Tuesday, December 22, 2015
Wimbo Mzuri wa Harusi (Ng'wanike Bejaga Kaya). Halafu Unaambiwa "Basukuma Dulibachangamku" Safi Sana !!!
Labels:
NYIMBO ZA HARUSI,
NYIMBO ZA KISUKUMA
Wednesday, April 29, 2015
UCHAMBUZI WA SHERIA YA MAKOSA YA MTANDAONI (2015) - SIAMINI KAMA KWELI J.K. ATAITIA SAHIHI
- Ni ukweli usiopingika kwamba tunahitaji sheria kali ya makosa ya mtandao na kusema kweli kama taifa tulikuwa tumechelewa sana ukilinganisha na wenzetu wengi hapa Afrika na kwingineko. Pamoja na ukweli huu, na kama ilivyo kawaida yetu, sheria hii muhimu inaonekana kuwa imetungwa haraka haraka tena bila kuwashirikisha walengwa (mf. mabloga) na hiyoooo imeipuliwa na kukimbizwa bungeni kidharura ikiwa bado inatokota. Matokeo yake kuna malalamiko kila kona kuhusu baadhi ya vipengele ambavyo ama vinakinzana au havieleweki ukiachilia mbali ukali wake ambao unawafanya wadau wengi waamini kuwa kama kweli itatiwa sahihi na kuachiwa ianze kufanya kazi kama ilivyo basi itabomoa kabisa uhuru wa kuhabarishana-ambao ni muhimili mmojawapo muhimu katika demokrasia yetu changa tunayojaribu kuijenga.
- Kuna ugumu gani kusikiliza malalamiko haya yanayotolewa na wadau mbalimbali na kuyafanyia kazi kama inawezekana? Mbona sheria hii inafanywa kuwa ni dharura ambayo lazima ipitishwe kabla ya uchaguzi hata bila kurekebisha makosa ya wazi ambayo yameonekana?
- Kama mimi ningekuwa ndiye mtia sahihi ningeirudisha kwa walioitunga ili wakairekebishe na kuzingatia matakwa mbalimbali ya watu wanaoathirika nayo moja kwa moja hasa wadau wa habari. Na kama kweli rais Kikwete ataitia sahihi sheria hii basi atakuwa ameharibu mojawapo ya legacy yake kubwa kabisa - uhuru wa habari. Na jambo hili litawashangaza wengi kwani katika hatua hizi za mwisho mwisho katika utawala, marais wengi huwa wanakazia macho zaidi kuhusu michango yao ya kudumu kwa watu wao na jinsi watakavyokumbukwa na historia. Wakati huu wa lala salama kamwe siyo wakati wa kupitisha maamuzi magumu na yenye utata hasa kama yanalalamikiwa sana na walengwa. Siamini kabisa kama rais huyu kijana na mwenye bashasha anataka aje akumbukwe kwa kupitisha sheria hii yenye mapungufu ya wazi na iliyojaa vipengele vinavyoweza kutumiwa vibaya na kuminya uhuru wa habari.
UTANGULIZI
Sheria hii ya Makosa ya Jinai kupitia Mtandao, 2015 ina mapungufu mengi. Mapungufu hayo yamebainika kuwa, kama sheria ikipita yanaweza kuifanya nchi ikawa ni kati nchi adui za matumizi ya mtandao wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano duniani.
Watanzania wote wanatakiwa kufahamu kuwa muswada ukipita utatumika nchini kote yani Tanzania Bara na Visiwani.
Watanzania walio wengi hawafahamu sheria hii inawahusu kwa namna gani; lakini kwa lugha rahisi ni kuwa itamuathiri mtu yeyote anayeweza tumia Mtandao wa Intaneti kwa kutumia kifaa chochote iwe kompyuta kubwa au vifaa vyenye uwezo wa kufanya kazi kama kompyuta kama Simu za mikononi, saa, televisheni na vifaa vingine vinavyoendana na hivyo.
Malengo ya Sheria hii ni kuainisha makosa yanayohusiana na matumizi ya mfumo wa kompyuta na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, kuweka utaratibu wa upelelezi, ukusanyaji na matumizi ya ushahidi wa kielektroniki na masuala mengine yanayohusiana na hayo.
Matumizi ya mitandao yote mikubwa kama Twitter, Instagram, Facebook, Barua pepe, WhatsApp, blogu na data zote zilizo katika kifaa chochote cha kielektroniki yanaathiriwa kwa kiwango kikubwa na Muswada huu.
UCHAMBUZI
Kifungu cha 7
(1-3): Hakibainishi ni aina gani za data ambazo haziruhusiwi kuguswa/kufutwa au zikiguswa/futwa ni kosa la jinai.
7(1g): Kipengele hiki katika kifungu hiki kinarudiwa mara kadhaa katika (Vifungu vya 32-35). Badala ya vifungu vya mbele kurejea kifungu hiki, watunga sheria wamekiacha kifungu hiki kikiwa hakieleweki hadi mtu asome vifungu vya mbele.
Je mtu aliyeidhinishwa katika ibara na kipengele hiki ni nani?
Kifungu cha 8:
Muswada huu haujaweka bayana iwapo nyaraka za siri zinaweza kuwekwa wazi katika mtandao kama zina maslahi ya nchi au wananchi mf. Matumizi mabovu ya pesa za umma
Kifungu cha 14:
Neno pornografia halijapewa maana na hivyo jambo lolote lenye mwonekano wa kiasherati (sexually vulgar) linaweza kutafsiriwa kama pornografia na kumuingiza mhusika matatizoni.
Ponografia ya mtandao isikatazwe kabisa ila inatakiwa kuweka ulinzi thabiti wa kuhakikisha watoto hawawezi kufungua mitandao ya aina hiyo.
Ponografia zote ni chafu lakini sio chafu zote ni ponorafia. Hivyo kutokana na kuwa sheria hii inasema ponografia zote ni chafu hii itasababisha kila mtu ahukumiwe chini ya kifungu B.
Uchafu na ponografia viwe vipengele viwili tofauti.
Kifungu cha 15:
Suala la kujifanya mtu mwingine kwenye mtandao, linaweza kuleta utata kwani kuna baadhi ya mitandao ambapo watumiaji hutumia majina ambayo sio ya kwao. Itakuwaje watu kwa madhumuni mabaya wakitafuta mtu mwenye jina kama hilo na kumshtaki mtumiaji wa mtandao?
Je, mtu kujifanya mtu mwingine inahusisha mtu kutumia jina lisilo lake hata kama hajajifanya mtu mwingine? Ni vema suala hili likafafanuliwa kisheria kwa kuwa ni suala muhimu lakini wachache wataelewa maana yake.
Kifungu cha 16:
Ni nani ana mamlaka ya kubainisha kuwa jambo lililowekwa kwenye mtandao ni la UKWELI, UONGO au UPOTOSHAJI? Ni wazi kuwa mamlaka husika inaweza tumia hili kama mtego kwa manufaa yao.
Kipengele hiki kama vingine kimeambatanisha muda usiopungua bila kusema muda usiozidi. Hivyo mtuhumiwa anaweza kufungwa hata kifungo cha maisha kutokana na mamlaka ya mahakama.
Watu binafsi wanaweza kutumia vibaya kifungu hiki kuzuia uhuru wa maoni kwa kuwaburuza watumiaji wa mtandao mahakamani kila kukicha na kuwapotezea muda wahusika ambao wanaweza kubainika mwishoni kuwa walionewa.
Kifungu cha 20:
Katika mawasililano ya mtandao kama ilivyo mawasiliano mengine kuna ujumbe ambao mtu hawezi kuacha kuupata. Mfano kutembea barabarani na kuona bango la matangazo, au kuwa ndani ya daladala iliyowasha redio.
Vivyo hivyo katika mtandao sio kila ujumbe anaopokea mpokeaji ameuomba na hivyo kifungu hiki kinafanya kila mtu atakayepokea ujumbe bila ridhaa yake kuwa amefanya kosa la jinai.
Kifungu cha 21(1):
Tafsiri za Kiswahili na kiingereza zipo tofauti kabisa.
Ya Kiswahili inamlenga Mtoa Huduma na huku ya kingereza inamlenga mtu yeyote anayetumia mtandao.
Ya Kiswahili inamlazimu mtoa huduma kumtaja mhusika aliyeweka ujumbe na pia kumuadhibu mtoa huduma huku ya kiingereza inazungumzia kuhusu tafiti kwa ujumla.
Ya kiingereza ni nzuri lakini ya Kiswahili imepotoshwa na inavunja uhuru wa mawasiliano.
MUHIMU:
Hakuna kinga yoyote kwa mtoa taarifa (source) kwa mujibu wa ibara hii.
Kifungu cha 22:
Je, nani ana mamlaka ya kuamua kuwa ujumbe kwenye mtandao unatolewa au kuboreshwa kwa kusudi au bila kusudi. Itambulike kuwa ujumbe wa kwenye mtandao huboreshwa (edit) au kufutwa wakati wowote muhusika anapoona inafaa mf. WhatsApp status, Facebook status nk.
Kifungu cha 23:
Unyayasaji wa kupitia mtandao (cyber bullying) haujapewa maana.
Sheria inatakiwa kuweka bayana maudhi ya kihisia ni nini.
Kwani mtu yeyote atakayeudhiwa ‘kihisia’ au kudai kuwa hisia zake zimeudhiwa anaweza kushtaki. Sio kila linalosababisha maudhi ya kihisia ni unyanyasaji
Kifungu cha 27
Ni nani anaamua kitendo fulani ni kula njama? Mazungumzo ya kawaida na maamuzi ya kukubalika na upande mmoja yanaweza kutafsiriwa kama kula njama na watu wa upande mwingine.
Kifungu cha 31 (3a)
Sheria ya kiingereza inasema ‘as soon as practicable’ lakini ya Kiswahili inasema wakati wa upekuzi na ukamataji wa mali. Hizi zina maana tofauti.
Ibara hii inawapa mamlaka Wakuu wa Vituo vya Polisi kufanya upekuzi na kuchukua mali (za kielektroniki) na taarifa binafsi za raia bila amri ya Mahakama.
Kifungu cha 32-35
Ibara hizi zinamlazimisha mtoa huduma kutoa data za wateja wake kwa Mkuu wa kituo cha Polisi bila kibali cha Mahakama. Wakuu wa Vituo vya Polisi wamepewa nguvu sana katika sheria hii! Mahakama ipewe mamlaka haya na si Polisi, na ifanyike hivi baada ya kujiridhisha kuwa mwananchi anatakiwa kufanyiwa upekuzi, kuchukuliwa data zake au za wateja wake n.k
Kifungu cha 39-45
Watoa huduma na wahifadhi tovuti wanalindwa na ibara hizi lakini kwa masharti.
Katika ibara ya 39, Waziri anapewa mamlaka ya kuamua kipi ni kosa na kipi si kosa. Anapewa mamlaka ya kusimamisha na kusitisha huduma, kuondoa taarifa juu ya kitendo husika (mfano kulazimisha kuondoa mijadala yote ya ufisadi fulani kama yeye ataona kwa mamlaka yake kuwa haufai kujadiliwa).
Muswada huu vifungu vya 31-38 na vifungu vya 39-46 zinakinzana kwani kwa wakati mmoja mtoa huduma anaweza akawa ameona jambo ameshalitoa na anajiandaa kuitaarifu mamlaka husika huku mamlaka husika (Askari Polisi) ikiwa na uwezo wa kwenda kuchukua vifaa na data za mtoa huduma.
Mamlaka ya Polisi imepewa kinga kubwa ambayo haiingiliani na sheria yoyote ile.
Baadhi ya Vipengele vya sheria hii ya mtandao
Kutoa taarifa za Uongo
16.- Mtu yeyote anayetoa taarifa, data au maelezo kwa njia ya picha, maandishi, alama au aina nyingine yoyote taarifa, data, kwenye m fumo wa kompyuta, endapo au maelezo hayo ni ya uongo, yanapotosha au yasiyo sahihi, atakuwa ametenda kosa, na akipatikana na hatia atalipa faini isiyopungua shilingi milioni tatu au kutumikia adhabu ya kifungo kisichopungua miezi sita au vyote.
Kwa Kiingereza:
Publication of false information
16.- Any person who publishes information, data or facts presented in a picture, text, symbol or any other form in a computer system where such information, data or fact is false, desceptive, misleading or inaccurate commits an offence, and shall on conviction be liable to a fine not less than three million shillings or to imprisonment for a term not less than six months or to both.
21.-(1) Mtoa huduma anayepokea amri kuhusiana na upelelezi wa kijinai, inayohitaji usiri, hatatoa taarifa yoyote iliyopo kwenye amri hiyo isivyo halali na makusudi.
(2) Mtu akatayekiuka kifungu kidogo cha (1) atakuwa ametenda kosa na atawajibika, iwapo atatiwa hatiani, kulipa faini isiyopungua shilingi milioni kumi au kutumikia kifungo kwa kipindi kisichopungua miaka mitatu au vyote.
Disclosure and collection of traffic data
34.-(1) where there is a reasonable ground that a computer data is required for the purpose of investigation, a police officer in charge of a police station or a law enforcement officer of a similar rank may issue an order to any person in possession of the data for-
(a) disclosure, collection or recording of the traffic data associated with a specified communication during a specified period; or
(b) permitting and assisting the law enforcement officer to collect or record that data.
(2) For the purposes of this section, “traffic data” means-
(a) information relating to communication by means of a computer system;
(b) the information generated by computer system that is part of the chain of communication; and
(c) information that shows the communication’s origin, destination, route, time, size, duration or the type of underlying service.
22. Mtu ambaye kwa makusudi na kinyume cha sheria ataharibu, atafuta, ataondoa, ataficha, atabadilisha au ataifanya data kompyuta kukosa maana kwa lengo la kuharibu ushahidi au kuchelewesha upelelezi atakuwa ametenda kosa na akitiwa hatiani atawajibika kulipa faini ya kiwango kisichopungua milioni tatu au kutumikia kifungo kwa muda usiopungua mwaka mmoja au vyote.
(2) Mtu ambaye kwa makusudi atazuia utekeleza au atashindwa kutekeleza amri iliyotolewa na sheria hii, atakuwa ametenda kosa na atawajibika, iwapo atatiwa hatiani, kulipa faini isiyopungua shilingi milioni tatu au kutumikia kifungo kwa kipindi cha kisichopungua mwaka mmoja au vyote.
Angalieni kipengele hiki pia:
Utoaji Data
32.-(1) Pale ambapo data inanitajika kuwekwa wazi kwa madhumuni ya uchunguzi wa kijinai au kuendeshwa kwa kesi mahakamani, Askari Polisi Mkuu wa kituo au afisa mtekelezaji wa sheria mwenye cheo cha askari mkuu wa kituo anaweza kutoa amri kumtaka-
(a) mtu yeyote kuwasilisha data iliyoainishwa ambayo mtu huyo anaimiliki au iliyo chini ya uangalizi wake ambayo imehifadhaiwa kwenye mfumo wa kompyuta; au
(b) mtoa huduma yeyote, kuwasilisha taarifa kuhusiana na mteja zilizo kwenye umiliki au uangalizi wake.
(2) Iwapo kitu chochote kinachohusiana na upelelezi kinajumuisha data iliyohifadhiwa kwenye mfumo wa kompyuta au kwenye kifaa, amri itachukuliwa kumtaka mtu kutoa au kuruhusu upatikanaji wa data hiyo katika namna ambayo inasomeka na inayoweza kuondolewa.
Chanzo: Global Publishers
Sheria ya Makosa ya Mtandao (2015) inapatikana HAPA
Labels:
MASUALA YA KISHERIA
Wednesday, November 21, 2012
KWA WOTE MLIOSOMA SHULE YA SEKONDARI KAHORORO ENZI ZILE. MWALIMU WETU MPENDWA MR. CHRISTIAN AGRICOLA AMEFARIKI DUNIA !!!
Picha kwa hisani ya Wanakahororo Group (FB)
Kwa mliosoma Shule ya Sekondari ya Kahororo mjini Bukoba bila shaka mtakuwa mnamkumbuka mwalimu wa Fizikia Mr. Agricola. Pengine mtakuwa mnakumbuka ule mwandiko wake maridadi ubaoni. Au lile tabasamu pana usoni mwake. Au wema wake na kutopenda kuchapa wanafunzi hovyo hovyo hata enzi zile ambapo fimbo zilikuwa ndo mfalme mashuleni. Vipi kuhusu umaridadi na uhodari wake wa kufundisha Fizikia - somo gumu, lisilo na bashasha na lisilopendwa na wanafunzi wengi? Mnakumbuka alipoanguka na baisikeli katika kona za milima ya Rugambwa akaja kutupa mchapo kuhusu madhara na athari za centrifugal force? Mnakumbuka msisitizo wake kuhusu nidhamu, maadili na kuwa watu wema maishani?
Basi Mwalimu Agricola alifariki tarehe 7 Novemba 2012 jijini Dar es salaam kwa kansa ya koo. Watu waliopata bahati ya kuongea naye siku za mwisho mwisho kabisa wakati madaktari wakiwa wameshakata tamaa walisema kuwa walishangazwa na utulivu wake na imani kuu aliyokuwa nayo. Japo alikuwa katika maumivu makali, alikuwa akitabasamu na kuwaambia kuwa wasiwe na wasiwasi kwani alikuwa na imani kubwa kwamba atapona.
Binafsi namkumbuka sana Mwalimu Agricola kwani alikuwa anapenda sana mwandiko wangu. Wakati ule tukiwa kidato cha nne na akina Matungwa Lwamwasha, Samsoni Nkaitwabo, Ngulingwa Balele, Medard Kalemani, Juma Ndekwa, Mihayo Msikhela, Edwin Kalisa, Kulwa Kindija, Tindyebwa Nkunuzi, Marko Nyanda, Bundi Sida, Shega Nkingwa, Stanslaus Ephraim .....aliwahi kunipa madaftari yenye kurasa nyingi kutokana na kuvutiwa na mwandiko wangu.
Pumzika salama mwalimu wetu mpendwa. Wanafunzi wako uliowajali na kuwapenda ndani na nje ya darasa lako la Fizikia wapo kila mahali. Na kupitia kwao, utaendelea kuishi !!!
Labels:
KUMBUKUMBU
Thursday, September 6, 2012
BINADAMU TUMEFICHWA YAJAYO !!!
- Sijui ingekuwaje kama binadamu tungejua siku na saa ya kufa kwetu. Nimelifikiria hili baada ya kuiona picha hii ya Mwangosi - mwandishi wa Channel Ten aliyeuawa na polisi (kwa bahati mbaya) kule Iringa.
- Inasemekana picha hii hapo juu ilipigwa dakika 20 tu kabla ya kifo chake cha kusikitisha. Hapa anaonekana akiendelea na shughuli zake za kupiga picha za mkutano wa Chadema bila wasiwasi. Kumbe masikini kifo nacho kilikuwa hapo pembeni tu kikimtazama...
- Pengine badala ya kulalamika na kunyong'onyea, inabidi tuamke na kushukuru kwa kila siku na saa ambayo tuko wazima hapa duniani. Ukweli ni kwamba tunaweza kuondoka wakati wo wote.
- Hebu na tukawatendee mema binadamu wenzetu ili siku tukiondoka - hata kama ni kwa ghafla na kwa kuonewa (au bahati mbaya) kama ndugu yetu Mwangosi, angalau tukaweze kukumbukwa kwa wema na ubinadamu wetu.
- Kila siku ni lazima tuwakumbatie watoto, ndugu na marafiki zetu na kuwaambia kuwa tunawapenda na kuwathamini. Ni vizuri pia kuweka hati zote za muhimu tayari tayari – urithi, bima, wosia na mengineyo tayari tayari. Safari yetu hapa duniani yaweza kukoma wakati wo wote !!!
- Pumzika salama ndugu Mwangosi. Yote ni ubatili na waliokutendea hivi (hata kama ni kwa bahati mbaya) nao siku moja watakukuta huko uliko. Duniani hapa sote tunapita tu !!!
Labels:
KIFO,
MASUALA YA KISIASA
Monday, July 16, 2012
BLOGU ZIMETUFANYA TUWE KAMA NDUGU: ASANTE DADA SUBI KWA WEMA WAKO !!!
- Kwa wanablog ambao tulianza kublog tu "kikomandoo" bila kujua cho chote kuhusu mambo ya kompyuta na mitandao, Dada Subi wa wavuti.com ni mkombozi na mlezi wetu. Kila mara tunapokwama au tunapokuwa na swali kuhusu blogu zetu hizi zisizo na wafadhili basi tunakimbilia kwake. Naye bila choyo amekuwa akitusaidia bure na bila kusita. Hata swali liwe gumu namna gani; au linalohitaji jibu la kitaalamu zaidi, yeye yuko tayari kuacha kazi zake na kusaka jibu rahisi na linaloeleweka kwa kila mtu. Na mara nyingi hubandika misaada hii kwa wanablogu katika tovuti yake pendwa ya wavuti. Ni wazi kuwa siku historia ya tovuti na blogu nchini Tanzania itakapokuja kuandikwa, jina la Dada Subi litatajwa kama mmojawapo wa watu waliosaidia sana katika kuimarisha, kutoa mwongozo na kuwasaidia wanablogu wachanga. Dada Subi, usikate tamaa wala kuchoka. Historia inakuona na siku moja itakuzawadia !!!
- Wema wa Da Subi hata hivyo hauishii katika maswala ya mitandaoni tu. Juzi juzi hapa nilipata kifurushi katika sanduku langu la posta. Nilipokifungua nilikutana na viboksi vya dawa ya Hedex - dawa pekee ambayo huninyamazishia maumivu ya kichwa kwa kasi. Kulikuwa pia na kipande cha karatasi kilichokuwa na maneno mawili tu - Dada Subi. Ndipo nikakumbuka: Akiwa kama mtaalamu wa mambo ya tiba, niliwahi kumtajia kuhusu udhaifu wa dawa nyingi za Kimarekani katika kupunguza maumivu na hasa maumivu ya kichwa. Ndipo nilimtajia kuwa dawa kiboko ya kichwa ni Hedex pekee. Kumbe angali anakumbuka.
- Japo viboksi hivi vya tembe za Hedex vyaweza kuonekana kuwa si lolote si cho chote lakini kwa hapa Marekani si jambo la kawaida mtu kukukumbuka, kuacha shughuli zake, kwenda posta na kupiga foleni ndefu na ya pole pole na kutoa pesa zake kulipia gharama za kukutumia kifurushi. Na huyu ni mtu ambaye wala hamjaonana na kufahamiana isipokuwa tu katika blogu.
- Nimeguswa sana na wema huu wa Dada Subi na kama nilivyowahi kusema HAPA, matendo ya wema kama haya, hata yakiwa ni madogo namna gani ndiyo hasa yanaonyesha ubinadamu na uhalisi wetu. Asante sana Dada Subi !!!
- Na hapa napenda kurudia tena maneno ya Mwanablogu mashuhuri Yasinta (aka Kapulya) kuwa wanablogu sisi ni ndugu. Hebu na tuendelee kusaidiana, kuelimishana, kupendana; na kuitetea, kuielimisha na kuionyesha njia jamii yetu. Tuko pamoja na Mungu Aendelee kutubariki!!!
Labels:
UBINADAMU
Subscribe to:
Posts (Atom)