NG'WANAKANUNDO - MANJU MASHUHURI WA KISUKUMA KUTOKA MWANZA

Saturday, February 27, 2010

MATETEMEKO YA ARDHI JAPAN NA CHILE - HALAFU HAITI

  • Jana Japan ilikumbwa na tetemeko kubwa la ardhi lenye ukubwa wa 7.0 katika kipimo cha Richter. Tetemeko hili lilikuwa na ukubwa sawa na lile lililoikumba Haiti na kusababisha vifo vya watu zaidi ya laki mbili na elfu hamsini pamoja na kuharibu kabisa mji mkuu wa nchi hiyo masikini. Kule Japan, tetemeko hili halikusababisha uharibifu mkubwa wa mali na maisha.
  • Leo, Chile imekumbwa na tetemeko kubwa kabisa lenye ukubwa wa 8.8 katika kipimo cha Richter. Wanasayansi wanasema kwamba tetemeko hili lilikuwa na nguvu mara 500 kuliko lile la Haiti. Habari zinazoendelea kupatikana kutoka Chile zinasema kwamba japo kuna uharibifu wa majengo na maisha, uharibifu huo hautafikia wala kukaribia ule wa Haiti.
  • Kinyume na Haiti, Japan na Chile zina uzoefu wa muda mrefu na matetemeko makubwa ya ardhi na teknolojia okozi na zuizi zinatumika katika ujenzi wa miundo mbinu yote.
  • Hii inaonyesha ni kwa jinsi gani umakinifu na maandalizi ya muda mrefu vinavyoweza kuokoa mali na maisha ya watu. Haiti na nchi zingine zinayo mengi ya kujifunza kutoka Chile.

Friday, February 26, 2010

FIKRA YA IJUMAA: ATI, KUNA NINI KATIKA OMBWE LA KUTOKUWAKO?

Hebu tuwaze: Kama kusingekuwa na cho chote, kungekuwa na nini?

**************************
  • Tuweko!

Thursday, February 25, 2010

ATI, HAWA WAKIZEEKA INAKUWAJE???

Ni katika ile patashika ya kumwangalia binadamu - mnyama tata asiyemaliza vituko!


Ati huyu chini ni mwanamke (Asante Mzee wa Changamoto kwa link!)

Wednesday, February 24, 2010

CHANGAMOTO ZA WATU WEUSI HAPA NINAPOISHI (NA POPOTE KWINGINEKO)

Ninaishi katika mji wa Gainesville, kata/tarafa/wilaya? (county) ya Alachua. Kidemografia, asilimia 22 ya wakazi wa Alachua ni weusi. Ripoti inayoainisha masuala ya kiafya ya wakazi weusi wa Alachua iliyotolewa wiki jana inashangaza na hata kusikitisha. Mbali na mambo mengine, ripoti hiyo inaonyesha kwamba:
  1. Vifo vinavyotokana na kansa viko juu kwa asilimia 24 kwa watu weusi ikilinganishwa na wazungu.

  2. Katika mwaka 2008, vifo vilivyotokana na kisukari (diabetes) vilikuwa juu kwa asilimia 211 kwa weusi ikilinganishwa na wazungu.

  3. Katika mwaka 2008, ni asilimia 60.7 tu ya akina mama weusi waliweza kupata huduma za ujauzito (prenatal care) ikilinganishwa na asilimia 78.7 kwa akinamama wa kizungu na asilimia 76.6 kwa akinamama wa kilatino.
Nilipoziona data hizi nilisikitika halafu nikamkumbuka AIKA. Popote pale tulipo, watu weusi tunaandamwa na changamoto ya kujikomboa na kuna sababu nyingi zinazosababisha hali hii - nyingine za kihistoria na kijamii - na nyingine za kujitakia. Msome na kumsikiliza Bill Cosby hapa kuhusu changamoto zinazowakabili Wamarekani weusi na mchango wao wenyewe katika kuziendeleza changamoto hizi.

Kwa sisi Afrika, mbali na mambo mengine, ukosefu wa viongozi bora na wenye uchungu na watu wao ni sababu mojawapo kuu inayolifanya bara letu tajiri liendelee kusikinika. Wamarekani weusi bado wanalaumu utumwa. Na sisi tutaendelea kulaumu ukoloni mpaka lini?

Monday, February 22, 2010

TUWAJENGEE KUMBUKUMBU NZURI WATOTO WETU

  • Haka kamalaika hapo chini kanaitwa Johari Long'hwe Matondo (kamefikisha miaka miwili jana). Wakati wa Krismasi mwaka jana kalitaka sana kupatiwa hizi blanketi zenye mikono ziitwazo "Snuggie". Na kweli kalipopata kalifurahia mno kiasi kwamba hata kulala ilikuwa shida. Natumaini kwamba taswira kama hizi zitakakumbusha baadaye kuhusu Krismasi hii iliyofana sana, pamoja na utoto wa kenyewe uliobarikiwa!
  • Ati, wewe unakumbuka nini hasa kuhusu utoto wako? Mimi nakumbuka mambo mengi yakiwemo vibano nilivyokuwa napata kutoka kwa baba mdogo (Mungu Amlaze mahali pema peponi) aliyekuwa hapendi mchezo na shule. Alikuwa hapendi kuona kosa lolote katika daftari la shule na siku hiyo kama ulikuwa umekosea swali shuleni basi ulijua kwamba kibano kikali kilikuwa kinakusubiri nyumbani.
  • Hata bado nakumbuka siku moja mbaya kabisa nilipokuwa darasa la pili au la tatu. Ilikuwa siku ya mkosi kweli kwani nilipofika shuleni tu asubuhi nikiwa nimechelewa nilikula viboko vinne. Basi kuanzia asubuhi ile viboko viliniandama na mpaka kufikia jioni nilikuwa nimefikisha viboko zaidi ya ishirini na vitano.
  • Inavyoonekana binadamu tunatunza kumbukumbu mbaya kwa umakinifu zaidi kuliko kumbukumbu nzuri. Pengine ni muhimu tujitahidi kuwapa watoto wetu kumbukumbu nzuri na upendo usiolegalega. Kuna faida nyingi za kufanya hivyo!


Sunday, February 21, 2010

Friday, February 19, 2010

NG'WANAMBITI - KUNA NINI HUKO MUSOMA???

Mataranyirato kwema?



Video Hii Inatisha: Jihadhari

FIKRA YA IJUMAA: VALENTINE DAY, MASHINDANO YA UREMBO, NOECLEXIS NA DHANA YA UZURI.


  • Jumapili iliyopita ilikuwa ni "Valentine Day". Kwetu sisi Afrika nadhani siku hii bado ina ugeni fulani. Kwa mfano, wakati nikisoma pale mlimani miaka michache tu iliyopita,, sikumbuki kuona watu wakihangaika kusherehekea hii Valentine Day. Mambo yamebadilika kwa kasi mno na siku hii sasa ni muhimu kwa wapendanao kusherehekea kwa kwenda pwani, kwenye kumbi za starehe na kwingineko. Blogu kadhaa ziliwaonya na kuwakumbusha washerehekeaji wa sikukuu hii juu ya hatari ya kuambukizana gonjwa la UKIMWI.
  • Siku hii ya wapendanao na mashindano ya urembo tunayoyashuhudia kila leo (vyote ni matokeo ya utandawazi) vimenikumbusha swali gumu ambalo limewasumbua wanafalsafa tangu enzi na enzi: Uzuri ni nini? Hili ni swali linalohusu kila kitu hapa duniani lakini leo nitatumia mifano ya washiriki wa mashindano ya urembo yaani mabinti.
  • Ni kweli kuna wazuri/warembo au pengine uzuri/urembo umo katika fikra za mtazamaji tu? Inakuwaje leo tunalazimishana kuwa na mrembo mmoja tu tena mwenye sifa zile zile za Kimagharibi- tineja, mkondefu, mrefu, mwenye miguu mchongoko na tumbo tambarare, mwenye madaha, nyanya msumari kifuani na ikiwezekana "aliyepigwa pasi"? Hebu chunguza picha hizi kwa makini halafu ufikiri tena dhana hii ya uzuri/urembo:
(1) Tunalazimishana kuamini kwamba eti mrembo ni lazima awe hivi:

(2) Huu ni uwongo kwa sababu katika jamii zingine za Kiafrika mrembo alitakiwa/anatakiwa awe hivi:

free image hostfree image host free image host

(3) Na katika jamii zingine mrembo alitakiwa/anatakiwa apambike hivi:

free image hostfree image hostfree image hostfree image host

(4) Kwa wengine, mrembo ni lazima awe amenona kama hivi:

free image hostimagebam.com

(5) Au awe na umbo namba 8 kama hili:

free image host

(6) Au mwili na sura hii ya Kihabeshi

free image host

(7) Wengine huwa hawajali umbo ali mradi kuwe na "kitu" wakipendacho!

free image hostfree image hostfree image host

(8) NOECLEXIS - Mwanamke tabia ati! Msikilize Dudubaya hapa chini.



(9) Swali: mbona tunalazimishana kwamba eti mrembo ni lazima awe hivi?

  • Na kama kila mtu ana dhana yake ya uzuri kama tulivyoona hapo juu, inawezekanaje tuwe na mzuri mmoja tu anayewakilisha dhana zote hizi? Ati, uzuri hasa ni nini? Wikiendi njema mnaposhuhudia "uzuri" uliotamalaki katika kila kitu hapa duniani!

Thursday, February 18, 2010

AFRIKA INAWEZA KUULISHA ULIMWENGU - RAIS JAKAYA KIKWETE

  • Hebu msikilize Mheshimiwa Rais Jakaya Kikwete katika "clip" hii ya dakika 1:42. Hapa ilikuwa tarehe 29/1/2010 alipokuwa akizungumza katika kongamano la Uchumi wa Dunia kule Davos nchini Switzerland.
  • Ni hotuba inayoonyesha welewa mzuri wa masuala ya msingi ambayo Afrika inahitaji katika harakati zake za kujikomboa katika sekta ya kilimo (ambayo ndiyo sekta ya msingi japo imetelekezwa) na hatimaye kuweza kujilisha yenyewe pamoja na ulimwengu mzima.
  • Kitu pekee ambacho Mheshimiwa Rais hakukitaja, na ambacho nadhani ni cha msingi kabisa, ni uongozi bora. Hata Afrika ikiwezeshwa kiteknolojia na kifedha kama anavyobainisha hapa, bila kuwa na viongozi makini na wenye moyo wa kweli wa kutaka kuwakomboa watu wao, itakuwa ni kazi bure. Ukosefu wa uongozi bora, kwa maoni yangu, ndiyo sababu mama inayoifanya Afrika iendelee kuwa katika paradoksi iliyomo - bara tajiri sana lakini lenye watu masikini sana!

MOLLEL - UJUMBE MZITO JUU YA GONJWA LA UKIMWI

  • Kwa nini maambukizi ya UKIMWI bado yanaendelea?
  • Ukimwi unaua hata wanakwaya na watunza hazina makanisani. Tafakari!

J.K.T HALIKUWA MCHEZO ATI!!!

  • Hapa ni Makutupora J.K.T Dodoma Operesheni Miaka 30 ya Uhuru. Naikumbuka siku hii kwa sababu ng'ombe wote hao walipotea kwa zaidi ya masaa sita. Kumbe walikuwa wametupiga chenga mimi na hao wachungaji wenzangu na kwenda kuparamia shamba la mizabibu tena ile myeupe. Ni stori ndefu hii, we acha tu. Maisha!

HAWA WALIWAZA NINI?????

  • Leo naingilia kipengele mashuhuri cha Mzee wa Changamoto cha Waliwaza Nini? Ati, hawa nao waliwaza nini mpaka wakaamua kuvaa nguo za aina hii? Ni fasheni au ni akili za binadamu kukosa akili? Matendo kama haya ni ya muhimu katika kumwelewa hasa binadamu ni mnyama wa aina gani.

Tuesday, February 16, 2010

SAA ZA WANASIASA ZINAPOTUMIWA KAMA FENI - UCHESHI

Jamaa mmoja alikuwa ananyosha miguu msituni jioni moja wakati wa joto kali. Mara akatokeza katika nyumba moja nzuri iliyokuwa inamilikiwa na ajuza mmoja. Nyumba hiyo ilikuwa na mkusanyiko mkubwa wa saa za ukutani.

"Saa zote hizi ni za nini?" Aliuliza yule jamaa
"Kila mtu hapa duniani ana saa yake" Alijibu yule ajuza kifalsafa na kuendelea "Kila mara unaposema uwongo, saa yako inasogea mbele kwa sekunde moja"

Yule jamaa aliona saa moja ambayo ilikuwa haisogei kabisa.
"Hii saa ni ya nani" Aliuliza kwa shauku
"Hii ni ya Mama Thereza. Haijasogea tangu iletwe hapa miaka mia moja iliyopita" Alijibu yule ajuza.
"Saa za wanasiasa ziko wapi?" Jamaa akauliza.
"Hizo huwezi kuziona hapa"Alijibu yule ajuza halafu akaendelea
"Huwa tunawagawia watu wasio na umeme wakati huu wa joto ili wakazitumie kama feni majumbani mwao"

Yule jamaa alitikisa kichwa chake na kuondoka kimya kimya bila kusema neno!

Monday, February 15, 2010

NIMEVUTIWA NA UJUMBE NYUMA YA PICHA HII

    Kwa maelezo zaidi kuhusu picha hii tembelea blogu ya mjengwa.

Saturday, February 13, 2010

PROFESA AUA WATATU NA KUJERUHI WENGINE WATATU

  • Yalipotokea kule Columbine, wahusika walikuwa ni wanafunzi. Hata kule Virginia Tech na kwingineko, wahusika walikuwa ni wanafunzi. Matukio ya matumizi ya bunduki mashuleni na vyuoni hapa Marekani bado yanaendeelea na sasa yameanza kuhusisha hata maprofesa.
  • Jana Ijumaa majira ya saa 10 jioni Profesa wa Elimu ya viumbe (Biology) - mwanamke aliyepata shahada yake ya uzamifu kutoka katika chuo kikuu mashuhuri cha Harvard - aliwatwanga risasi na kuwaua maprofesa wenzake watatu akiwemo mkuu wake wa idara. Pia aliwajeruhi watu wengine watatu - maprofesa wawili na karani.

  • Inasemekana kwamba tukio hilo lilitokea wakati waalimu hao wakiwa katika mkutano wa idara ambapo profesa anayeshukiwa aliambiwa kwamba maombi yake ya kupatiwa "tenure" yalikuwa yamekataliwa.
  • Kwa habari kamili soma hapa.

Friday, February 12, 2010

FIKRA YA IJUMAA: ATI, MSOMI NI NANI???

  • Hivi karibuni maoni mafupi ya Profesa Mbele kuhusu uzembe wa Watanzania, na uraia wa nchi mbili yalitundikwa katika blogu ya Issa Michuzi. Maoni hayo yalichangamsha watu sana na kama ilivyo kawaida, hoja za msingi ziliachwa na Profesa Mbele akaanza kuandamwa binafsi tena kwa matusi, kejeli na dhihaka (Nilishaligusia jambo hili hapa). Baada ya kuyasoma maoni hayo ya wachangiaji 76, nilianza kujiuliza maana hasa ya msomi. Ati jamani msomi ni nani? Ni lazima kuwa na shahada kuwa msomi? Vipi kuhusu babu jirani yetu kule kijijini (mganga wa kienyeji) anayefahamu karibu kila mti na matumizi yake tena bila kutumia daftari kuwekea kumbukumbu? Je, yeye ni msomi? Wewe ni msomi? Kuna faida ya kuwa msomi?
  • Hapa chini ni maoni wakilishi ya mitazamo tofauti ya wadau mbalimbali kutoka kwa Michuzi kuhusu dhana hii ya "usomi"
**************************
(1). Tarehe Tue Feb 09, 07:14:00 PM, Mtoa Maoni: Anonymous Anonymous
  • Prof, Kuhn-Tucker conditions unazijua wewe?? super and submodularity je?? Je, vipi kuhusu maximum principle na calculas of variations (CV). Niambie unawezaje kujua iwapo a twice differentaible function ni concave au ni convex!! Baada ya hapo naomba u-state transversality condition ya Infinite Horizons model!! Ukimaliza hapo nieleze matumizi na umuhimu wa ARCH and GARCH models especially as applied to high frequency financial data, kabla ya kumalizia na maelezo kuhusu procedures zilivyo katika ku-conduct augument dickey fuller test (ADF) na short comings zake. Ahsante
  • Kidokezo changu: Kwa huyu mdau, huwezi kuwa "msomi" na kuweza kuanzisha wala kushiriki mjadala kama hukusoma kozi za juu za Uchumi na hatimaye kuweza kujibu maswali anayoyauliza hapa. Sina uhakika ni watu wangapi wanaweza kuyajibu maswali haya na hivyo kuonekana "wasomi". Je, tuupime usomi wa mtu kwa kuangalia uwezo wake wa kujibu maswali tata katika taaluma yake aliyosomea? Huyu mdau akiulizwa maswali kutoka katika taaluma zingine ataweza kuyajibu? Au pengine "Economics" ni taaluma bora kuliko zingine zote?
(2). Tarehe Tue Feb 09, 12:12:00 AM, Mtoa Maoni: Anonymous Fundi_mangungo
  • Huyu ni Professor wa kiswahili, I wonder anajifanya anaijuwa siasa na uchumi! Ni miongoni mwa wale wanaodhani kujipendekeza sana kwa Kikwete basi huenda wakapata hata ubunge wa kuteuliwa!!! Nna mashaka na u professor wake! Na daima ntaendelea kuwa hivyo! Uwezo wake wa kufikiri na kujenga hoja hauna tofauti na Baba yangu aliyeshia darasa la nne la mkoloni! Of coz sikutegemea kusikia mchango wa maana kuhusu uchumi kutoka kwa Professor wa Mofimu, virai, viima na viarifu (kiswahili), lakini nilitegemea angalau anyamaze au afunguwe blog afundishe watanzania Kiswahili! Unapopiga kelele watanzania wanapiga soga wakati huna statistical data na wewe kama Professor si aibu hiyo, una tofauti gani na hao unaowalaumu (wapiga soga)...uliozungumza ni mazungumzo ya maandazi tu! Tanzania ina hasara sana kama ina Professors wa aina hii! Na kama huu ndo u professor, mungu mie usinijaalie kamwe kuwa professor!
  • Kidokezo changu: Fundi Mangungo haamini kama mtu aliyesoma lugha anaweza kuanzisha mjadala wala kutoa mchango wa kitaalamu na wa kina katika mada zingine nje ya mofimu, virai, viima na viarifu! Vipi kuhusu mtu aliyesoma Jiografia, Udaktari, Fizikia, Historia, Sayansi ya Siasa au Kemia? Anaweza kutoa mchango wowote wa maana katika mijadala nje ya uwanja wake wa kitaaluma au pengine upungufu huu ni kwa "vilaza", "ngwini" na "mbumbumbu" waliosoma lugha tu? Tazama pia maoni kama haya ya Fundi Mangungo hapa.
(3). Tarehe Tue Feb 09, 12:43:00 PM, Mtoa Maoni: Anonymous MADELA WA-MADILU
  • Professor Mbele, Heshima mbele mkuu mwenzangu. Kama una nia ya kutumwagia matusi sisi akina MADELA WA- MADILU njoo pale kwenye jamvi. Wote tuko hapa Marekani tunaganga njaa, shule tumepiga kisawasawa lakini si wote shule zetu zinafanana na kufundisha kiswahili. Hesabu za majoka (Calculus) na Ngeli wapi na wapi???

  • Kidokezo changu: Pengine kusoma hesabu za majoka (calculus) ni bora kuliko kusoma ngeli; na kufundisha hisabati ni bora kuliko Kiswahili. Pengine pia ni kweli kwamba mtu aliyesoma hesabu za majoka ni msomi kuliko aliyesoma ngeli. Na hesabu ni bora kuliko lugha!!!
*********************
Kulikuwa pia na maoni makini ambayo yalizingatia hoja. Mfano ni maoni ya Mdau Mkweli (Tue Feb 09, 01:49:00 AM) na ya mdau wa Tue Feb 09, 12:15:00 AM.
  • Turudi tena kwenye fikra yetu ya leo: Kwako wewe msomi ni nani? Unaweza pia kusoma hadithi hii fupi kuhusu dhana hii ya usomi.

JIANDIKISHE HAPA

Enter your email address:

Delivered by FeedBurner

BLOGU ZA BURUDANI NA UREMBO