NG'WANAKANUNDO - MANJU MASHUHURI WA KISUKUMA KUTOKA MWANZA

Wednesday, February 1, 2012

MGOMO WA MADAKTARI: HIVI KWELI TUKO SIRIAZI NA INCHI HII ???

  • Kuna kipindi walimu walitishia kuitisha mgomo wa nchi nzima. Waziri wa elimu wa wakati ule alitoa kauli ya dharau sana akisema kuwa kama kweli walimu wale walikuwa wanataka kugoma, basi kulikuwa hakujaharibika neno kwani angeweza kuokota watu mabarabarani wakaingia madarasani kufundisha bila wasiwasi wo wote
  • Ningali naikumbuka kauli hii kwani, mbali na kuonyesha kiburi na kutojali kwa serikali ya wakati ule, inaonyesha jinsi taaluma ya ualimu na sekta ya elimu kwa ujumla inavyodharauliwa. Walimu wanaweza kuokotwa tu mabarabarani !!! Na wakati huo huo eti hii ndiyo sekta-mama katika maendeleo ya nchi yo yote ile hapa duniani kwani hakuna nchi ambayo imeshawahi kuendelea bila kuimarisha sekta yake ya elimu.
  • Kati ya taaluma zinazoheshimika hapa nchini na duniani kote pengine ni hii ya udaktari. Taaluma hii ni nyeti kwa maana kwamba inahusu uokoaji wa maisha ya watu moja kwa moja na kuwa daktari inakubidi usome kwa miaka mingi (kule Marekani si chini ya miaka 6 katika Chuo Kikuu). Taaluma hii haina mwanya wa kufanya makosa na waipatayo hula kiapo cha kuokoa maisha ya wagonjwa wao na si vinginevyo - popote pale na katika hali yo yote ile.
  • Mgomo wa madaktari unaoendelea unasikitisha sana. Serikali haikujua kuwa madaktari  ni muhimu kuliko walimu na kwamba hawawezi kuokotwa mabarabani? Serikali haikujua kwamba kama madaktari wangegoma basi maisha ya watu wake na hasa masikini yangepotea? Kama serikali ililijua hili, kwa nini haikuchukua hatua kuhakikisha kuwa mgomo huu hautokei. Si tunaambiwa kwamba kinga ni bora kuliko tiba? 
  • Taarifa zinazosema kwamba mpaka sasa wagonjwa wapatao 201 wameshapoteza maisha yao kutokana na mgomo huu zinasikitisha sana. Bila shaka hawa ni wagonjwa masikini ambao hawana uwezo wa kwenda katika hospitali za binafsi ambazo ni ghali sana kwa wananchi wa kawaida. Wangekuwa na uwezo bila shaka wangekuwa wameshakimbilia huko au India kabisa!
  • Ati, ni nani anayepaswa kulaumiwa kutokana vifo hivi? Ni madaktariserikali au wote wawili? Au pengine kwa vile ni vifo vya watu masikini basi haina neno? Kwa wenzetu mkasa kama huu unatosha kuwafanya wahusika wote kujiuzulu, kuchukuliwa hatua za kisheria na kulipa fidia za mamilioni ya dola. Lakini kwetu sisi, ni siasa, utoto na kutojali tu kama kawaida.  Ndiyo maana nikauliza kama kweli tuko siriazi na nchi yetu hii nzuri iliyojaliwa kwa kila kitu na Muumba. 
Katuni kutoka kwa Said Michael
  • Itakuwaje kama siku moja hawa masikini tunaowaacha wakifa kiholela hivi kama wanyama katika makorido ya hospitali zisizo na madaktari wakiamka na kusema sasa yatosha? Jibu bila shaka linapatikana katika historia. Mungu Ibariki Tanzania !!!
Kwa habari mbalimbali kuhusu mgomo huu soma HAPA au HAPA

HIZI POSHO ZA WABUNGE MBONA KASHESHE ???

Katuni kwa hisani ya Said Michael.
*****************

(1) Spika anasema hata hizo walizoongezewa Bado Hazitoshi 

(2) Naibu Spika alishawahi sema kuwa watajadili jinsi ya kuzifuta.

(3) J.K. Aligoma kuzibariki posho hizi. 

(4) Jana ikaripotiwa kuwa J.K. Amezibariki Posho Hizo

(5). Ikulu mara moja imekana kwamba J.K hajabariki posho

(6). Waziri wa fedha naye hajui kitu kuhusu hizi posho.

(7) CCM nao wakaonyesha wasiwasi wao kuhusu hizi posho.



(6). Hii mbona kasheshe? Ni nani aliyeidhinisha kupandishwa kwa posho hizi? Nini kinaendelea katika sakata hili? Ni sarakasi, mazingaombwe ama siasa ???

Monday, January 30, 2012

ANA MIAKA 85. AMEBADILI KATIBA ILI AWEZE KUGOMBEA KIPINDI CHA TATU. SASA WATU WAKE WANAANDAMANA

  • Kwa upande mmoja kuna Mwalimu Nyerere na rafiki yake Madiba. Marafiki hawa daima watabakia kuwa nyota zinazong'ara barani Afrika. Pamoja na kuandika historia kwa kuwa mababa wa taifa, kuonyesha uadilifu wa kiwango cha juu wakati wakiwa madarakani na kuweka dira za kihistoria na kisiasa katika nchi zao, viongozi hawa waliamua kuachia madaraka pamoja na ukweli kwamba wangeweza kuendelea kubakia madarakani kama wangetaka. Ati, ni nani angeweza kumpinga Nyerere (na akafanikiwa) kama angeamua kubakia madarakani?
  • Kwa upande mwingine wapo akina Mubarak wa Misri na kundi lake - viongozi ambao hawakutaka na bado hawataki kuachia madaraka. Viongozi wa kundi hili, hata wazeeke vipi na fikra zao kuchakaa namna gani, bado watafanya kila wawezalo ikiwemo kubadilisha katiba na hata kuiba kura ili tu waweze kubakia madarakani. Ikibidi ni lazima wafie madarakani au wang'olewe kwa nguvu na hata kuuawa. Kuna msururu mrefu wa viongozi wa aina hii barani Afrika! 
  • Abdoulaye Wade - rais mkongwe (miaka 85) wa Senegal naye ameingia katika kundi hili. Yeye amebadilisha katiba ili aweze kugombea kipindi cha tatu. Pia amefanikiwa kumfanyia mizengwe mgombea wa upinzani, mwanamuziki mashuhuri Youssou N'Dour  ili asiruhusiwe kugombea. Jambo la kufurahisha ni kwamba umma wa Senegal umeonyesha kukerwa na jambo hili na tayari maandamano yanafanyika kujaribu kumpinga huyu babu kuendelea kubakia madarakani. Itafurahisha sana kama matakwa ya umma yatashinda kama ilivyokuwa kule Misri, Tunisia na Libya.
  • Pengine jambo la muhimu tunalopaswa kujiuliza hapa ni hili: Kwa nini viongozi wa Afrika wana uchu wa madaraka namna hii kiasi cha kupuuza matakwa ya watu wao na kufikia hata kubadilisha katiba za nchi zao ili tu waendelee kubakia madarakani? Utakuta kiongozi amekaa madarakani miaka nenda miaka rudi na hakuna la maana alilofanya mbali na ufisadi na kusikinisha watu wake lakini bado tu anataka aendelee kubakia madarakani. Kwa nini? Na umma wa Afrika, kama vile kondoo wapelekwao machinjioni, umeonyesha uvumilivu wa kupita kiasi kwa viongozi hawa wa milele. Ni mpaka hivi karibuni tu umeanza kuamka na kusema sasa yatosha. 
  • Tabia hii ya viongozi wapenda madaraka kung'ang'ania madarakani barani Afrika inabidi ikomeshwe; na natumaini kwamba umma wa Senegal utashinda
Mungu Ibariki Afrika !!! 

Sunday, January 29, 2012

MCHEZA SINEMA AJIUA ILI KUOMBOLEZA NA KUPINGA KUUAWA KWA MBWA WAKE

  • Mcheza sinema huyo kwenye picha anaitwa Nick Santino (47). Jana (28/1/2012) aliamua kubugia makumi ya vidonge na kuacha ujumbe akilalamika kuhusu kuuawa kwa mbwa wake aitwaye Rocco. Rocco ilibidi auawe baada ya wamiliki wa jumba alimokuwa akipanga kule jijini New York kupinga wapangaji wake kuwa na majibwa makubwa (pitbulls) kama Rocco. Baadhi ya wapangaji wenzake pia walilalamika kwamba Rocco alikuwa akibweka sana. 
  • Kwa wenzetu hawa mbwa ni sehemu ya familia na hivyo hutunzwa na kugharamiwa kama vile memba wengine wa familia. Mbwa wengine huwa na bima ya afya, hupelekwa kwa daktari kufanyiwa uchunguzi wa afya zao kila mwaka na kupatiwa chanjo mara kwa mara na wakati mwingine huweza hata kuachiwa urithi. Na mbwa anapofariki, familia nzima huwa na huzuni kwa kuondokewa na memba wa familia.
  • Jirani yangu hapa alifiwa na mbwa wake aliyekuwa amekaa naye kwa miaka 13. Watoto wake walihuzunika sana kiasi kwamba ilibidi wapatiwe ushauri nasaha. Nasi ilibidi kuwatumia kadi za kuwapa pole na kuwatia moyo! 
  • Kwa sisi Waafrika kisa kama hiki cha mtu kujiua eti kwa sababu ya mbwa wake kufariki linaweza kuonekana kuwa jambo la kuchekesha. Katika makabila mengi mbwa walifugwa hasa kwa lengo la kusaidia katika uwindaji na ulinzi wa nyumba au mifugo. Nakumbuka siku nilipowaambia wanafunzi wangu Wamarekani kwamba kijijini nitokako mbwa hapaswi kulala ndani ya nyumba bali nje ili kuhakikisha kuwa mifugo na familia iko salama. Wanafunzi hao walishangaa na wengine waliona kuwa ilikuwa ni ukatili kuwalaza mbwa nje ya nyumba. 
  • Inabidi tujibidishe kujifunza na kuziheshimu tofauti hizi za kitamaduni hasa katika wakati huu ambapo dunia inazidi kufungamana zaidi. Ni dalili ya ujinga kucheka na kudharau tamaduni zingine hata kama zinaonekana kuwa ngeni, za "kishenzi" na kushangaza namna gani. Baadhi ya tofauti za kitamaduni kati ya Waafrika na wazungu zimeeelezwa vizuri katika kitabu mashuhuri cha Profesa Mbele kiitwacho Africans and Americans: Embracing Cultural Differences

 Kisa hiki cha kusikitisha kinapatikana HAPA

Tuesday, January 24, 2012

"MACHO YAKO MBONA HAYATULII MUME WANGU? WEWE LAZIMA UTAKUWA NA MWANAMKE WA NJE" !!!


Katika tamaduni nyingi za makabila ya Kitanzania, kukaziana macho wakati wa mazungumzo ni jambo geni. Mara nyingi watoto hawaruhusiwi kuwatazama watu wazima usoni wakati wa mazungumzo. Kufanya hivyo ni ukosefu wa adabu. Hali kadhalika katika makabila mengi wanawake pia hawakupaswa kuwaangalia wanaume usoni wakati wa mazungumzo. Kufanya hivyo ilikuwa dalili ya uchakaramu. 

Nakumbuka nilipofika hapa Marekani kuanza masomo swala hili lilinipa shida sana kwani nilikuwa siwezi kuongea na maprofesa, wanafunzi wenzangu na watu wengine huku nikiwa nimewakazia macho usoni. Nilizidi kuchanganyikiwa zaidi pale wasichana wa Kimarekani walipokuwa wakiongea nami huku wamenikazia macho usoni. 

"Wasichana gani hawa wasio na aibu?" Nilikuwa nikijiuliza mara kwa mara.


Sikujua kuwa hili lilikuwa ni tatizo mpaka siku moja mshauri wangu aliponiita ofisini kwake na kuniambia kwamba watu walikuwa wakilalamika kwamba nilikuwa siwaangalii machoni wakati wa mazungumzo. Aliniambia kwamba kwa Wamarekani kuongea na mtu bila kumwangalia usoni ni jambo baya sana. Linaonyesha kwamba pengine unachokisema si cha kweli na kwamba wewe siyo mtu wa kuaminika. 

Japo nilijibidisha sana kufanya mabadiliko na kuanza kuwakazia watu macho usoni wakati wa mazungumzo, ni lazima nikiri hapa kwamba hili halikuwa jambo rahisi. Na kusema kweli mpaka leo sijalizoea jambo hili na daima huwa sijisikii huru kufanya hivyo.

Ndiyo maana hii katuni kidogo imenishangaza. Pengine ni matokeo ya utandawazi na minyororo yake ya kitamaduni. Ni tangu lini mke na mume wa Kiswahili wakakaziana macho wakati wa mazungumzo? Pengine wanandoa wasomi wa mijini lakini siyo kule vijijini. Na simlaumu huyo baba kwenye katuni kwa kushindwa kwake kuhakikisha kwamba kunakuwa na "eye contact" kati yake na mkewe. Huu si utamaduni wetu na kwa sisi wazee hili ni jambo ambalo inabidi tujifunze kama kuna ulazima wa kufanya hivyo.

Kwa tofauti na mifano mbalimbali ya migongano ya kitamaduni kati ya Waafrika na Wazungu (hasa Wamarekani) jaribu sana kusoma kitabu mashuhuri cha Profesa Mbele kiitwacho Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Monday, January 23, 2012

UTAFITI: WAKAZI WA NCHI ZA BARIDI WANA MACHO NA UBONGO MKUBWA KULIKO WAKAZI WA NCHI ZA JOTO

 
Matokeo ya utafiti yaliyochapishwa mwaka jana yanaonyesha kwamba watu wanaoishi katika ukanda wa nchi za baridi juu ya mstari wa Ikweta wana macho na ubongo mkubwa zaidi kuliko wenzao wanaoishi karibu na mstari huo.

Kwa vile nchi nyingi za baridi mbali na mstari wa Ikweta zipo Ulaya, Urusi, Asia na Amerika ya Kaskazini, hii inamaanisha kwamba wakazi wa nchi hizi wana macho na ubongo mkubwa.

Na kwa vile sote tunajua kwamba ubongo mkubwa unahusianishwa moja kwa moja na akili nyingi, swali la muhimu linalozushwa na utafiti huu ni hili: Wakazi wa nchi za baridi (wengi wao ni weupe) wana akili kuliko wakazi wa sehemu zilizo karibu na Ikweta (weusi)? 

Japo watafiti wamekwepa kufanya jumuisho hili, inavyoonekana wamefanya hivyo ili kukwepa mitafaruku tu. Je, ugunduzi huu mpya unaweza kueleza tofauti za kimaendeleo na kisayansi kati ya watu wa “kaskazini” na “kusini”?

Mgunduzi mwenza wa “DNA” mwenyewe alipata matatizo makubwa alipotoa dai kama hili mwaka 2007, dai ambalo lilimfanya afukuzwe au kujiuzulu nyadhifa zake zote za kisayansi na kiuongozi alizokuwa akizishikilia

Kwa maoni ya kutatanisha kuhusu mkondo huu wa mawazo tazama maoni ya binti machachari wa Kichaga aitwaye Aika HAPA. Maoni haya yaliwasha moto mkubwa sana huku wengine wakimshambulia na wengine wakimuunga mkono.

Wewe una maoni gani? Ni kweli watu weusi tuna akili “pungufu” tukilinganishwa na weupe?

Sunday, January 22, 2012

KUTENDA KOSA SI KOSA, KOSA NI ........!!!

  • Makosa mapya yanaonyesha kwamba unakua, unabadilika na unasonga mbele kifkra na kimaendeleo. Makosa mapya yanaonyesha kwamba unajaribu vitu vipya na katika kujaribu huko ndimo hatimaye mna mafanikio. Na kusema kweli makosa mapya ni ya lazima katika maisha yetu.
  • Na kama unajifunza kutokana na makosa hayo na kuepuka kuyarudia tena na tena basi hili ni jambo jema. Tangu hapo kutenda kosa siyo kosa isipokuwa kurudia kosa ati ! 

HATIMAYE IMEKUWA: DR. SLAA AKUTANA NA DR. J.K. ANA KWA ANA !!!

Dr. Slaa akisalimiana na Dr. Kikwete ikulu jana. Ni picha ya 
Kihistoria ama?
  • Makala ya Bwn. Ally Ulanga yaliyochapishwa kule Wanabidii nami nikayaweka HAPA yaliwasha moto mkali. Katika makala hayo, Bw. Ulanga alimlalamikia sana Dr. Slaa kutokana na kitendo chake cha "kukwepa" kukutana na Dr. Kikwete katika mazishi ya mbunge wa Chadema, Regia Mtema. Bwana Ulanga aliendelea kubainisha kwamba Dr. Slaa alikuwa hajawahi kukutana na Rais Dr. Kikwete ana kwa ana tangu alipogaragazwa katika uchaguzi mkuu uliopita. 
  • Habari hizi pia ziliripotiwa na gazeti la Mwananchi. Habari za kidaku zikaendelea kusema kwamba Dr. Slaa alimkwepa Dr. Kikwete eti kwa sababu alikatazwa na mkewe kusalimiana na rais. 
  • Nimefurahishwa na taarifa hizi kwamba Dr. Slaa hatimaye ametinga ikulu jana na kusalimiana ana kwa ana na rais Dr. Kikwete. Naamini kwamba jambo lililompeleka ikulu ni kubwa na la muhimu kwa maslahi ya taifa letu. Kwa hili Dr.Slaa na Dr. Kikwete wanastahili pongezi kwa kutuonyesha Watanzania kwamba pamoja na tofauti zao kali za kisiasa bado wanaweza kukaa pamoja na kujadili masuala muhimu yanayohusu taifa letu. 
  • Ni lazima tuendeleze ule utamaduni wa kutatua matatizo na tofauti zetu kwa njia ya mazungumzo. Na kwa hili Dr. Slaa na Dr. Kikwete wameonyesha ukomavu mkubwa wa kisiasa !
Picha zote ni kutoka Jamii Forums

Soma maoni ya Mwanaharakati Mwl. Lwaitama kuhusu suala hili HAPA

Wednesday, January 18, 2012

HEBU ITAZAME VIZURI HII MELI ILIYOLALA. IFIKIRIE KAMA NI NCHI.....

  • Meli kubwa hili la kifahari kwa jina Costa Concordia limelala chali ufukoni mwa bahari ya Tucsan kule Italy. Mpaka sasa watu 11 wameshathibitishwa kuwa wamefariki. Wengine 29 hawajulikani waliko. Lita za mafuta zipatazo 500,000 huenda zikamiminika baharini katika sehemu ambayo imetengwa kuwa mazalia salama ya nyangumi na pomboo (dolphins). Kwa nini ajali hii imetokea?
  • Inavyosemekana ni uzembe wa nahodha. Yeye aliacha kufuata ramani za njia aliyopangiwa na badala yake akaisogeza meli karibu na pwani zaidi ili kujionyesha. Kwa kufanya hivyo meli ikagota kwenye mwamba. Ajali ikatokea. Na kibaya zaidi, nahodha mwenyewe akatimua mbio na kulitelekeza jukumu lake la kuhakikisha kwamba kila abiria ameokolewa. 
  • Ni manahodha wangapi waliwahi kuangusha meli za nchi zao kama huyu nahodha mchovu wa Costa Concordia? Wafikirie akina Mobutu, akina Bokassa, akina Idd Amin, akina Banda, akina ......Afrika ina msururu mrefu wa manahodha wazembe waangusha meli. Tanzania je? Tuna bahati ama? 
  • Pengine maswali ya kujiuliza ni haya: Abiria wanastahili lawama katika uzembe huu wa manahodha wao? Kwa nini mtu mmoja awe na madaraka makubwa ya kusogeza meli karibu na miamba na hakuna mtu wa kumkataza? Wakati unaposoma makala haya mafupi unajua meli ya bara lako na nchi yako inaelekea wapi? Usije ukashangaa sana kama meli hiyo itakuwa inaelekea ufukoni kunako miamba ya hatari. Kama abiria mwema, jukumu lako ni nini?

Tuesday, January 17, 2012

HONGERA CHUO KIKUU CHA DAR ES SALAAM KWA KUWA MOJA YA VYUO VIKUU BORA BARANI AFRIKA !!!

  • Pamoja na changamoto zote zinazokikabili, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kimetamba barani Afrika kwa kushika nafasi ya 36 kwa ubora katika ripoti iliyoandaliwa na shirika lisilo la kiserikali la URAP. Kiulimwengu kimeshika nafasi ya 1593.
  • Vyuo vikuu vingine vya Tanzania vilivyotajwa katika ripoti hiyo ni Muhimbili (42 barani Afrika, 1,716 kiulimwengu) na Sokoinne (45 barani Afrika, 1,771 kiulimwengu). Chuo Kikuu cha Capetown nchini Afrika Kusini ndicho kimeshika nafasi ya kwanza barani Afrika na kama kawaida Chuo Kikuu cha Harvard nchini Marekani kimeshika nafasi ya kwanza kiulimwengu. 
  • Vigezo vilivyotumika pamoja na na habari za ziada kuhusu ripoti hii vinapatikana HAPA. Habari hii pia iliripotiwa katika gazeti la Daily News la tarehe 8/1/2012 HAPA

Monday, January 16, 2012

DR. WILBROAD SLAA, KWA HILI UMECHEMSHA


Na Ulanga Ally
Wanabidii (16/1/2012)

Natanguliza pole kwa familia na wanamageuzi kwa msiba wa mpiganaji mwenzetu Bi. Regia Mtema. Hakika msiba huu nipigo kubwa kwa Taifa. Tunamuomba Mwenyezi Mungu amuweke mahali pema peponi,amina. 

Dr. Slaa ukiwa kiongozi mwenye sura ya kitaifa, utambue kuwa maisha  yako yote yanakuwa mikononi mwa jamii (watanzania).Hii na maana ya kwamba kwa lolote utakalo shughulika nalo lazima litaifikia jamii na kupata fursa ya kulitafakari. Tunatambua kuwa kila mtu anatabia zake binafsi aidha kutokana na malezi, mafundisho ama kuzaliwa. Ni dhahiri pamoja na yote kuna tabia zisizokubalika (mbaya) na zinazokubalika (nzuri) katika jamii. 


Tunatambua uligombea nafasi kubwa ya uongozi wa juu wa Taifa letu (U- Rais) na kwa bahati nzuri ama mbaya ulishindwa na Rais akapatikana naye ni Ndugu Jakaya Mrisho Kikwete. 

Tutambue kuwa kulingana na sheria zetu pamoja na Katiba tuliyo nayo huyu ndiye kiongozi wetu Watanzania na ndio maana kila mtu akimtaja anaanza na "Rais". Katika ushindani kuna kushinda na kushindwa na inapokuwa shida kupinga ushindi wa mtu ki-ushahidi na kimazingira ni busara kukubali kushindwa. 


Hivi vitu kwako vimekuwa ni vigumu kuvikubali na katika hali ya kawaida umeonekana ni mtu mwenye chuki kubwa tena ya wazi kwa Rais wa nchi. Binafsi mwenendo wa tabia yako siupendi kwani umejaaa unafiki,wivu,chuki na majungu ambapo haipaswi kwa kiongozi wa Kitaifa kama wewe na zaidi mtu wa imani (Padri Mstaafu) kuwa nayo. 


Tunatambua kuwa Kikwete kama Rais na kama binafsi ana mapungufu yake lakini hawezi kuwa mbaya kwa yote. Sidhani kwamba imefikia hatua tunajali ya KIJINGA na kuacha MEMA.Kitendo chako cha kumuona Rais wa Nchi kama adui yako namba moja kiasi cha kutosalimiana (nitafafanua chini) hata katika shughuli za kijamii ni aibu kwa taifa, kwako  binafsi, kwa kiongozi wako Mbowe na Chama kwa ujumla. Sikuwa na waza juu ya muendelezo wa tabia yako lakini sasa nimebaini kuwa wewe si muungwana na haufai kuwa kiongozi wa Taifa hili kama hutobadilika. Mifano:- 


1) Ulipinga matokeo ya uchaguzi kupitia vyombo vya habari kwamba si halali na hii ni kwa sababu hukushinda. (Watanzania tulikusikia na kukuona). 

2) Ulikataa kuhudhuria katika mwaliko wa kumtangaza Kiongozi aliyeshinda U-Rais huku na wewe ukiwa mgombea. (Watanzania tulikusikia). 

3) Mchakato wa Katiba hukushiriki kwenda kumuona Rais Ikulu huku ukiwa kiongozi na mratibu Mkuu wa Chama kwa nafasi yako ya Ukatibu Mkuu. (Watanzania tunajua). 

4) Umekataa kuhudhuria Sherehe zote za Kitaifa hasa pindi chama kinapoalikwa na kukuteua wewe kuhudhuria. 

5) Kumkwepa Rais wa Nchi katika Msiba wa kipenzi chetu Bi. Regia Mtema (Hili limenisikitisha kuliko yote) huku ukiwa na taarifa ya ujio wake na baadae kuwasili baada ya kusikia Rais ameondoka. (tunajua waweza sema kuwa ulikuwa na majukumu mengine). 


Picha, Maelezo na Maoni HAPA na HAPA

Hizi tabia zako hazipaswi kuvumilika hata kidogo na ni zaidi ya unyama. Wewe kama Kiongozi unayejiamini ni kwa nini ujifiche ama umkimbie mtu unayemuona kama adui yako? (unapaswa ukabiliane nae) tabia hii inaonyesha mengi huwa unaidanganya jamii juu yake sasa ni AIBU kuonana nae uso kwa uso. Tambua maisha yako na ya viongozi wengine wa vyama vya kisiasa ndani ya Nchi hii yako mikononi mwa Watanzania na si kwao binafsi. Hivi kama ni kuku -assassinate unafikiri TISS wanashindwa? Ukweli ni kwamba wanaweza lakini watawaambia nini Watanzania juu ya kifo chako. Hii nimeisema kama unahisi kuonana na Kikwete ata katika MSIBA maisha yako yatakuwa hatarini. 


Tunajua by implication wewe ni mfuasi wa vegeance policy hasa utakapo pata madaraka (U-rais) , lakini sidhani kusalimia na mtu kutakupunguza hasira na malengo yako ya kutochukua maamuzi unayoyapenda. 

Regia Mtema (Marehemu) -Ametukutanisha hapa msibani kwa sababu ya uungwana wake kwa watu wote pasipo kujali itikadi ya vyama ama dini. Huyu alikuwa binti mdogo sana lakini kwa miaka 32 (umri wake) ameweza kufanya makubwa na kusababisha sote kumpenda. Regia angekuwa mbaguzi, mwenye chuki, asiyekubali kubadilika leo hii pamoja na msiba wake , lakini maneno mengi ya chini chini yangekuwa yakipita juu ya ubaya wake. 

Dr. Slaa tunakuthamini kwa mchango wako wa mageuzi ya kisiasa, changamoto pamoja na umri wako (miaka 64 tarehe 29/10/2012 utatimiza). Hivi kweli kujitenga kwako ama kwa tabia hizi unatufundisha nini sisi vijana tunaokuwa na tegemeo la Taifa? 

Nampongeza sana Mwenyekiti wa Chama Mhe. Freeman Aikaeli Mbowe hakika ni tofauti kabisa na wewe. Yote ambayo umekwepa kuyatekeleza ata amabayo yamekuwa yakikuhusu , yeye ameweza kuyatekeleza napengine si kwa nafasi yake bali kwa kujali utu na kutambua kuwa SIASA SI VITA (pale demokrasia inapochukua mkondo wake). Chama Cha Demokrasia na Maendeleo kimepata kiongozi bora na mtu wa watu. Mhe. Freeman Mbowe hakika:-

1) Ni mpenda watu 
2) Hana Makuu, majungu wala fitina 
3) Ni binadamu wa kweli anayeishi kulingana na mwenendo wa maisha ulivyo. 
4) Kiongozi bora wa Kisiasa na Kijamii 
5) Hana visasi na mwenye kutambua utu wa mtu 
6) Muungwana na si mgumu wa kusamehe 
7) Mwenye msimamo thabiti wenye kujali haki za wananchi na Wajibu wa Watawala 
8) Mtu wa kujichanganya na wengine pasipo kujali cheo chake, madaraka yake na pesa zake. “Ewe Mwenyezi Mungu tunakuomba umzidishie Umri pamoja na Busara Kiongozi huyu.” 

WITO


Dr. Slaa tunajua ni jinsi gani ilivyo ngumu kubadili tabia yako hasa katika utu uzima ulio nao,lakini hakuna kinachoshindikana mbele ya Mungu. Rudi nyuma utubu na Mwenyezi Mungu atakupa busara ya kutuongoza  vinginevyo "Your leadership can be another disaster to our Nation". 

JIANDIKISHE HAPA

Enter your email address:

Delivered by FeedBurner

BLOGU ZA BURUDANI NA UREMBO