NG'WANAKANUNDO - MANJU MASHUHURI WA KISUKUMA KUTOKA MWANZA

Monday, June 21, 2010

BINADAMU NA UBINADAMU WETU: SHILINGI 5,000 ZINAPOMLIZA MTU MZIMA

  • Nianze na angalizo: Lengo langu hapa siyo kujigamba wala kujionyesha bali ni kuonyesha  (kama vile ambavyo nimekuwa nikisema mara kwa mara) jinsi matendo madogo madogo ya kibinadamu yanavyoweza kuwa na athari katika maisha ya binadamu wenzetu hususan wale wenye shida. 
*********************************
  • Tarehe 9/6/2010 nilipanda daladala kutoka Masaki Mwisho kwenda Posta Mpya. Tulipofika mwisho wa safari nilishuka na kuanza kuelekea jingo la Posta Mpya. Kwa mbele yangu alikuweko mzee mmoja ambaye tulikuwa wote kwenye daladala. Mzee huyu alikuwa amevaa kandambili na nguo zilizozeeka.
  • Kwa vile kulikuwa na tope kidogo, mzee yule aliteleza kidogo na kandambili yake ya mguu wa kulia ikakatika. Nilimwangalia akiwa ameghafilika huku akiwa hajui la kufanya na wakati huo huo watu wakianza kumrushia maneno ya kuacha kuzubaazubaa na “kulivaa” tope.
  • Kwa bahati nzuri kando ya barabara kulikuwa na vijana waliokuwa wanauza fulana, magazeti, viatu (vya bei mbaya), mikanda pamoja na kandambili.
  • Nilitoa noti ya shilingi 5,000 na kumpa yule mzee na kumwambia anunue kandambili mpya. Kwa mikono miwili aliipokea ile noti na kunishukuru tena mno “Mungu Akubariki na kukuzidishia mwanangu”. Alisema huku machozi yakimlengalenga. Na kweli alikwenda na kujinunulia kandambili nyekundu mpya. Nilimtakia siku njema na  nikaendelea na mishughuliko yangu.


  • Kwangu mimi ni matendo madogo madogo kama haya ndiyo hasa yanasaidia kuupambanua ubinadamu wetu. Si ajabu mzee huyu asikisahau kitendo hiki kidogo maishani mwake kama mimi nilivyoshindwa kukisahau kitendo nilichofanyiwa na mzee mwenye kibaraghashia cheupe, kanzu nyeupe na kandambili za bluu zaidi ya miaka 17 iliyopita pale Muhimbili.
  • Hebu na tukawasaidie na kuwatendea wema binadamu wenzetu. Hakuna tendo lenye kuliwaza na kuleta furaha na ridhiko la kweli hapa duniani kama kumsaidia binadamu mwenzako hasa mwenye shida!

Saturday, June 19, 2010

MH. MALECELA NA UMASIKINI WA WATANZANIA

  • Hapa chini ni kauli ya Mheshimiwa John Malecela aliyoitoa tarehe 6/6/2010 kule wilayani Kahama alipokuwa akifungua mkutano mkuu wa Benki ya Maendeleo ya Jamii Vijijini (VICOBA). Yuko sahihi?
****************************

Akizungumzia umasikini miongoni mwa Watanzania, alisema Tanzania hakuna umasikini wa kumfanya mtu alale na njaa na kusubiri kufa.

Alisema kama kungekuwa na watu wa aina hiyo, nchi isingekuwa na amani na utulivu kama ilivyo sasa.

“Mtu hawezi kukubali kufa njaa, vinginevyo ataenda kuvunja nyumba ya mtu ye yote ili apate chakula na hapo ndipo mwanzo wa kutoweka kwa amani,” alisema.

Chanzo: Gazeti la Mwananchi la tarehe 8/6/2010 (Ukurasa wa 10)

****************************

Friday, June 18, 2010

FIKRA YA IJUMAA: DATA HIZI ZINAFIKIRISHA. TUTAFAKARI!!!


  • Kama tungepunguza ukubwa wa dunia na kuifanya iweze kukaliwa na watu 100 tu huku uwiano wa watu uliopo sasa ukibakia ule ule, mambo yangeonekana kama ifuatavyo:
*******

  1. Watu 57 wangetoka bara la Asia
  2. Watu 21 wangetoka bara la Ulaya
  3. Watu 8 wangetoka bara la Afrika
  4. Watu 52 wangekuwa wanawake
  5. Watu 48 wangekuwa wanaume
  6. Watu 70 wangekuwa si weupe (wazungu)
  7. Watu 30 wangekuwa weupe (wazungu)
  8. Watu 70 wangekuwa si Wakristo
  9. Watu 30 wangekuwa Wakristo
  10. Watu 89 wangekuwa "heterosexuals"
  11. Watu 11 wangekuwa mashoga na wasagaji
  12. Watu 6 wangemiliki asilimia 59 ya utajiri wote wa dunia, na wote sita wangetoka Marekani.
  13. Watu 80 wangeishi katika makazi duni
  14. Watu 70 wangekuwa hawajui kusoma na kuandika
  15. Watu 50 wangekuwa wanasumbuliwa na utapiamlo
  16. Mtu 1 angekuwa anakaribia kuiaga dunia
  17. Mtu 1 angekuwa anakaribia kuzaliwa
  18. Mtu 1 tu angekuwa amesoma mpaka chuo kikuu
  19. Mtu 1 tu angekuwa na kompyuta
    Chanzo: Jones, Laurie B. 2004. Teach Your Team to Fish: Using Ancient Wisdom for Inspired Teamwork. Three Rivers Place.  

Thursday, June 17, 2010

PRECISION AIRLINES WANAJITAHIDI

  • Hivi karibuni nilisafiri kutoka Mwanza kuja Dar es salaam na ndege ya Boeing 737 ya shirika la ndege la Precision. Nilifurahishwa na huduma zao nzuri (ukiachilia mbali udogo wa uwanja wa ndege wa Mwanza ambao hauchelewi kusababisha msongamano wa abiria). Ndege ilifika na kuondoka katika muda uliopangwa. Ndege ilikuwa safi na wahudumu walikuwa wachangamfu na wenye bashasha. Chakula  - sandwich moja– pia kilikuwa kizuri.
  • Kule Marekani tumezoea ukipanda ndege katika daraja la kawaida hasa katika safari fupi kama hii basi unapata kimfuko kidogo cha karanga zilizokaangwa na kutiwa chumvi na pengine maji. Ndiyo maana nilipomwona mhudumu akipita na bia za makopo za Kilimanjaro, nilimuuliza kama bia hizo zilikuwa zinauzwa. Binti yule mweusi mrefu mtanashati alicheka sana na kuniambia nimpe pesa zote nilizokuwa nazo ili akaniletee bia. Basi alibakia amesimama pale huku akisubiri nimpe pesa. Nilipomuuliza bei ya bia moja aliniambia tena kwamba nimpe pesa zote nilizokuwa nazo mfukoni mwangu. Ndipo nikajua kwamba alikuwa anatania!
  • Kama vile kunikomoa, aliondoka na kurudi na bia nne. Aliziweka katika kimeza changu, akanikaribisha kwa uchangamfu na kunijulisha kwamba kila kitu katika ndege za Precision kilikuwa bure; na kwamba nikihitaji kitu kingine cho chote basi nisisite kumwambia. Mbele yangu kulikuwa na kundi la vijana kama 6 hivi ambao walikuwa wakisafiri pamoja. Binti yule alionekana akicheka nao kwa uchangamfu mkubwa huku akiwahudumia. Hii ilikuwa mandhari ya kufurahisha kwani tumeshazoea wafanyakazi wachovu ambao muda wote huwa wamenuna. Ilikuwa mandhari nzuri!
  • Nilipendezwa sana na utani na uchangamfu wa mfanyakazi yule mrefu mtanashati. Ndege ilipotua na abiria tukaanza kutoka mfanyakazi yule aliniambia kwamba katika safari zangu zingine ni lazima nihakikishe kwamba nasafiri na Precision Airlines. Nadhani nitafanya hivyo!
Angalizo: Usije ukaniuliza nilifanya nini na zile bia nne za bure nilizoletewa! Tazama hapa kuhusu "kero" za Precision!

JIANDIKISHE HAPA

Enter your email address:

Delivered by FeedBurner

BLOGU ZA BURUDANI NA UREMBO