

Nimeshangazwa na ukweli kwamba mtoto wa darasa la pili wa Kimarekani anaweza kukueleza vizuri kabisa na kwa kutumia maneno yake mwenyewe mfumo mzima wa maji (hydrological cycle) pamoja na dhana mbalimbali za msingi katika sayansi kama usumakishaji (magnetism), umeme, nguvu ya uvutano (gravity), mwendo (motion), ukinzani (friction), mfumo wa sayari (planetary system), sauti, sifa za mada (properties of matter), hali ya hewa na majira, nishati (energy) pamoja na dhana nyinginezo. Ni kutokana na ukweli huu kwamba nilianza kujiuliza kama wanafunzi hawa wana akili zaidi kuliko wanafunzi wa nyumbani. Nilikumbuka pia utafiti mmoja ambao ulilinganisha watoto wa Ulaya na wa Afrika. Utafiti huo ulionyesha kwamba watoto wa Afrika wako "slow" wakilinganishwa na wenzao wa Ulaya. Kwa nini?

Mbali na matatizo mengi yanayoukumba mfumo wetu wa elimu (ambayo mengi ni ya kujitakia tu), tatizo kubwa kabisa kwa maoni yangu ni lugha ya kufundishia. Ni ukweli wa kisayansi kwamba elimu ya kweli inawezekana tu pale mtoto anapofundishwa katika lugha anayoifahamu vizuri. Ili mtoto aweze kukomaa na kufikia kilele chake cha kiakili ni lazima afundishwe kwa lugha yake mwenyewe. Cha ajabu ni kwamba mtoto wa Kiafrika, kinyume na mtoto wa Kichina anayefundishwa kwa lugha yake ya mama, kinyume na mtoto wa Kijapani anayesomeshwa kwa lugha yake ya kwanza, kinyume na mtoto wa Kithailand anayefundishwa kwa lugha yake ya mama, kinyume na....mtoto wa Kiafrika yeye anafundishwa katika lugha ambayo HAIELEWI, lugha ambayo haifundishwi vizuri na hata wafundishaji wenyewe hawaimudu vizuri. Matokeo yake elimu inakosa maana na inageuka kuwa zoezi la kukariri tu - hata kwa dhana zilizoko katika mazingira yake mwenyewe kama hii ya "hydrological cycle", mmomonyoko wa udongo, mito n.k. Ati, kukariri "Newton's Laws of Motion" kikasuku kweli ni elimu?

Bila mabadiliko ya kweli katika mfumo mzima wa elimu mimi naamini kwamba Afrika tutaendelea kuwa washangiliaji tu katika mchezo wa kisiasa, kitamaduni na kiuchumi unaochezwa hapa duniani. Mbaya zaidi hata "wasomi" wachache tunaowapata kupitia mfumo wetu huu wa kukaririshana kikasuku hasa katika nyanja za utabibu na uhandisi wanakimbia kwenda nje na hakuna anayejali.

Watoto wote wako sawa na dai la kijumla kwamba eti watoto wa Ulaya/Kizungu/Kimarekani wana akili kuliko watoto wa Kiafrika halina ukweli wo wote wa kisayansi. Kama watoto wa Ulaya/Kizungu/Kimarekani wanaonekana kuwa "sharp" ni kwa sababu elimu yao iko makini zaidi na wanayo bahati ya kufundishwa katika lugha yao wenyewe. Kwa bahati mbaya sana mtoto wa Kiafrika hana bahati hiyo!

Monday, September 28, 2009

HIKI CHOO KIMENIKUMBUSHA MBALI SANA - FUNZO KWA WATUNGA SERA

Kwa wale ambao mmekulia mijini pengine hamjawahi kutumia choo kama hiki. Lakini kwa wale waliokulia mijini, choo kama hiki ni cha kawaida sana na mpaka leo ukienda vijijini vyoo vya aina hii bado utaviona!

Nakumbuka katikati ya miaka ya 80 kulikuwa na kipindupindu kijijini kwetu na serikali iliamru kila familia kuchimba choo pamoja na kuchemsha maji ya kunywa. Kila siku ungewaona vijana wa mgambo wakizunguka kila kaya kukagua kama kulikuwa na choo na kama maji ya kunywa yalikuwa yanachemshwa.

Ambacho wanamgambo hawa hawakukijua ni kwamba watu walitii amri ya serikali na kuchimba vyoo lakini walikuwa hawavitumii, na walikuwa wanachemsha maji ya kunywa na kuyaweka katika mtungi mkubwa sana kwa ajili ya kuwaonyesha wanamgambo hawa wakija lakini maji haya walikuwa hawayanywi. Wakati ule sikuelewa ni kwa nini wakati kweli kipindupindu kilikuwepo na kilikuwa kinaua watu.

Baadaye niligundua kwamba kulikuwa na tatizo: watu walikuwa hawaamini kwamba kipindupindu kilikuwa kinasababishwa na kunywa maji machafu bali ushirikina. Eti watu walikuwa wanarogana na kusingizia kipindupindu. Kwa mantiki hii, watu hawakuona sababu ya kunywa maji yaliyochemshwa (ambayo walidai hayana ladha nzuri kama yale ambayo hayakuchemshwa) na kutumia vyoo (ambavyo walidai vinanuka sana) wakati wanajua kwamba haisaidii cho chote katika kuzuia kipindupindu.

Serikali nayo kwa upande wake haikuchukua hatua yo yote kuwaelewesha watu kwa kina kuhusu visababishi, kinga na tiba ya kipindupindu. Yenyewe iliweka amri tu ya kuchimba vyoo na kuchemsha maji ya kunywa ikidhani kwamba watu hawa wa kijijini "wasiofahamu" cho chote wangetenda kama walivyoambiwa. Mpaka leo, sera nyingi (hata ziwe nzuri namna gani) zinashindwa kwa sababu zimepandikizwa tu kwa walengwa wake - hasa walengwa hao wakiwa ni watu wa kijijini ambao inasadikiwa na kuaminika kwamba ni watu ambao wanastahili kuambiwa na kuelekezwa nini cha kufanya. Sera nyingi za serikali na mashirika yasiyo ya kiserikali zingepata mafanikio mno kama zingejipa muda wa kuwaelewa walengwa wake - zikajibidisha sana kujumuisha maoni, maarifa na uzoefu wao katika uandaaji na upangaji wa sera hizo. Bila kufanya hivi, tutaendelea kucheza katika mduara usio na fundo huku tukiwalaumu watu wa kijijini kuwa ni "wajinga", wasio na elimu, wasiostaarabika, wasiosaidika wakati ukiangalia na kuchunguza vyema - pengine watunga sera, "wasomi" na mabingwa wa kuelekeza ndiyo wajinga!

Picha ni kutoka kwa Mjengwa

Saturday, September 26, 2009

NI LAZIMA TUKOJOE "VICHOCHORONI"?

Mwanafunzi mmoja mzungu aliyekuwa anafanya utafiti kule Tanga, Mbeya na Dar es Salaam alinieleza kushangazwa kwake na tabia ya wanaume kukojoa hovyo hovyo mijini. Swali hilo lilinikumbusha Mtanzania mmoja ambaye alipigwa faini kali pamoja na kupewa adhabu ya kuokota takataka mabarabarani baada ya kubambwa laivu akikojoa katika sehemu ya maegesho ya magari kule jijini Los Angeles. Mtanzania huyu alishangaa zaidi kwamba tabia yake hii ya kukojoa hovyo kidogo imletee matatizo alipokwenda kwenye usaili kwa ajili ya kupatiwa "Green Card". Aliulizwa kama alikuwa amewahi kukojoa tena hadharani. Baada ya miaka saba - bado rekodi zilikuweko kwamba alikuwa amewahi kukojoa hadharani (public urination, indecent exposure)!

Ati, ni kwa nini tunapenda kukojoa mabarabarani na vichochoroni? Ni ukosefu wa vyoo vya umma na miundombinu wezeshi (kama mitaro mizuri, madampo, magari ya kuzoa taka n.k) au ni tabia yetu ya kupenda "uchafu"? Ni kweli kwamba sisi tunapenda "uchafu"?

Huyu mwanafunzi mzungu aliniambia kwamba vikojozi wote wa umma aliowaona walikuwa wanaume na kamwe hakuwahi kuona mwanamke akikojoa barabarani. Nilimpa maoni yangu kuhusu suala hili na kumtaka asifikie majumuisho (generalizations) ya haraka haraka kama mababu zake walivyofanya walipotia guu Afrika kwa mara ya kwanza wakiwa na Biblia zao mikononi huku wakidai kwamba walikuwa wamekuja "kutustaarabisha"

Hawa jamaa hapo juu wamenifurahisha jinsi walivyoamua "kukilinda" kijiwe chao na hili tangazo. Wasiwasi wangu ni kwamba sidhani kama hili tangazo litasaidia cho chote!

Friday, September 25, 2009

PESA ZAKO ZINANUKA - NA BEN R. MTOBWA

Pesa Zako Zinanuka ni Riwaya nzuri sana iliyoandikwa na Marehemu Ben R. Mtobwa na kuchapishwa na Heko Publishers mwaka 1984. Niliisoma nikiwa Mlimani lakini nilipoziona picha za hawa "waheshimiwa" nikaikumbuka riwaya hiyo. Itabidi niitafute niisome upya. Mwisho wa "waheshimiwa" hawa sijui utakuwaje. Ngoja tusubiri tuone lakini ni wazi kwamba mabilioni yao yananuka. What a legacy!