NG'WANAKANUNDO - MANJU MASHUHURI WA KISUKUMA KUTOKA MWANZA

Tuesday, May 26, 2009

MASHINDANO YA UREMBO KILA KONA - UTANDAWAZI HUU UNATUPELEKA WAPI?

Wanablogu wenzangu, nilikuwa nimebanwa na pilikapilika za kubeba maboksi kwa wiki moja na ushee hivi. Sasa nimesharudi na kama kawaida tuendelezeni mapambano ya kuipigania jamii.
==================================================================
Inavyoonekana sasa kila kona ni mashindano ya urembo. Juzijuzi hapa nilisoma katika magazeti kwamba kulikuwa na mashindano ya kumtafuta Miss Maswa - wilaya moja katika Mkoa wangu wa Shinyanga. Halafu tena nikasoma kuhusu mashindano ya kumtafuta Miss. Malampaka - kakitongoji kamoja kule kule Shinyanga. Na karibu kila siku ukisoma gazeti ni lazima utakutana na aina fulani ya mashindano ya urembo mpaka haya mashindano Miss Landmine kutoka Angola.

Kwangu mimi naona kuna ruwaza (pattern) fulani hapa. Kwa kawaida sisi tunayo tabia ya kuiga vitu hata kuwazidi hao tunaojaribu kuwaiga, na hili si jambo la kufurahisha. Na katika haya mashindano ya urembo nadhani tunafanya vivyo hivyo - tena kwa kutumia vigezo vile vile vya hao mabwana wetu wenye utamaduni wenye hadhi. Tukiendelea hivi nadhani mwishowe tutakuwa na Miss Tarafa, Miss Kata, Miss Kijiji na hata Miss familia. Sijui tunaelekea wapi. Wakati mwingine hata nawasikitikia hawa dada zetu wanaojikondesha ili waweze kushiriki haya mashindano ya "urembo".

Mambo yamebadilika kwa kasi sana kwani juzijuzi tu hapa wembamba kwa Mwafrika ulikuwa ni dalili ya matatizo ya kiafya na watu walipendelea mwenzi aliyetakata. Na kutokana na mazingira ya kufanya kazi sana, wenzi hawa waliotakata hata hawakuwa na matatizo ya kiafya mengi kama saratani, kiharusi na shinikizo la damu - magonjwa ambayo sasa yanaenea kwa kasi bila kujali kama mtu amejikondesha ama la. Kwa ujumla utandawazi unavuruga kila nyanja ya maisha yetu. Sijui tunaelekea wapi.


Thursday, May 14, 2009

HAPA KIPANYA ANATUAMBIA NINI???

Ni uthibitisho wa ile dhana kwamba Watanzania hatupendi kusoma vitabu? Au ni ile imani iliyoenea kwamba eti wazungu ni wadadisi na wasiochoka kusaka maarifa mapya - katika mazingira yo yote yale na kwa gharama yo yote ile? Kama ni kweli kwamba Watanzania hatupendi kujisomea, tumeshawahi kujiuliza ni kwa nini? Inawezekana kwamba pengine kusoma vitabu si njia pekee ya kujipatia maarifa. Au pengine vitabu vingi vina "maarifa" ambayo hayaendani na mazingira yetu na watu hawaoni sababu ya kupoteza pesa zao na muda wao kununua na kusoma vitu ambavyo havitawasaidia?

Vitabu tuliletewa na wakoloni na ni wazi kwamba tulikuwa na njia zetu za kurithishana na kupeana maarifa hata bila uwepo wa vitabu. Tunajua pia kwamba elimu yetu ya wakati ule kabla hatujaingiliwa na wakoloni ilikuwa ni elimu ya moja moja ambayo ilitufunza kutenda na kupambana na mazingira yetu ana kwa ana - siyo hii ya sasa ya kukariri vitabu wakati mwingine hata bila kujua unachokisoma na kukikariri kina maana au faida gani katika mazingira yako halisi. Nimechoka kusikia kila mara kwamba eti Watanzania hawapendi kujisomea. Wakati umefika sasa wa kujiuliza ni kwa nini hawataki kusoma vitabu na kama kweli ni lazima wasome vitabu ndiyo wapate maarifa, nini kifanyike!

Friday, May 8, 2009

KIDOGO NIPIGWE FAINI (TIKETI) YA DOLA 350!!!

Basi la wanafunzi lilikuwa limesimama likipakia wanafunzi - na ile alama ya STOP ikiwa imeinuliwa. Lilikuwa ni eneo karibu na shule na tayari nilikuwa naendesha maili 20/saa. Nilipoliona hilo gari nilisimama mara moja ingawa jamaa aliyekuwa nyuma yangu alianza kunipigia honi. Kumbe kwenye kona tu mbele yetu kulikuwa na polisi mwenye pikipiki amejibanza. Basi alikuja na kuanza kuniambia kwamba japo nilikuwa nimesimama, nilikuwa nimesimama karibu sana na hilo basi. Jamaa akaanza kupima umbali kati ya basi na gari langu, akakuta nilikuwa nimezidi kama futi moja hivi. Basi akanipa onyo kwamba mara nyingine nisimame mbali zaidi vinginevyo dola 350 zitanitoka. Aliponiuliza ni nani alikuwa anapiga honi nilimwambia ni huyo jamaa wa nyuma yangu. Basi alimwendea huyo jamaa na sijui kama alimpa tiketi au la.

Tukio hili linaonyesha vizuri kabisa jinsi wenzetu walivyojiwekea utaratibu mzuri wa usafiri kwa wanafunzi wao. Katika maeneo ya shule spidi ni maili 20/saa na kama basi la wanafunzi linapakia au kushusha wanafunzi, magari yote ni lazima yasimame. Halafu nikakumbuka mshikemshike wanaokumbana nao wanafunzi wetu kule nyumbani kama hizi picha zinavyoonyesha. Ni kweli hatuwezi kuwa na utaratibu mzuri wa kuhakikisha kwamba wanafunzi hawa wanapata usafiri unaoaminika (na salama) wa kwenda shuleni na kurudi majumbani mwao? Au tunasubiri mpaka wafadhili waje watusaidie?

Wednesday, May 6, 2009

KANISANI WAMENIUDHI

Wiki jana nilipeleka mtoto kanisani kwa ajili ya darasa lake la katikati ya wiki. Tulipoingia kanisani darasa lilikuwa bado halijaanza ingawa kulikuwa na watoto wengi pamoja na wazazi wao. Pengine kwa ajili ya kusubiri mwalimu afike, kulikuwa na slide show ya picha kutoka sehemu mbalimbali duniani - bustani nzuri na kangaroo kutoka Australia, mito na majumba marefu kutoka Japan, barafu na milima ya theluji kutoka Uswisi n.k. Ilipofika "zamu" ya Afrika zikaja picha za wagonjwa wa UKIMWI tena ambao wako nyang'anyang'a kabisa kiasi kwamba watoto walishtuka na wengine kufunika nyuso zao na kuanza kulia. Mhudumu mmoja wa kanisa aliyekuweko karibu na mitambo alizima ile slide show mara moja. Nimeandika barua ya kulalamika kuhusu jambo hili kwa uongozi wa kanisa. Kama mada ilikuwa ni uzuri wa mazingira kama walivyofanya katika mabara mengine - mbona wasionyeshe Mlima Kilimanjaro, Serengeti n.k. ilipofika zamu ya Afrika? Mbona wasionyeshe wagonjwa kutoka Australia, Japan na Ulaya? Au huko hawaugui na kufa? Inasikitisha sana kuona kwamba maoni ya kipumbavu na kibaguzi kama haya yamo mpaka makanisani - sehemu ambayo mtu ungetegemea kwamba kutakuwa na upendo, usawa na heshima kwa wote!

Tuesday, May 5, 2009

TUZO ZA HESHIMA KWA WANAFUNZI BORA

Habari hii nimeipata kwa Michuzi Mdogo na iliwahi kuongelewa katika blogu mbalimbali. Ni wazo zuri sana hili kwani litasaidia katika kuhamasisha vijana wetu wasome kwa bidii. Ni wazo ambalo wizara ya elimu inapaswa kuliunga mkono.


Wanafunzi Bora Tz nao Kuneemeka na Tuzo za Heshima

Tuesday, April 28, 2009
Profesa,Wakali Kwanza,Tundaman kusindikiza tuzo za Wanafunzi bora TZ.

Hii ni kwa mara ya kwanza kabisa nchini kushuhudia tuzo za elimu zikitolewa kwa wanafunzi waliofanya vizuri kwenye ngazi za shule za msingi pamoja na sekondari na katika utoaji huo wa tuzo wanamuziki mbalimbali ambao ni Profesa Jay,QJ na Makamua,Tundaman,Spark pamoja na kundi zima la Bongo Dar-Es-Salaam wakiwemo kusindikiza utoaji wa tuzo hizo mwezi ujao ndani ya viwanja vya Leaders.

Tumezoea kusikia tuzo zinatolewa kwa wanamuziki bora,waigizaji bora wachezaji bora na tuzo nyingine mbalimbali lakini kwa hapa nchini hatujawahi kusikia tuzo zinatolewa kwa wanafunzi bora nchini lakini kwa mara ya kwanza PTECHS inakuletea tuzo kwa wanafunzi bora nchini ambazo zitakuwa na lengo moja kuu na la muhimu la kutaka kuwapa moyo wanafunzi ili waweze kufanya vizuri na kuinua elimu nchini.

Mmoja wa waandaaji wa tuzo hizo za elimu,Godfrey Maginga alisema kwamba yeye pamoja na wenzake waliweza kukaa chini na kujiuliza maswali kwanini kila siku zinaibuka tuzo mbalimbali na elimu inakuwa inapewa kisogo na ndiyo maana wameamua kuchukua uamuzi wa kuandaa tuzo hizo maalumu kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari Tanzania.

"Kila siku tunasikia tuzo kwa wasanii mbalimbali lakini hata siku moja hatujawahi kusikia tuzo kwa wanafunzi ambao ni kizazi chetu cha kesho hivyo ndiyo maana tuliamua kuandaa tuzo hizi za wanafunzi wanaofanya vizuri nchini"Alisema Godwin Maganga.

Akielezea kuhusu mchakato mzima wa tuzo hizo,msemaji huyo alisema tuzo haziwezi kutolewa bila ya burudani yeyote ile hivyo kusindikiza utoaji wa tuzo hizo wameamua kuwaalika wanamuziki mbalimbali ambao nao watahamasisha wanafunzi kushiriki mashindano ambayo yanawapelekea kupata tuzo hizo pamoja na burudani.

Bongo 5 iliweza kuongea na baadhi ya wanamuziki hao ambao watatoa burudani siku hiyo na walisema kwamba ni moja ya changamoto ambayo itaweza kuamsha juhudi za wanafunzi nchini kufanya vizuri mashuleni.

"Kwakweli ni moja kati ya tuzo ambazo zitawapa mwamko wanafunzi wa kusoma kwa bidii ili waweze kupata tuzo hizo"Makamua.

Naye Profesa Jay,mzee wa mitulinga alisema kwamba tuzo hizo ni moja kati ya tuzo zinazotakiwa kupewa heshima zake nchini kwa kuwa ni moja kati ya tuzo ambazo zinaweza kuibua viongozi wa kesho.

Tuzo hizi zinatarajiwa kutolewa may 23 ndani ya viwanja vya Leaders.

Friday, May 1, 2009

MAJERUHI WA MABOMU YA MBAGALA

Watu hawa waliumizwa na mabomu yaliyokuwa yakiripuka hovyo katika kambi la jeshi kule Mbagala jana na hapa wanawahishwa kwenda hospitali kupata matibabu - wote katika mikokoteni! Magari ya wagonjwa yako wapi? Ingekuwa kijijini nisingeuliza lakini hata jijini Dar es salaam? Hata raia wenye magari, bajaji hakuna isipokuwa tu hii mikokoteni?













Picha ya kwanza kutoka Haki-Ngowi

JIANDIKISHE HAPA

Enter your email address:

Delivered by FeedBurner

BLOGU ZA BURUDANI NA UREMBO