- Huwa unajisikiaje unapomsikia mbunge wako akitoa hoja bungeni huku akichanganya Kiswahili na Kiingereza? Huwa unamwelewa? Kama huwa unamwelewa basi ni wazi kwamba unafahamu Kiingereza. Ingekuwaje kama ungekuwa hufahamu Kiingereza? Wabunge hawa wanapochanganya lugha namna hii, huwa wanafikiria kwamba kuna watu wanaowawakilisha ambao Kiingereza hawakifahamu (vizuri)? Kuna ulazima wowote kwa "waheshimiwa" hawa kuchanganya lugha namna hii? Wewe nawe huwa una tabia ya kuchanganya lugha katika mazungumzo yako? Kama jibu ni ndiyo, ni kwa nini huwa unafanya hivyo?
****************
BAKITA lawashukia wabunge
(Alhamisi, 14/4/2011)
*Wadaiwa kuwaacha wananchi hewani
*Latamani kuwafunda
*Lugha yatajwa tatizo
Na Simon Nyalobi, Jijini
BARAZA la Kiswahili la Tanzania (BAKITA) limewakumbusha wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutumia Kiswahili pekee badala ya kuchanganya na Kiingereza kwani linawafanya wananchi kutoelewa vizuri hoja zao.
Akizungumza juzi na Dar Leo Ofisini kwake, Kaimu Katibu Mtendaji wa Bakita, Noel Karekezi, alisema wabunge wanatakiwa kulitambua hilo kila wanapochangia hoja zao ili waeleweke na wananchi.
“Malalamiko yetu tangu awali ni uchanganyaji wa Kiswahili na Kiingereza. Unakuta wanajisahau kuwa wanazungumza wenyewe kumbe wanasikilizwa na wananchi wengi,” alisema.
Amesema kuchanganya lugha hizo kunawafanya wananchi kushindwa kuelewa hoja wanazozitoa na hivyo kuwataka kujifunza kutumia Kiswahili wakati wakitoa hoja zao.
Amekiri suala la uchanganyaji wa lugha hizo ni la kitaifa kutokana na mazoea yaliyojengeka katika jamii.
“Wakati mwingine tatizo la kuchanganya lugha ni gumu kuliacha kwa sababu unakuta Kiswahili unatumia nyumbani na Kiingereza unatumia ofisini,” alisema.
Ameongeza kuwa BAKITA ina azma ya kuwapa semina wabunge hao, lakini kutokana ufinyu wa bajeti wameshindwa kutimiza azma yao lakini bado wataendelea kuwakumbusha juu ya matumizi ya Kiswahili.
Katika hatua nyingine, Kaimu Katibu Mtendaji huyo amesema wahisani wengi toka nje ya nchi wamekuwa wazito kukubali kufadhili uenezwaji wa lugha ya Kiswahili kwa kile alichodai kuwa wengi wanataka lugha na tamaduni zao ziendelezwe.
- Ni kutokana na kikwazo hiki cha lugha kwamba serikali imeamru muswada tata wa katiba uandikwe katika Kiswahili kwanza ili uweze kusomwa na Watanzania walio wengi. Pengine huu ni ushahidi kwamba Kiingereza kimeshatushinda na inashangaza kidogo kuona kwamba hatufanyi lolote la maana katika kurekebisha sera yetu kengeufu ya lugha. Hata Profesa Mbele alishawahi kuombwa kuandika kwa Kiswahili kwa sababu Kiingereza hakieleweki!
- Msikilize Anna Makinda hapa akitoa ufafanuzi kuhusu suala la lugha katika muswada wa sasa wa katiba.