Ni wazi kwamba Kiingereaza kimeshatushinda, lakini je, hata Kiswahili nacho kinakaribia kutushinda? Lugha ya kufundishia ni nguzo muhimu katika mfumo wo wote ule wa elimu na kusema kweli bila kuwa na sera thabiti ya lugha ya kufundishia, elimu hugeuka na kuwa kama mchezo tu. Ni lini tutafanya marekebisho yanayotakiwa na kuhitajika sana katika sera yetu ya lugha ya kufundishia?
***********
Ni Aibu kwa Wanafunzi wa Tanzania Kufeli Kiswahili
(Ijumaa, 23/12/ 2011)
HIVI karibuni tumesikia kuwa ufaulu katika somo la Kiswahili kwa matokeo ya darasa la saba mwaka huu, umeshuka ukilinganisha na ufaulu wa somo Kiingereza.
Hali hiyo inaweza kuwashangaza watu wengi waliopo nchini kwa wanafunzi kushindwa kumudu lugha yao ya taifa.
Hasa kwakuwa inafahamika wazi kuwa Kiswahili ndiyo lugha inayotumika kama lugha ya mawasiliano kwa mwanafunzi kwa ngazi ya shule ya msingi kwa kipindi chote cha masomo kwa miaka saba, wakati Kiingereza kinafundishwa kama somo tu.
Kwa kiasi kikubwa, Watanzania wanaweza kuzungumza Kiswahili fasaha, lakini akiingia darasani kufanyia mtihani anaweza kufeli vibaya hata ukimshindanisha na mtu ambaye ni lugha yake ya tatu au ya kujifunza.
Waswahili husema “mdhaarau mwiba mguu huota tende, hayo ndiyo tunayoyaona sasa katika kiwango cha ufaulu katika somo la Kiswahili. Lakini katika ngazi ya elimu ya msingi na shule za upili Kiswahili hutumika, ili kukidhi mahitaji ya mwanafunzi katika kumjenga ili kuwa na msingi mzuri katika kufahamu vyema lugha yake.
Tukiwa tunatafakari katika matokeo hayo, yapo mambo kadhaa yanayopaswa kutazamwa na kuchukuliwa hatua ili kuepuka fedheha kwa wanafunzi kufeli somo hilo.
Hata hivyo kwa upande wa wanafunzi wa ngazi za juu ya elimu ya chuo kikuu na vyuo huwa, na rejesta zao mojawapo ni kukiona Kiswahili kuwa kigumu.
Hata hivyo usemi huo unaweza ukawa na athari chanya iwapo watu watachukua hatua kukabiliana na changamoto hiyo kwa kubaini ugumu kwake uko wapi na kushirikiana na wenzake katika kupitia mada zinazomsumbua ama asizozielewa vyema kwa msaada zaidi, ikiwa ni pamoja na kupitia maandiko mbalimbali ya wataalamu wa Kiswahili ndani na nje ya Tanzania.
Vilevile wanafunzi wa shule za msingi wanapaswa kazingatia masomo na kwa kupunguza michezo na soga pamoja na mambo yasiyo na tija pamoja na kutafuta muda wa ziada kujisomea kwa bidii ili kuyatafutia ufumbuzi yale ambayo hayakueleweka vyema wakati wa vipindi vya darasani.
Upande wa walimu wanapaswa kuendelea kufundisha somo la Kiswahili kitaaluma zaidi kuliko kufundisha kwa mazoea na kurahisisha mbinu za kufundishia kwa wanafunzi hao.
Ushirikiano huo wa walimu na wanafunzi ukiwa thabiti na kila mtu akatekeleza majukumu yake, hakuna sababu ya mwanafunzi kufeli somo la Kiswahili katika ngazi zote.
Hii ni kutokana na mambo mengi yanayoelezwa katika lugha hiyo yanahusu mazingira yaliyo karibu na mwanafunzi. Hata hadithi zinazoelezewa na watunzi wa vitabu ni kutoka mazingira hayo ambapo makabila ya Watanzania ni wazungumzaji wakubwa wa lugha ya Kiswahili.
Kwa upande wa mwenendo wa kuendelea kushuka kwa ufaulu wa mwanafunzi nchini si jambo la kuachwa kwani hiyo inadhihirisha kwamba jamii ya Watanzania hawafahamu mambo mengi katika lugha yao licha ya kuzungumza kila wakati.
Kwa hali hiyo ningetegemea kuona somo la Kiswahili linakuwa la kwanza katika ufaulu wa masomo mengine licha ya kuwa masomo mengine nayo yanafundishwa kwa lugha ya Kiswahili kwa ngazi zote kinakofundishwa.
Ipo haja ya kubaini chanzo cha wanafunzi hao kutofanya vyema katika somo hilo ikiwa ni njia ya kuelekea kupata ufumbuzi wa moja kwa moja. Lakini chanzo moja wapo ni wanafunzi kutofahamu sarufi ya lugha yao ya Kiswahili. Kwani sarufi katika lugha yoyote ndiyo uti wa mgongo wa lugha hiyo.
Kuwa na walimu wenye uzalendo na waliopikwa katika kufundisha somo la Kiswahili hilo, watumike ipasavyo katika maeneo yenye uhaba na si mwalimu yeyote anayezungumza lugha hiyo apewe nafasi ya kufundisha Kiswahili. Hilo linaweza kuwa na tija katika kuleta maendeleo ya kuinua kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari.
Jambo lingine la kuzingatia ni kuimarisha kwa kiwango cha zana za kufundishia. Huku baadhi ya walimu wamekuwa hawazingatii hilo kwa wa kwa kuona kuwa ni kupoteza muda na gharama, wakati hata zipo njia mbalimbali za kuunda zana hizo bila gharama yeyote.
Aidha katika kukabiliana na changamoto hiyo ya kuendelea kushuka kwa kiwango cha Kiswahili, pia walimu wa Kiswahili kwa umoja wao wanapaswa kuliangalia katika umoja wao walimu wa Kiswahili kwa ngazi mbalimbali.
Tunapojiandaa kuingia mwaka mpya, natumaini wanafunzi wataendelea kujizatiti ili kuhakikisha kuwa wanafanya vyema katika mitihani yao ya Kiswahili kwa mwaka unaokuja.
Walimu ambao ndiyo walezi wakuu wa wanafunzi hao, nao wanapaswa kuangalia njia nzuri za kuondokana na aibu hii ya kila mwaka kuendelea kushuka kwa ufaulu wa somo la Kiswahili.
Njia pekee ni kuwa na mipango endelevu inayoakisi maendeleo ya Kiswahili katika kukikuza na kukieneza.
Baraza la Kiswahili nchini kwa kushirikiana na taasisi za lugha ya Kiswahili nchini nalo linapaswa kutoa mchango wake kwa wanafunzi na wananchi kwa ujumla ili kukifikisha Kiswahili katika hadhi na kukitangaza nje ya Tanzania.
Mathalani, kuwapo na ushirikiano baina ya walimu wa Kiswahili na watendaji wa Baraza la Kiswahili la Taifa, kutaleta tija katika kusukuma gurudumu la maendeleo nchini.