- Rais wetu alishawahi kulalamikiwa sana kwa safari zake za nje za mara kwa mara. Wapo waliohoji manufaa ya safari hizo kwa taifa hasa ukizingatia kwamba zinatafuna pesa nyingi za walipa kodi. Wachambuzi wengine makini waliona kwamba safari hizo zilikuwa na tija kwa taifa letu. Kutokana na utata huu, Rais mwenyewe aliamua kupunguza idadi ya "wapambe" katika misafara mbalimbali ya viongozi.
- Rais Obama naye ameweka rekodi ya kuwa rais anayesafiri sana kwa kipindi alichokaa madarakani. Yeye amevunja rekodi ya kusafiri ya maraisi wote wa nchi hiyo kwa kutumia siku 55 akiwa safarini katika kipindi cha miaka yake miwili aliyokaa madarakani. Rekodi ya mwanzo ilikuwa inashikiliwa na rais George W. Bush (II) aliyetumia siku 54 akiwa safarini nje ya nchi katika kipindi cha miaka miwili ya mwanzo ya utawala wake.
- Baadhi ya mambo yaliyoibuliwa katika safari hizi za Obama ni pamoja na ukweli kwamba dege lake la Air Force One linatafuna karibu dola 181,000 kwa saa moja!. Hizi ni pesa ambazo zinamtosha Mmarekani wa kawaida kuweza kununua nyumba nzuri ya vyumba vitatu!
- Inasemekana pia kwamba safari yake ya hivi karibuni aliyoifanya katika nchi za Asia ilikuwa inatafuna karibia dola milioni 200 kwa siku moja. Hiki ni kiasi kikubwa cha pesa hasa katika wakati huu ambapo hali ya uchumi inalegalega kiasi kwamba nyongeza ya mishahara ya wafanyakazi wote wa serikali imependekezwa kupigwa marufuku.
- Sitaki kuibua upya mjadala huu lakini nadhani "common sense" inabidi itumike na kutanguliza matakwa ya taifa mbele kwa kuepuka safari ambazo si za lazima. Agizo la rais la kupunguza wapambe katika safari hizi pia ni hatua nzuri sana ya kupunguza gharama.
- Malalamiko kuhusu safari za Obama yanapatikana hapa; na kama kawaida malalamiko haya yanatoka kwa wahafidhina wa Fox News.












































